Biblia Todo Logo
線上聖經

- 廣告 -

Hesabu 5 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Watu wenye uchafu

1 Yawe akamwambia Musa:

2 Uwaamuru Waisraeli wamutoe inje ya kambi kila mutu mwenye ukoma, kila mutu anayetokwa usaha, na kila anayekuwa muchafu kwa kugusa maiti.

3 Mutawatoa inje ya kambi watu wote hawa, wanaume na wanawake, kusudi wasichafue kambi yangu ninamokaa.

4 Waisraeli wakafanya hivyo, wakawafukuza inje ya kambi. Kama vile Yawe alivyomwambia Musa, ndivyo Waisraeli walivyofanya.


Malipo ya makosa

5 Kisha Yawe akamwambia Musa:

6 Uwaambie Waisraeli kwamba: Mutu yeyote, mwanaume au mwanamuke, akimukosea mwenzake, yeye anatenda zambi mbaya mbele ya Yawe.

7 Anapaswa kutubu zambi yake aliyotenda; na atatoa malipo kamilifu kwa kosa lake, akiongeza asilimia makumi mbili ya malipo hayo; atatoa malipo hayo kwa yule aliyemukosea.

8 Lakini ikiwa mutu huyo amekufa na hana ndugu wa karibu ambaye anaweza kupokea malipo hayo, basi, malipo ya kosa yatatolewa kwa Yawe kwa ajili ya makuhani; malipo haya ni pamoja na kondoo dume wa upatanisho ambaye atatumiwa kwa kumufanyia upatanisho kwa ajili ya zambi yake.

9 Kila sadaka ya matoleo yote matakatifu ya Waisraeli watakayomuletea kuhani, itakuwa yake.

10 Na kila kitu kitakatifu cha mutu kitakuwa cha kuhani; kitu chochote mutu anachomutolea kuhani kitakuwa chake.


Maneno ya wake wasiokuwa waaminifu kwa waume zao

11 Yawe akamwambia Musa:

12 Uwaambie Waisraeli: Kama muke wa mutu yeyote amepotoka na kukosa uaminifu kwa mume wake,

13 akilala na mutu mwingine bila mume wake au mutu mwingine yeyote kujua; amejichafua ingawa hakuna mutu aliyeshuhudia kitendo chake kwa sababu hakukamatwa.

14 Lakini, mume wake akiingiwa na shaka na kuwa na wivu juu ya muke wake aliyejichafua; au kama amekuwa na wivu juu ya muke wake ingawa muke wake hakujichafua,

15 basi wote wawili watakwenda kwa kuhani na kupeleka sadaka inayotakiwa, ni kusema sehemu ya kumi ya unga wa shayiri; lakini bila kuitia mafuta au ubani, kwa sababu ni sadaka ya vyakula ya mume anayekuwa na wivu kwa muke wake, kwa ukumbusho wa kosa.

16 Kuhani atamupeleka huyo mwanamuke karibu, na kumusimamisha mbele ya Yawe.

17 Kisha, atamimina maji matakatifu katika chombo cha udongo na atatwaa vumbi inayokuwa chini ndani ya hema takatifu na kuitia katika maji hayo kwa kuyafanya machungu.

18 Kuhani atamuweka mbele ya Yawe na kumufunua nywele na kumupa sadaka hiyo ya vyakula inayotolewa kwa sababu ya wivu wa mume wake. Kuhani mwenyewe atashikilia kile chombo chenye maji machungu yanayoleta laana.

19 Halafu kuhani atamwapisha mwanamuke huyo akisema: Ikiwa haukulala na mwanaume mwingine na kujichafua wakati uko chini ya mamlaka ya mume wako, basi, hautapatwa na laana inayoletwa na maji haya machungu.

20 Lakini kama umepotoka wakati uko chini ya mamlaka ya mume wako, na kujichafua kwa kulala na mwanaume mwingine asiyekuwa mume wako,

21 Yawe akuazibu hata ukuwe laana na kiapo kati ya watu wako, ukuwe tasa na tumbo lako livimbe.

22 Maji haya yanayoleta laana yaingie ndani ya tumbo lako na kukufanya tasa na tumbo lako livimbe. Naye mwanamuke ataitikia: Amina! Amina!

23 Kisha kuhani ataandika laana hizi katika kitabu na kuzisafisha katika maji machungu.

24 Atamukunywesha mwanamuke hayo maji machungu yanayaleta laana nayo yataingia ndani yake na kumuletea maumivu makali.

25 Kisha kuhani atatwaa ile sadaka ya vyakula ya wivu katika mikono ya mwanamuke huyo na kuitikisa mbele ya Yawe, na kuipeleka juu ya mazabahu.

26 Halafu, atatwaa mukono mumoja wa sadaka hiyo ya vyakula kwa ukumbusho na kuiteketeza juu ya mazabahu. Kisha atamukunywesha mwanamuke maji hayo.

27 Akisha kunywa, kama amejichafua na hakukuwa mwaminifu kwa mume wake maji hayo yanayoleta laana yataingia ndani ya matumbotumbo yake na kuwa machungu, na tumbo lake litavimba naye atakuwa tasa. Mwanamuke huyo atakuwa laana kati ya watu wake.

28 Lakini kama mwanamuke huyo hajajichafua na hana kosa, basi hatapatwa na hasara na ataweza kupata watoto.

29 Basi, hii ndiyo sheria kuelekea maneno ya wivu kama mwanamuke akiwa chini ya mamlaka ya mume wake, anapotoka na kujichafua,

30 au wakati mwanaume anaposhikwa na wivu na kuwa na mashaka na muke wake. Atamusimamisha mwanamuke huyo mbele ya Yawe, na kuhani atatimiza masharti yote ya sheria hii.

31 Mume wake hatakuwa na kosa lolote, lakini mwanamuke atabeba lazima ya uovu wake.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
跟著我們:



廣告