Biblia Todo Logo
Biblia ya mtandaoni
- Matangazo -

Methali 10 - Swahili Revised Union Version


KITABU CHA PILI Mithali za Sulemani

1 Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye; Bali mwana mpumbavu ni mzigo wa mamaye.

2 Hazina za uovu hazifaidii kitu; Bali haki huokoa na mauti.

3 BWANA hataiacha nafsi ya mwenye haki ife na njaa; Bali tamaa ya mtu mwovu huisukumia mbali.

4 Atendaye mambo kwa mkono mlegevu huwa maskini; Bali mkono wake aliye na bidii hutajirisha.

5 Akusanyaye wakati wa joto ni mwana mwenye hekima; Bali asinziaye wakati wa mavuno ni mwana mwenye kuaibisha.

6 Baraka humkalia mwenye haki kichwani; Bali jeuri hufunika kinywa chake mtu mwovu.

7 Kuwakumbuka wenye haki huwa na baraka; Bali jina la mtu mwovu litaoza.

8 Aliye na akili moyoni mwake atapokea agizo; Bali mpumbavu mwenye maneno mengi ataanguka.

9 Aendaye kwa unyofu huenda salama; Bali apotoshaye njia zake atajulikana.

10 Akonyezaye kwa jicho huleta masikitiko; Bali mpumbavu mwenye maneno mengi ataanguka.

11 Kinywa chake mwenye haki ni chemchemi ya uzima; Bali jeuri hufunika kinywa chake mtu mwovu,

12 Kuchukiana huleta fitina; Bali kupendana husitiri makosa yote.

13 Hekima hupatikana midomoni mwa mwenye ufahamu; Bali fimbo hufaa kwa mgongo wake asiye na ufahamu.

14 Watu wenye akili huweka akiba ya maarifa; Bali kinywa cha mpumbavu ni uangamivu ulio karibu.

15 Mali ya tajiri ndio ngome yake; Ufukara wa maskini ndio umwangamizao.

16 Kazi yake mwenye haki huuelekea uzima; Mazao ya wabaya huielekea dhambi.

17 Akubaliye kurudiwa huwa katika njia ya uzima; Bali yeye aachaye maonyo hukosa.

18 Yeye afichaye chuki ana midomo ya uongo, Na yeye asingiziaye ni mpumbavu.

19 Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na maovu; Bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili.

20 Ulimi wa mwenye haki ni kama fedha safi; Moyo wa mtu mbaya haufai kitu.

21 Midomo ya mwenye haki hulisha watu wengi; Bali wapumbavu hufa kwa kuwa hawana ufahamu.

22 Baraka ya BWANA hutajirisha, Wala hachanganyi huzuni nayo.

23 Kwa mpumbavu kutenda maovu ni kama mchezo; Bali mtu mwenye ufahamu ana hekima.

24 Aogopacho mtu asiye haki ndicho kitakachomjilia; Na wenye haki watapewa matakwa yao.

25 Kisulisuli kikiisha pita asiye haki hayuko tena; Bali mwenye haki ni msingi wa milele.

26 Kama siki menoni, na kama moshi machoni, Ndivyo alivyo mtu mvivu kwa hao waliomwajiri.

27 Kumcha BWANA kwaongeza siku za mtu; Bali miaka yao wasio haki itapunguzwa.

28 Matumaini yao wenye haki yatakuwa furaha; Bali matarajio yao wasio haki yatapotea.

29 Njia ya BWANA ni kimbilio lake mtu mkamilifu; Bali ni uharibifu kwao watendao maovu.

30 Mwenye haki hataondolewa milele; Bali wasio haki hawatakaa katika nchi.

31 Kinywa cha mwenye haki hutoa hekima; Bali ulimi wa ukaidi utakatiliwa mbali.

32 Midomo ya mwenye haki huyajua yatakayokubaliwa; Bali kinywa chao wasio haki hunena ukaidi.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.

Bible Society of Kenya
Tufuate:



Matangazo