Biblia Todo Logo
Biblia ya mtandaoni
- Matangazo -

Zaburi 143 - Swahili Revised Union Version - SRUVDC


Sala ya ukombozi kutoka kwa adui Zaburi ya Daudi.

1 Ee BWANA, uisikie sala yangu, uzisikilize dua zangu Unijibu Kwa uaminifu wako, Unijibu kwa haki yako.

2 Wala usimhukumu mtumishi wako, Maana kwako hakuna aliye hai mwenye haki.

3 Maana adui ameifuatia nafsi yangu, Ameutupa chini uzima wangu. Amenikalisha mahali penye giza, Kama watu waliokufa zamani.

4 Na roho yangu imezimia ndani yangu, Moyo wangu ndani yangu umeshtuka.

5 Nimezikumbuka siku za kale, Nimeyatafakari matendo yako yote, Naziwaza kazi za mikono yako.

6 Nakunyoshea mikono yangu; Nafsi yangu inakuonea kiu kama nchi kame.

7 Ee BWANA, unijibu hima, roho yangu imelegea; Usinifiche uso wako, Nisifanane nao washukao shimoni.

8 Uniwezeshe kusikia fadhili zako asubuhi, Kwa maana nimekutumaini Wewe. Unifundishe njia nitakayoiendea, Kwa maana ninakuinulia nafsi yangu.

9 Ee BWANA, uniponye kutoka kwa adui zangu; Nimekukimbilia Wewe, unifiche.

10 Unifundishe kuyatenda mapenzi yako, Kwa maana ndiwe Mungu wangu; Roho yako mwema aniongoze katika njia iliyo sawa,

11 Ee BWANA, uniponye kwa ajili ya jina lako, Kwa haki yako unitoe roho yangu taabuni;

12 Kwa fadhili zako utawakatilia mbali adui zangu; Na kuwaangamiza wote wanitesao nafsi, Kwa maana mimi ni mtumishi wako.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.

Bible Society of Kenya
Tufuate:



Matangazo