Biblia Todo Logo
線上聖經

- 廣告 -

Marko 15 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Yesu mbele ya Pilato
( Mat 27.1-2 , 11-14 ; Lk 23.1-5 ; Yn 18.28-38 )

1 Asubui mapema, mara moja wakubwa wa makuhani wakafanya shauri pamoja na wasimamizi wa watu, walimu wa Sheria na wakubwa wote wa baraza. Wakamufunga Yesu, wakamupeleka na kwenda kumutoa kwa Pilato.

2 Pilato akamwuliza Yesu: “Wewe ni Mufalme wa Wayuda?” Yesu akamujibu: “Umesema.”

3 Nao wakubwa wa makuhani wakamushitaki Yesu juu ya mambo mengi.

4 Basi Pilato akamwuliza tena: “Wewe haujibu hata neno? Angalia mambo haya yote wanayokushitakia!”

5 Lakini Yesu hakujibu neno lolote tena, hata Pilato akashangaa.


Yesu anahukumiwa kufa
( Mat 27.15-26 ; Lk 23.13-25 ; Yn 18.39–19.16 )

6 Kila sikukuu ya Pasaka, Pilato alizoea kuwafungulia watu mufungwa mumoja, yule waliyemutaka.

7 Kulikuwa mufungwa mumoja, jina lake Baraba, aliyefungwa pamoja na waasi wamoja kwa sababu ya uuaji na uasi walioufanya.

8 Watu wakamwendea Pilato, wakaanza kumwomba awatendee kama ilivyokuwa desturi yake.

9 Pilato akawajibu, akiwauliza: “Munataka niwafungulie ‘Mufalme wa Wayuda?’ ”

10 Alisema vile kwa maana alitambua kwamba wakubwa wa makuhani wamemutoa Yesu kwa sababu walimwonea wivu tu.

11 Lakini wakubwa wa makuhani wakawachochea watu wamwombe Pilato awafungulie Baraba.

12 Pilato akawauliza watu tena: “Basi munataka nifanye nini na huyu munayemwita Mufalme wa Wayuda?”

13 Wakapiga kelele tena wakisema: “Atundikwe juu ya musalaba!”

14 Pilato akawauliza: “Alifanya ubaya gani?” Lakini wakazidi kupiga kelele wakisema: “Atundikwe juu ya musalaba!”

15 Kwa kuwa Pilato alitaka kuwapendeza watu, basi akawafungulia Baraba. Na kisha kuamuru wamupige Yesu fimbo, akamutoa kusudi atundikwe juu ya musalaba.


Waaskari wanamuchekelea Yesu
( Mat 27.27-31 ; Yn 19.2-3 )

16 Waaskari wakamupeleka Yesu ndani ya upango wa nyumba ya liwali, nao wakaita kundi lao lote wakusanyike.

17 Wakamuvalisha Yesu nguo nyekundu, na wakasokota taji na tawi lenye miiba na kumuvalisha nalo juu ya kichwa.

18 Kisha wakaanza kumusalimia, wakisema: “Jambo, Mufalme wa Wayuda!”

19 Wakamupigapiga tete juu ya kichwa, wakamutemea mate, wakapiga magoti na kuinama mbele yake.

20 Walipokwisha kumuchekelea, wakamuvua ile nguo nyekundu na kumuvalisha nguo zake. Kisha wakaondoka naye inje kwa kwenda kumutundika juu ya musalaba.


Yesu anatundikwa juu ya musalaba
( Mat 27.32-44 ; Lk 23.26-43 ; Yn 19.17-27 )

21 Mutu mumoja wa Kurene, aliyeitwa Simoni, baba ya Alesanduro na Rufu, alikuwa akipita katika njia, akitoka kwenye vijiji. Waaskari wakamushurutisha abebe musalaba wa Yesu.

22 Wakamufikisha Yesu kwenye pahali palipoitwa Golgota, maana yake “Kilima cha Mufupa wa Kichwa.”

23 Wakamupa divai iliyochanganywa na manemane, lakini akaikataa.

24 Kisha wakamutundika juu ya musalaba, wakagawanyana nguo zake kwa kuzipigia kura, kusudi wajue nguo gani kila mumoja atakazopaswa kutwaa.

25 Ilikuwa saa tatu ya asubui wakati walipomutundika juu ya musalaba.

26 Na tangazo hili liliandikwa kwa kuonyesha sababu ya kuhukumiwa kwake. “Mufalme wa Wayuda.”

27 Vilevile waliwatundika wanyanganyi wawili juu ya misalaba pamoja na Yesu, mumoja kwa upande wake wa kuume na mwingine kwa upande wa kushoto. [

28 Maandiko Matakatifu yanayosema hivi yakatimizwa: “Alihesabiwa pamoja na watenda mabaya.”]

29 Watu waliokuwa wakipita pale walimutukana na kutikisatikisa vichwa vyao, wakisema: “Ewe! Wewe uliyetaka kubomoa hekalu na kujenga lingine katika siku tatu,

30 ujiokoe sasa mwenyewe, ukijishusha juu ya musalaba!”

31 Vilevile wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria kati yao walimusimanga Yesu, wakisemezana: “Aliokoa wengine, lakini sasa anashindwa kwa kujiokoa yeye mwenyewe!

32 Kristo, Mufalme wa Waisraeli, ajishushe sasa juu ya musalaba, kusudi nasi tupate kuona na kumwamini.” Hata wale waliotundikwa pamoja naye walimutukana vilevile.


Kufa kwa Yesu
( Mat 27.45-56 ; Lk 23.44-49 ; Yn 19.28-30 )

33 Ilipokuwa saa sita ya muchana, giza likakuwa katika inchi yote mpaka saa tisa.

34 Na saa tisa Yesu akalalamika: “Eloi, Eloi, lama sabaktani” maana yake “Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniacha?”

35 Na watu wamoja waliokuwa pale walipomusikia, wakasema: “Musikilize, anamwita Elia.”

36 Na mumoja wao akaenda mbio, akachovya kikausho ndani ya divai yenye kuchacha na kukifungia juu ya tete. Kisha akakipandishia Yesu, kusudi apate kunywa, akisema: “Mwache tuone kama Elia atakuja kumushusha juu ya musalaba.”

37 Lakini Yesu akalalamika kwa sauti kubwa, akakata roho.

38 Basi pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu mpaka chini.

39 Mukubwa wa waaskari aliyekuwa akisimama mbele ya Yesu, alipoona namna alivyokata roho, akasema: “Hakika mutu huyu alikuwa Mwana wa Mungu!”

40 Kulikuwa wanawake wamoja walioangalia kwa mbali. Kati yao kulikuwa Maria wa Magdala, Maria mama ya kijana Yakobo na Yose na mwanamuke mwingine Salome.

41 Wanawake hawa ni wale waliomufuata Yesu na kumushugulikia wakati alipokuwa Galilaya. Wanawake wengine wengi waliomufuata mpaka Yerusalema walikuwa pale vilevile.


Kuzikwa kwa Yesu
( Mat 27.57-61 ; Lk 23.50-56 ; Yn 19.38-42 )

42-43 Ilipokwisha kuwa magaribi, Yosefu wa Arimatea, akafika kwa Pilato. (Yosefu alikuwa mutu mwenye heshima katika Baraza Kubwa, na vilevile alikuwa akitazamia kuja kwa Ufalme wa Mungu). Siku ile ilikuwa ya matayarisho ya siku ya Sabato iliyofuata. Kwa hiyo Yosefu akaenda bila woga kwa Pilato kwa kumwomba maiti ya Yesu.

44 Pilato akashangaa sana kusikia kwamba Yesu amekwisha kufa. Basi akamwita yule mukubwa wa waaskari na kumwuliza kama kumepita muda murefu tangia Yesu alipokufa.

45 Alipokwisha kuhakikishwa na yule mukubwa wa waaskari kwamba Yesu amekwisha kufa, akamuruhusu Yosefu atwae maiti yake.

46 Yosefu akanunua vitambaa, akaondoa maiti ya Yesu juu ya musalaba, akaifungafunga na vile vitambaa na kuiweka ndani ya kaburi lililochimbwa ndani ya jiwe. Kisha wakasukumia jiwe kwenye kiingilio cha lile kaburi.

47 Maria wa Magdala na Maria mama ya Yose walikuwa wakiangalia, pahali walipomuzika Yesu.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
跟著我們:



廣告