Biblia Todo Logo
Biblia ya mtandaoni
- Matangazo -

Maombolezo 5 - Swahili Revised Union Version


Ombi la kuhurumiwa

1 Ee BWANA, kumbuka yaliyotupata; Utazame na kuiona aibu yetu.

2 Urithi wetu umegeuka kuwa mali ya wageni; Na nyumba zetu kuwa mali ya mataifa.

3 Tumekuwa yatima waliofiwa na baba; Mama zetu wamekuwa kama wajane.

4 Tumekunywa maji yetu kwa fedha; Kuni zetu twauziwa.

5 Watufuatiao wako juu ya shingo zetu; Tumechoka, tusipate pumziko lolote.

6 Tumewapa hao Wamisri mkono; Na Waashuri nao, ili tushibe chakula.

7 Baba zetu walitenda dhambi hata hawako; Na sisi tumeyachukua maovu yao.

8 Watumwa wanatutawala; Hakuna mtu wa kutuokoa na mikono yao.

9 Twapata chakula kwa kujihatarisha nafsi zetu; Kwa sababu ya upanga wa nyikani.

10 Ngozi yetu ni nyeusi kama tanuri; Kwa sababu ya joto ya njaa ituteketezayo.

11 Wanawake katika Sayuni wanashikwa kwa nguvu; Na mabikira katika miji ya Yuda.

12 Wakuu hutundikwa kwa mikono yao; Nyuso za wazee hazipewi heshima.

13 Vijana huyachukua mawe ya kusagia; Na watoto hujikwaa chini ya kuni.

14 Wazee wameacha kwenda langoni; Na vijana kwenda ngomani.

15 Furaha ya mioyo yetu imekoma; Machezo yetu yamegeuka maombolezo.

16 Taji ya kichwa chetu imeanguka; Ole wetu! Kwa kuwa tumetenda dhambi.

17 Kwa sababu hiyo mioyo yetu imezimia; Kwa ajili ya hayo macho yetu hayaoni vema.

18 Kwa ajili ya mlima Sayuni ulio ukiwa, Mbweha hutembea juu yake.

19 Wewe, BWANA, unadumu milele; Kiti chako cha enzi ni tangu kizazi hata kizazi.

20 Mbona watusahau sikuzote; Na kutuacha muda huu mwingi?

21 Ee BWANA, utugeuze kwako, nasi tutageuka; Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.

22 Ingawa wewe umetukataa kabisa; Nawe una hasira nyingi sana juu yetu.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.

Bible Society of Kenya
Tufuate:



Matangazo