Biblia Todo Logo
Biblia ya mtandaoni
- Matangazo -

Hosea 11 - Swahili Revised Union Version


Huruma za Mungu kwa Israeli

1 Israeli alipokuwa mtoto, nilikuwa nikimpenda, nikamwita mwanangu atoke Misri.

2 Kadiri walivyowaita ndivyo walivyoondoka na kuwaacha; waliwatolea dhabihu Mabaali, na kuzifukizia uvumba sanamu za kuchonga.

3 Lakini nilimfundisha Efraimu kwenda kwa miguu; niliwachukua mikononi mwangu; hawakujua ya kuwa niliwaponya.

4 Niliwavuta kwa kamba za kibinadamu, kwa mafungo ya upendo; nami nilikuwa kwao kama hao waondoao kongwa tayani mwao, nikaandaa chakula mbele yao.

5 Hatarudi tena nchi ya Misri; bali huyo Mwashuri atakuwa mfalme wake; kwa sababu walikataa kurejea.

6 Na upanga utaiangukia miji yake, utayaharibu makomeo yake na kuyala, kwa sababu ya mashauri yao wenyewe.

7 Na watu wangu wamejipinda kuniacha; ingawa wawaita kwenda kwake Aliye Juu, hapana hata mmoja atakayemtukuza.

8 Niwezeje kukuacha, Efraimu? Niwezeje kukuachilia Israeli? Niwezeje kukufanya kama Adma? Niwezeje kukuweka kama Seboimu? Moyo wangu umegeuka ndani yangu, huruma zangu zimewaka pamoja.

9 Sitatumia ukali wa hasira yangu, sitamwangamiza Efraimu tena; kwa maana mimi ni Mungu, si mwanadamu mimi; mimi ndiye aliye Mtakatifu katikati yenu; wala sitaingia ndani ya mji.

10 Watakwenda kumfuata BWANA, atakayenguruma kama simba; kwa maana atanguruma, nao watoto watakuja kutoka magharibi wakitetemeka.

11 Watakuja wakitetemeka kama shomoro, toka Misri, na kama hua, toka nchi ya Ashuru; nami nitawakalisha katika nyumba zao, asema BWANA.

12 Efraimu amenizunguka kwa maneno ya uongo, na nyumba ya Israeli kwa udanganyifu; na Yuda hata sasa anasitasita kwa Mungu, na kwake aliye Mtakatifu, naye ni mwaminifu.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.

Bible Society of Kenya
Tufuate:



Matangazo