Biblia Todo Logo
Biblia ya mtandaoni

- Matangazo -

Hesabu 35 - Swahili Revised Union Version - SRUVDC


Miji kwa makuhani

1 Kisha BWANA akanena na Musa katika nchi tambarare za Moabu, karibu na mto wa Yordani, hapo Yeriko, akamwambia,

2 Uwaagize wana wa Israeli wawape Walawi miji wapate mahali pa kukaa, katika milki yao; pamoja na malisho yaliyoizunguka hiyo miji kotekote mtawapa Walawi.

3 Hiyo miji watakuwa nayo ili wakae humo, na malisho watakuwa nayo kwa wanyama wao wa mifugo, na kwa mali zao, na kwa wanyama wao wote.

4 Na yale malisho ya miji mtakayowapa Walawi, ukubwa wake utakuwa tangu ukuta wa mji kupima kiasi cha dhiraa elfu pande zote.

5 Nanyi mtapima hapo nje ya mji upande wa mashariki dhiraa elfu mbili, na upande wa kusini dhiraa elfu mbili, na upande wa magharibi dhiraa elfu mbili, na upande wa kaskazini dhiraa elfu mbili, huo mji ulio katikati. Hayo ndiyo yatakayokuwa kwao malisho ya miji.

6 Na hiyo miji mtakayowapa Walawi, itakuwa miji sita ya kukimbilia, mtakayoweka kwa ajili ya mwenye kumwua mtu, ili akimbilie huko; pamoja na hiyo mtawapa miji arubaini na miwili zaidi.

7 Miji yote mtakayowapa hao Walawi jumla yake itakuwa miji arubaini na minane; mtawapa miji hiyo pamoja na malisho yake.

8 Tena katika miji mtakayotoa ya hiyo milki ya wana wa Israeli, katika hao walio wengi mtatwaa miji mingi; na katika hao walio wachache mtatwaa miji michache; kila mtu kama ulivyo urithi wake atakaourithi, atawapa Walawi katika miji yake.


Miji ya makimbilio

9 Kisha BWANA akanena na Musa, na kumwambia,

10 Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Mtakapovuka mto wa Yordani na kuingia nchi ya Kanaani,

11 Ndipo mtajiwekea miji itakayokuwa ya makimbilio kwa ajili yenu; ili kwamba mwenye kumwua mtu, pasipo kukusudia kumwua, apate kukimbilia huko.

12 Na hiyo miji itakuwa kwenu kuwa makimbilio, kumkimbia mwenye kulipiza kisasi, ili asiuawe mwenye kumwua mtu, hata atakaposimama mbele ya mkutano ahukumiwe.

13 Na hiyo miji mtakayowapa itakuwa kwenu ni miji sita ya kukimbilia.

14 Mtawapa miji mitatu ng'ambo ya pili ya Yordani, na miji mitatu mtawapa katika nchi ya Kanaani; miji hiyo itakuwa ni miji ya makimbilio.

15 Miji hiyo sita itakuwa pa kukimbilia usalama kwa ajili ya wana wa Israeli, kwa ajili ya mgeni na kwa ajili ya aishiye nao kama mgeni; ili kila amwuaye mtu, bila kukusudia kuua, apate mahali pa kukimbilia.


Kuhusu kuua na kulipiza kisasi cha damu

16 Lakini kama alimpiga kwa chombo cha chuma, akafa, ni mwuaji huyo; mwuaji hakika yake atauawa.

17 Na kama alimpiga kwa jiwe lililokuwa mkononi mwake, ambalo kwa hilo humkini mtu kufa, naye akafa, yeye ni mwuaji; huyo mwuaji lazima atauawa.

18 Au kama alimpiga kwa chombo cha mti kilichokuwa mkononi mwake ambacho kwa hicho humkini mtu kufa, naye akafa, ni mwuaji huyo, mwuaji lazima atauawa.

19 Mwenye kutwaa kisasi cha damu ndiye atakayemwua mwuaji; hapo atakapokutana naye, atamwua.

20 Tena kama alimsukuma kwa kumchukia au kama alimtupia kitu kwa kumvizia, hadi akafa;

21 au akampiga kwa mkono wake kwa kuwa ni adui, naye akafa; yeye aliyempiga lazima atauawa; yeye ni mwuaji; mwenye kutwaa kisasi cha damu atamwua mwuaji, hapo atakapokutana naye.

22 Lakini ikiwa alimsukuma ghafla pasipo kumchukia; au akamtupia kitu chochote pasipo kumvizia,

23 au kwa jiwe liwalo lote, ambalo kwa kupigwa kwalo humkini mtu kufa, bila kumwona akamtupia hata akafa, naye hakuwa adui yake, wala hakumtakia madhara;

24 ndipo mkutano utaamua kati ya huyo aliyempiga mtu na huyo atakayelipiza kisasi cha damu, kama hukumu hizi zilivyo;

25 nao mkutano utamwokoa yule aliyemwua mtu na mkono wa mwenye kulipiza kisasi cha damu; tena mkutano utamrejesha katika mji wake wa makimbilio, aliokuwa anaukimbilia; naye atakaa humo hata kifo chake kuhani mkuu, aliyepakwa mafuta matakatifu.

26 Lakini kama mwenye kumwua mtu akienda wakati wowote kupita mpaka wa huo mji wa makimbilio, alioukimbilia;

27 na mwenye kutwaa kisasi cha damu akamwona, naye yuko nje ya mpaka wa mji wake wa makimbilio, na mwenye kutwaa kisasi cha damu akamwua huyo mwuaji, hatakuwa na hatia ya damu;

28 kwa sababu ilimpasa kukaa ndani ya mji wake wa makimbilio hadi kifo chake kuhani mkuu lakini kuhani mkuu atakapokwisha kufa huyo mwuaji atarudi aende nchi ya urithi wake.

29 Mambo haya yatakuwa ni amri ya hukumu kwenu, katika vizazi vyenu vyote, katika makazi yenu yote.

30 Mtu yeyote atakayemwua mtu, huyo mwuaji atauawa kwa vinywa vya mashahidi; lakini shahidi mmoja hatashuhudia juu ya mtu akauliwa.

31 Tena, msipokee fidia kwa ajili ya uhai wa mwuaji, ambaye amekuwa na hatia ya mauti; Lakini lazima atauawa.

32 Tena hamtapokea fidia kwa ajili ya huyo aliyeukimbilia mji wake wa makimbilio, apate kwenda tena kukaa katika nchi, hata kifo cha kuhani mkuu.

33 Hivi hamtaitia unajisi nchi ambayo mwakaa; kwa kuwa damu huitia nchi unajisi; wala hapana sadaka itoshayo kwa ajili ya nchi, kwa ajili ya damu iliyomwagwa ndani yake, isipokuwa ni damu ya huyo aliyeimwaga.

34 Kwa hiyo msiitie unajisi nchi mwishiyo ambayo nami nakaa kati yake; kwa kuwa mimi BWANA nakaa kati ya wana wa Israeli.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.

Bible Society of Kenya
Tufuate:



Matangazo