Mwanzo 11 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Munara wa Babeli 1 Watu wote katika dunia walikuwa na luga moja, walitumia maneno mamoja. 2 Basi, wakati watu waliposafirisafiri toka mashariki, wakafika katika inchi ya mabonde kule Sinari, wakakaa. 3 Kisha wakaambiana: “Tufanye matofali, tuyachome kwa moto vizuri.” Walikuwa na matofali pahali pa mawe, na kabulimbo pahali pa chokaa. 4 Wakasema: “Tujijengee muji na munara ambao chongo yake itafika mbinguni kusudi tujipatie sifa, kusudi tusisambazwe katika dunia yote.” 5 Halafu Yawe akashuka chini kuona muji ule na munara ambayo wanadamu walijenga. 6 Yawe akasema: “Watu hawa ni taifa moja na wote wana luga moja; huu ni mwanzo tu wa yale watakayofanya. Jambo lolote wanalokusudia kufanya watafanikiwa. 7 Basi, tushuke chini na kuvuruga luga yao kusudi wasielewane wao kwa wao.” 8 Hivyo, Yawe akawatawanya pahali pote katika dunia, nao wakaacha kujenga ule muji. 9 Muji ule ukaitwa Babeli, kwa sababu kule ndiko Yawe alikovuruga luga ya dunia yote, na tokea kule akawatawanya watu kila pahali katika dunia. Wazao wa Semu 10 Hawa ndio wazao wa Semu. Miaka miwili nyuma ya yale mafuriko ya maji, Semu akiwa na umri wa miaka mia moja, alizaa Aripakisadi. 11 Nyuma ya kuzaa Aripakisadi, Semu aliishi miaka mia tano, na kupata wana wengine na wabinti. 12 Aripakisadi alipokuwa na umri wa miaka makumi tatu na mitano, akazaa Sela. 13 Nyuma ya kuzaa Sela, Aripakisadi aliishi miaka mia ine na mitatu, na kupata wana wengine na wabinti. 14 Sela alipokuwa na umri wa miaka makumi tatu, alizaa Eberi. 15 Kisha kuzaa Eberi, Sela aliishi miaka mia ine na mitatu, na kupata wana wengine na wabinti. 16 Eberi alipokuwa na umri wa miaka makumi tatu na mine, akazaa Pelegi. 17 Kisha kuzaa Pelegi, Eberi aliishi miaka mia ine na makumi tatu, na kupata wana wengine na wabinti. 18 Pelegi alipokuwa na umri wa miaka makumi tatu, akazaa Reu. 19 Kisha kuzaa Reu, Pelegi aliishi miaka mia mbili na tisa, na kupata wana wengine na wabinti. 20 Reu alipokuwa na umri wa miaka makumi tatu na miwili, akazaa Serugi. 21 Kisha kuzaa Serugi, Reu aliishi miaka mia mbili na saba, na kupata wana wengine na wabinti. 22 Serugi alipokuwa na umri wa miaka makumi tatu, akazaa Nahori. 23 Kisha kuzaa Nahori, Serugi aliishi miaka mia mbili, na kupata wana wengine na wabinti. 24 Nahori alipokuwa na umri wa miaka makumi mbili na tisa, akazaa Tera. 25 Kisha kuzaa Tera, Nahori aliishi miaka mia moja kumi na tisa, na kupata wana wengine na wabinti. 26 Tera alipokuwa na umri wa miaka makumi saba, akazaa Abramu, Nahori, na Harani. Wazao wa Tera 27 Hawa ndio wazao wa Tera, baba ya Abramu, Nahori na Harani. Harani alikuwa baba ya Loti. 28 Huyo Harani alikufa wakati baba yake Tera alikuwa anaishi kule Uri, muji wake wa kuzaliwa. 29 Abramu na Nahori wakaoa. Muke wa Abramu aliitwa Sarai. Muke wa Nahori aliitwa Milka, binti ya Harani ambaye vilevile alikuwa baba ya Isika. 30 Sarai hakukuwa na mutoto kwa sababu alikuwa tasa. 31 Tera akatwaa Abramu mwana wake, Loti mujukuu wake aliyekuwa mwana wa Harani, na Sarai muke wa Abramu, wakaondoka wote pamoja toka Uri, muji wa Wakaldea, na kwenda katika inchi ya Kanana. Lakini walipofika Harani, wakakaa pale. 32 Tera akakufia kule Harani akiwa na umri wa miaka mia mbili na mitano. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo