Biblia Todo Logo
Biblia ya mtandaoni
- Matangazo -

Methali 15 - Swahili Revised Union Version

1 Jawabu la upole hugeuza hasira; Bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.

2 Ulimi wa mwenye hekima hutamka maarifa vizuri; Bali vinywa vya wapumbavu humwaga upumbavu.

3 Macho ya BWANA yako kila mahali; Yakimchunguza mbaya na mwema.

4 Ulimi safi ni mti wa uzima; Bali ukorofi wa ulimi huvunja moyo.

5 Mpumbavu hudharau kurudiwa na babaye; Bali yeye aangaliaye maonyo hupata busara.

6 Katika nyumba ya mwenye haki mna akiba nyingi; Bali mapato ya mtu mbaya huwa taabu tu.

7 Midomo ya mwenye haki hueneza maarifa; Bali moyo wa mpumbavu haufanyi hivyo.

8 Sadaka ya mtu mbaya ni chukizo kwa BWANA; Bali maombi ya mtu mnyofu ni furaha yake.

9 Njia ya mtu mbaya ni chukizo kwa BWANA; Bali humpenda mtu afuatiaye wema.

10 Adhabu kali ina yeye aiachaye njia; Naye achukiaye kukemewa atakufa.

11 Kuzimu na Uharibifu viko wazi mbele za BWANA; Si zaidi basi, mioyo ya wanadamu?

12 Mwenye mzaha hapendi kukaripiwa; Wala yeye hawaendei wenye hekima.

13 Moyo wa furaha huchangamsha uso; Bali kwa huzuni ya moyo roho hupondeka.

14 Moyo wa mwenye ufahamu hutafuta maarifa; Bali kinywa cha wapumbavu hula upumbavu.

15 Siku zote za mtu ateswaye ni mbaya; Bali ukunjufu wa moyo ni karamu ya daima.

16 Kuwa na mali chache pamoja na kumcha BWANA; Ni bora kuliko mali nyingi pamoja na taabu.

17 Chakula cha mboga palipo na upendo; Ni bora kuliko ng'ombe aliyenona pamoja na kuchukiana.

18 Mtu wa hasira huchochea ugomvi; Bali asiye mwepesi wa hasira hutuliza mashindano.

19 Njia ya mtu mvivu ni kama boma la miiba; Bali mapito yao wenye unyofu hufanyika njia kuu.

20 Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye; Bali mpumbavu humdharau mamaye.

21 Upumbavu ni furaha kwake aliyepungukiwa na akili; Bali mwenye ufahamu huunyosha mwenendo wake.

22 Pasipo ushauri mipango vuhunjika; Bali kwa wingi wa washauri huthibitika.

23 Mtu hulifurahia jibu la kinywa chake; Na neno linenwalo wakati wa kufaa ni jema kama nini!

24 Kwa mtu mwenye akili njia ya uhai huenda juu; Ili atoke katika kuzimu chini.

25 BWANA ataing'oa nyumba ya mwenye kiburi; Bali atauthibitisha mpaka wa mjane.

26 Ushauri mbaya ni chukizo kwa BWANA; Bali maneno yapendezayo ni safi.

27 Atamaniye faida huifadhaisha nyumba yake mwenyewe; Bali achukiaye zawadi ataishi.

28 Moyo wa mwenye haki hufikiri jinsi atakavyojibu; Bali kinywa cha wasio haki humwaga mabaya.

29 BWANA yuko mbali na wasio haki; Bali huisikia sala ya mwenye haki.

30 Mng'ao wa macho huufurahisha moyo; Habari njema huinenepesha mifupa.

31 Sikio lisikilizalo lawama yenye uhai Litakaa kati yao wenye hekima.

32 Akataaye maonyo huidharau nafsi yake mwenyewe; Bali yeye asikilizaye lawama hujipatia ufahamu.

33 Kumcha BWANA ni maonyo ya hekima; Na kabla ya heshima hutangulia unyenyekevu.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.

Bible Society of Kenya
Tufuate:



Matangazo