Biblia Todo Logo
Biblia ya mtandaoni

- Matangazo -

Wagalatia 4 - Swahili Revised Union Version - SRUVDC

1 Lakini nasema ya kuwa mrithi, wakati wote awapo mtoto, hana tofauti na mtumwa, ingawa ni bwana wa yote;

2 bali yuko chini ya mawakili na watunzaji, hadi wakati uliokwisha kuamriwa na baba.

3 Kadhalika na sisi, tulipokuwa watoto, tulikuwa tukitumikishwa na kawaida za kwanza za dunia.

4 Lakini ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria,

5 kusudi awakomboe hao waliokuwa chini ya sheria, ili sisi tupate kupokea hali ya kuwa wana.

6 Na kwa kuwa ninyi mmekuwa wana, Mungu alimtuma Roho wa Mwanawe mioyoni mwetu, aliaye, Aba, yaani, Baba.

7 Kama ni hivyo, wewe si mtumwa tena bali u mwana; na kama u mwana, basi, u mrithi kwa Mungu.


Paulo awashutumu Wagalatia

8 Lakini wakati ule, kwa kuwa hamkumjua Mungu, mliwatumikia wao ambao kwa asili si miungu.

9 Bali sasa mkiisha kumjua Mungu, au zaidi kujulikana na Mungu, kwa nini kuyarejea tena mafundisho ya kwanza yaliyo manyonge, yenye upungufu, ambayo mnataka kuyatumikia tena?

10 Mnashika siku, na miezi, na nyakati, na miaka.

11 Nawachelea, isiwe labda nimejitaabisha bure kwa ajili yenu.

12 Ndugu zangu, nawasihi, iweni kama mimi, maana mimi ni kama ninyi. Hamkunidhulumu kwa lolote.

13 Lakini mwajua ya kuwa niliwahubiria Injili mara ya kwanza kwa sababu ya udhaifu wa mwili;

14 na jaribu lililowapata katika mwili wangu hamkulidharau wala kulikataa, bali mlinipokea kama malaika wa Mungu, kama Kristo Yesu.

15 Kuko wapi, basi, kule kujiita heri? Maana nawashuhudu kwamba, kama ingaliwezekana, mngaling'oa macho yenu, mkanipa mimi.

16 Je! Nimekuwa adui yenu kwa sababu nawaambia yaliyo kweli?

17 Hao wana shauku nanyi, lakini si kwa nia nzuri, bali wanataka kuwafungia nje, ili kwamba ninyi mwaonee wao shauku.

18 Navyo ni vizuri kuonewa shauku katika neno jema sikuzote, wala si wakati nikiwapo mimi pamoja nanyi tu.

19 Watoto wangu wadogo, ambao nawaonea uchungu tena mpaka Kristo aumbike ndani yenu;

20 laiti ningekuwapo pamoja nanyi sasa, na kuigeuza sauti yangu! Maana naona shaka kwa ajili yenu.


Mfano wa Hajiri na Sara

21 Niambieni, ninyi mnaotaka kuwa chini ya sheria, je! Hamwisikii sheria?

22 Kwa maana imeandikwa ya kuwa, Abrahamu alikuwa na wana wawili mmoja kwa mjakazi, na mwingine kwa mwanamke huru.

23 Lakini yule wa mjakazi alizaliwa kwa mwili, yule wa mwanamke huru kwa ahadi.

24 Mambo haya husemwa kwa mfano; kwa maana hawa ndio kama maagano mawili, moja kutoka mlima Sinai, lizaalo kwa utumwa, ambalo ni Hajiri.

25 Maana Hajiri ni kama mlima Sinai ulioko Arabuni, umelingana na Yerusalemu wa sasa; kwa kuwa yuko utumwani pamoja na watoto wake.

26 Bali Yerusalemu wa juu ni muungwana, naye ndiye mama yetu sisi.

27 Kwa maana imeandikwa, Furahi, wewe uliye tasa, usiyezaa; Paza sauti, ulie, wewe usiye na uchungu; Maana watoto wake aliyeachwa pekee ni wengi Kuliko wa huyo aliye na mume.

28 Basi, ndugu zangu, kama Isaka sisi tu watoto wa ahadi.

29 Lakini kama vile siku zile yule aliyezaliwa kwa mwili alivyomwudhi yule aliyezaliwa kwa Roho, ndivyo ilivyo na sasa.

30 Lakini lasemaje andiko? Mfukuze mjakazi na mwanawe, kwa maana mwana wa mjakazi hatarithi kabisa pamoja na mwana wa muungwana.

31 Kwa hiyo, ndugu zangu, sisi si watoto wa mjakazi, bali tu watoto wa huyo aliye muungwana.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.

Bible Society of Kenya
Tufuate:



Matangazo