1 Mambo ya Nyakati 14 - Swahili Revised Union Version - SRUVDCDaudi ajiimarisha katika Yerusalemu 1 Naye Hiramu, mfalme wa Tiro, akatuma wajumbe kwa Daudi, akampelekea na mierezi, na waashi, na maseremala, ili wamjengee nyumba. 2 Daudi akajua ya kwamba BWANA amemweka imara ili atawale Israeli, na kwamba milki yake imetukuka zaidi kwa ajili ya watu wake Israeli. 3 Tena Daudi akazidi kuoa wake huko Yerusalemu; akazidi kuzaa wana na binti. 4 Na haya ndiyo majina ya watoto aliozaliwa huko Yerusalemu; Shamua, na Shobabu, na Nathani, na Sulemani; 5 na Ibhari, na Elishua, na Elpeleti; 6 na Noga, na Nefegi, na Yafia; 7 na Elishama, na Eliada, na Elifeleti. Kushindwa kwa Wafilisti 8 Wafilisti waliposikia ya kwamba Daudi ametiwa mafuta ili awe mfalme wa Israeli wote, Wafilisti wote wakapanda kumtafuta Daudi; naye Daudi akasikia, akatoka nje kupigana nao. 9 Basi hao Wafilisti walikuwa wamekuja na kujitawanya katika bonde la Warefai. 10 Daudi akamwuliza Mungu, akisema, Je! Nipande juu ya Wafilisti! Utawatia mikononi mwangu? Naye BWANA akamwambia, Panda; kwa kuwa nitawatia mikononi mwako. 11 Basi wakapanda mpaka Baal-perasimu, Daudi naye akawapiga huko; Daudi akasema, BWANA amewafurikia adui zangu kwa mkono wangu, kama mafuriko ya maji. Basi wakapaita mahali pale jina lake Baal-perasimu. 12 Nao wakaiacha miungu yao huko; naye Daudi akaamuru, ikateketezwa kwa moto. 13 Lakini hao Wafilisti wakajitawanya tena mara ya pili bondeni. 14 Na Daudi akamwuliza Mungu tena; naye Mungu akamwambia, Hutapanda kuwafuata; zunguka mbali nao, na kuwajia ukielekea miforsadi. 15 Kisha itakuwa utakapoisikia sauti ya kwenda katika vilele vya miforsadi, ndipo utakapokwenda nje vitani; kwa maana ndipo Mungu ametoka mbele yako, awapige jeshi la Wafilisti. 16 Daudi akafanya kama vile Mungu alivyomwamuru; wakawapiga jeshi la Wafilisti toka Geba mpaka Gezeri. 17 Sifa za Daudi zikafika nchi zote; naye BWANA akawaletea mataifa yote hofu yake. |
Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Bible Society of Kenya