Biblia Todo Logo
Biblia ya mtandaoni
- Matangazo -

Zekaria 5 - Swahili Revised Union Version


Maono ya sita: Gombo linalopuruka

1 Basi, nikainua macho yangu tena, nikaona, na tazama, gombo la kitabu lirukalo.

2 Akaniuliza, Unaona nini? Nikajibu, Naona gombo la kitabu lirukalo; na urefu wake ni dhiraa ishirini, na upana wake dhiraa kumi.

3 Ndipo akaniambia, Hii ndiyo laana itokayo kwenda juu ya uso wa nchi yote; maana kwa hiyo kila aibaye atakatiwa mbali kama ilivyoandikwa upande, na kwa hiyo kila aapaye kwa uongo atakatiliwa mbali kama ilivyo andikwa upande wa pili.

4 Nitaituma itokee, asema BWANA wa majeshi, nayo itaingia katika nyumba ya mwizi, na katika nyumba ya yeyote aapaye kwa uongo kwa jina langu; nayo itakaa katika nyumba yake, na kuiteketeza, pamoja na boriti zake na mawe yake.


Maono ya saba: Mwanamke akiwa katika kikapu

5 Ndipo yule malaika aliyesema nami akatokea, akaniambia, Inua macho yako sasa, uone ni kitu gani kitokeacho.

6 Nikasema, Ni kitu gani? Akasema, Kitu hiki ni efa itokeayo. Tena akasema, Huu ndio uovu wao katika nchi hii yote;

7 na tazama, kifuniko cha risasi kiliinuliwa; na tazama, mlikuwa na mwanamke ndani ya kikapu.

8 Akasema, Huyu ni Uovu; akamsukuma ndani ya kile kikapu; akalitupa lile jiwe la risasi juu ya mdomo wa ile efa.

9 Ndipo nikainua macho yangu, nikaona, na tazama, wanawake wawili walitokea, nao upepo ulikuwa katika mabawa yao; na mabawa yao yalikuwa kama mabawa ya korongo; wakaiinua ile efa kati ya dunia na mbingu.

10 Ndipo nikamwambia yule malaika aliyesema nami, Hawa wanaipeleka wapi efa hii?

11 Akaniambia, Wanakwenda kumjengea nyumba katika nchi ya Shinari; tena ikiisha kutengenezwa, atawekwa huko mahali pake mwenyewe.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.

Bible Society of Kenya
Tufuate:



Matangazo