Biblia Todo Logo
Biblia ya mtandaoni
- Matangazo -

Isaya 47 - Swahili Revised Union Version


Kuaibishwa kwa Babeli

1 Haya, shuka, keti mavumbini, Ewe bikira, binti Babeli; Keti chini pasipo kiti cha enzi, Ewe binti wa Wakaldayo; Maana hutaitwa tena mwororo, mpenda anasa.

2 Twaa mawe ya kusagia, usage unga; Vua utaji wako, ondoa mavazi yako, Funua mguu wako, pita katika mito ya maji.

3 Uchi wako utafunuliwa, Naam, aibu yako itaonekana. Nitalipa kisasi; simkubali mtu yeyote.

4 Mkombozi wetu, BWANA wa majeshi ndilo jina lake, Mtakatifu wa Israeli.

5 Kaa kimya, ingia gizani, Ee binti wa Wakaldayo; Maana hutaitwa tena Malkia wa falme.

6 Nilikuwa nimekasirika na watu wangu, niliutia unajisi urithi wangu, nikawatia mkononi mwako; wewe hukuwatendea rehema; kwa wazee uliifanya nira yako kuwa nzito sana.

7 Ukasema, Mimi nitakuwa malkia milele; hata hukuyatia hayo moyoni mwako, wala hukukumbuka mwisho wa mambo hayo.

8 Sasa, basi, sikia haya, wewe upendaye anasa, ukaaye na kujiona salama, wewe usemaye moyoni mwako, Mimi ndiye, wala hapana mwingine zaidi yangu mimi; sitaketi kama mjane, wala sitajua kufiwa na watoto;

9 lakini mambo haya mawili yatakupata katika dakika moja siku moja, kufiwa na watoto, na ujane; yatakupata kiasi kamili, uchawi wako ujapokuwa mwingi, na uganga wako mwingi mno.

10 Maana umeutumainia ubaya wako; umesema, Hapana anionaye; hekima yako, na maarifa yako yamekupotosha, nawe umesema moyoni mwako, Mimi ndiye, wala hapana mwingine zaidi yangu mimi.

11 Kwa sababu hiyo uovu utakupata; wala hutaweza kuuagua; na msiba utakuangukia; hutaweza kuuondoa; na ukiwa usioujua utakupata kwa ghafla.

12 Simama sasa na uganga wako, na wingi wa uchawi wako, uliojitaabisha nao tangu ujana wako; labda utaweza kupata faida, labda utaweza kushinda.

13 Umechoka kwa wingi wa mashauri yako; basi, na wasimame hao wanajimu, wazitazamao nyota, watabirio kila mwezi mambo ya mwezi huo, wakakuokoe kutoka kwa mambo yatakayokupata.

14 Tazama, watakuwa kama mabua makavu; moto utawateketeza; hawatajiokoa kutoka kwa nguvu za muali wa moto; hili halitakuwa kaa la kujipasha moto, wala moto wa kuota.

15 Ndivyo yatakavyokuwa mambo hayo uliyojitaabisha nayo; wale waliofanya biashara nawe tangu ujana wako watatangatanga mbali nawe, kila mtu akienda zake; hapatakuwa na mtu wa kukuokoa.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.

Bible Society of Kenya
Tufuate:



Matangazo