Biblia Todo Logo
Biblia ya mtandaoni
- Matangazo -

1 Wathesalonike 1 - Swahili Revised Union Version - SRUVDC


Salamu

1 Paulo, Silwano na Timotheo, kwa kanisa la Wathesalonike, lililo katika Mungu Baba, na katika Bwana Yesu Kristo. Neema na iwe kwenu na amani.


Imani na kielelezo cha Wathesalonike

2 Twamshukuru Mungu siku zote kwa ajili yenu nyote, tukiwataja katika maombi yetu.

3 Wala hatuachi kuikumbuka kazi yenu ya imani, na taabu yenu ya upendo, na subira yenu ya tumaini lililo katika Bwana wetu Yesu Kristo, mbele za Mungu Baba yetu.

4 Kwa maana, ndugu mnaopendwa na Mungu, tunajua uteule wenu;

5 ya kwamba Injili yetu haikuwafikia katika maneno tu, bali na katika nguvu, na katika Roho Mtakatifu, na uthibitifu mwingi; kama vile mnavyojua jinsi zilivyokuwa tabia zetu kwenu, kwa ajili yenu.

6 Nanyi mkawa wafuasi wetu na wa Bwana, mkiisha kulipokea neno katika dhiki nyingi, pamoja na furaha ya Roho Mtakatifu.

7 Hata mkawa kielelezo kwa watu wote waaminio katika Makedonia, na katika Akaya.

8 Maana kutoka kwenu neno la Mungu limevuma, si katika Makedonia na Akaya tu, ila na kila mahali imani yenu mliyo nayo kwa Mungu imeenea; hata hatuna haja sisi kunena lolote.

9 Kwa kuwa wao wenyewe wanatangaza habari zetu, jinsi kulivyokuwa kuingia kwetu kwenu; na jinsi mlivyomgeukia Mungu mkaziacha sanamu, ili kumtumikia Mungu aliye hai, wa kweli;

10 na kumngojea Mwanawe kutoka mbinguni, ambaye alimfufua katika wafu, naye ni Yesu, mwenye kutuokoa kutoka kwa ghadhabu itakayokuja.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.

Bible Society of Kenya
Tufuate:



Matangazo