Isaya 32 - Swahili Revised Union VersionUfalme wenye haki watabiriwa 1 Tazama, mfalme atamiliki kwa haki, na wakuu watatawala kwa hukumu. 2 Na mwanadamu atakuwa kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu. 3 Tena macho yao waonao hayatakuwa na kiwi, na masikio yao wasikiao yatasikiliza. 4 Tena moyo wa mtu mwenye hamaki utafahamu maarifa, na ndimi zao wenye kigugumizi zitakuwa tayari kunena sawasawa. 5 Mpumbavu hataitwa tena muungwana, wala mlaghai hataitwa kuwa ni mheshimiwa. 6 Maana mpumbavu atanena yaliyo upumbavu, na moyo wake utafanya maovu, ili kutenda hila na kusema yasiyo kweli juu ya BWANA, ili kuziacha nafsi za watu wenye njaa bila chakula, na kuwanyima kinywaji wenye kiu. 7 Tena vyombo vyake mlaghai ni vibaya; hutunga hila mbaya, ili kuwaangamiza wanyonge kwa maneno ya uongo, mtu mhitaji ajaposema maneno yenye haki. 8 Bali muungwana huwaza mambo ya kiungwana, naye hushika sana mambo ya kiungwana. Wanawake wasiojali waonywa juu ya maafa 9 Inukeni, enyi wanawake mnaostarehe, isikieni sauti yangu; enyi binti za watu msiojali, tegeni masikio yenu msikie maneno yangu. 10 Maana mtataabishwa kwa zaidi kidogo ya mwaka, enyi wanawake mliojikinai; kwa sababu mavuno ya mizabibu yatakoma, wakati wa kuvuna vitu vya mashamba hautakuja. 11 Tetemekeni, enyi wanawake mnaostarehe; taabikeni, enyi msiokuwa na uangalifu; jivueni, jivueni nguo zenu kabisa, na kujivika nguo za magunia viunoni. 12 Watajipiga vifua kwa ajili ya mashamba mazuri, kwa ajili ya mzabibu uliozaa sana. 13 Juu ya nchi ya watu wangu itamea michongoma na mibigili; naam, juu ya nyumba za furaha katika mji ulio na shangwe; 14 maana jumba la mfalme litaachwa; mji uliokuwa na watu wengi utakuwa hauna mtu; kilima na mnara utakuwa makao ya wanyama milele, furaha ya punda mwitu, malisho ya makundi ya kondoo; 15 hata roho itakapomwagwa juu yetu kutoka juu; hata jangwa litakapokuwa shamba lizaalo sana; nalo shamba lizaalo sana litakapohesabiwa kuwa msitu. Amani ya utawala wa Mungu 16 Ndipo hukumu itakaa katika jangwa, na haki itakaa katika shamba lizaalo sana. 17 Na kazi ya haki itakuwa amani; na mazao ya haki yatakuwa ni utulivu na matumaini daima. 18 Na watu wangu watakaa katika makao ya amani; na katika maskani zilizo salama, na katika mahali pa kupumzikia penye utulivu. 19 Lakini mvua ya mawe itanyesha, wakati wa kuangushwa miti ya msituni; na huo mji utadhilika. 20 Heri ninyi mpandao mbegu kando ya maji yote, na kuiacha miguu ya ng'ombe na punda waende kokote. |
Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Bible Society of Kenya