Yoshua 16 - Swahili Revised Union VersionNchi ya Efraimu 1 Sehemu waliopewa wana wa Yusufu ilianza kutoka mto wa Yordani hapo Yeriko, hapo penye maji ya Yeriko upande wa mashariki, maana, ni hiyo nyika, kukwea kutoka Yeriko kati ya hiyo nchi ya vilima mpaka Betheli; 2 kisha ikatoka huko Betheli kwendelea Luzu, kisha ikaendelea hata kuufikia mpaka wa Waarki mpaka Atarothi; 3 kisha ikateremkia upande wa magharibi hadi kuufikia mpaka wa Wayafleti, hadi mpaka wa Beth-horoni ya chini, hadi kufikia Gezeri; na matokeo yake yalikuwa hapo baharini. 4 Na wana wa Yusufu, Manase na Efraimu, walitwaa urithi wao. 5 Na mpaka wa wana wa Efraimu kwa kufuata jamaa zao ulikuwa hivi; mpaka na urithi wao upande wa mashariki ulikuwa ni Ataroth-adari, hata Beth-horoni wa juu; 6 kisha mpaka ukatokea kwendelea upande wa magharibi huko Mikmeta upande wa kaskazini; kisha mpaka ukazunguka kwendea upande wa mashariki hata Taanath-shilo, kisha ukaendelea upande wa mashariki wa Yanoa; 7 kisha uliteremka kutoka Yanoa hadi Atarothi, na Naara, kisha ukafika Yeriko, na kutokea hapo penye mto wa Yordani. 8 Kutoka hapo Tapua mpaka ukaendelea upande wa magharibi hadi kijito cha Kana; na mwisho wake ulikuwa baharini. Huo ndio urithi wa hao wana wa Efraimu kwa kufuata jamaa zao; 9 pamoja na ile miji iliyotengwa kwa ajili ya wana wa Efraimu katikati ya urithi wa hao wana wa Manase, miji yote pamoja na vijiji vyake. 10 Nao hawakuwatoa Wakanaani waliokuwa wakikaa Gezeri; lakini hao Wakanaani waliketi kati ya Efraimu, hata hivi leo, wakawa watumishi wa kufanya kazi za shokoa. |
Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Bible Society of Kenya