Biblia Todo Logo
Biblia ya mtandaoni
- Matangazo -

Methali 13 - Swahili Revised Union Version

1 Mwana mwenye hekima husikiliza mausia ya babaye; Bali mwenye dharau hasikilizi maonyo.

2 Mtu atakula mema kwa matunda ya kinywa chake; Bali nafsi ya mtu haini itakula jeuri.

3 Yeye alindaye kinywa chake huilinda nafsi yake; Bali afunuaye midomo yake atapata uharibifu.

4 Nafsi ya mtu mvivu hutamani asipate kitu; Bali nafsi ya mwenye bidii itanenepeshwa.

5 Mwenye haki huchukia kusema uongo; Bali mtu mbaya huwa karaha, hupatwa na aibu.

6 Haki humlinda yeye aliye mnyofu katika njia yake; Bali ubaya humwangusha mwenye dhambi.

7 Kuna mtu anayejitajirisha, lakini hana kitu; Kuna anayejifanya kuwa maskini, lakini ana mali nyingi.

8 Fidia ya nafsi ya mtu ni utajiri wake; Bali mtu maskini hasikii ogofyo lolote.

9 Nuru ya mwenye haki yang'aa sana; Bali taa ya mtu mbaya itazimika.

10 Kiburi huleta mashindano tu; Bali hekima hukaa nao wanaoshauriana.

11 Mali iliyopatikana kwa haraka itapunguka; Bali yeye achumaye kidogo kidogo atazidishiwa.

12 Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua. Bali haja ya mtu ikipatikana, ni mti wa uzima.

13 Kila anayelidharau neno hujiletea uharibifu; Bali yeye anayeiogopa amri atapewa thawabu.

14 Sheria ya mwenye akili ni chemchemi ya uzima, Ili kuepukana na tanzi za mauti.

15 Ufahamu mwema huleta upendeleo; Bali njia ya muasi huangamiza.

16 Kila aliye na busara hutenda kazi kwa maarifa; Bali mpumbavu hueneza upumbavu.

17 Mjumbe mbaya huanguka maovuni; Bali mjumbe mwaminifu ni afya.

18 Umaskini na fedheha zitampata yeye akataaye kurudiwa; Bali yeye aangaliaye maonyo ataheshimiwa.

19 Haja iliyopatikana ni tamu nafsini mwa mtu; Bali kujitenga na maovu ni chukizo kwa wapumbavu.

20 Nenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; Bali rafiki wa wapumbavu ataumia.

21 Uovu huwafuatia wenye dhambi; Bali mwenye haki atalipwa mema.

22 Mtu mwema huwaachia wana wa wanawe urithi; Na mali ya mkosaji huwa akiba kwa mwenye haki.

23 Chakula kingi chapatikana kwa ukulima wa maskini; Bali viko viharibiwavyo kwa sababu ya dhuluma.

24 Yeye asiyetumia fimbo yake humchukia mwanawe; Bali yeye ampendaye humrudi mapema.

25 Mwenye haki hula akaishibisha nafsi yake; Bali tumbo la mtu mbaya litaona njaa.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.

Bible Society of Kenya
Tufuate:



Matangazo