Zefania 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mwito wa kumurudilia Yawe 1 Mukusanyike, mukusanyike, enyi taifa la watu wasiokuwa na haya, 2 mbele hamujapeperushwa mbali kama maganda, mbele haijawafikia siku ya hasira kali ya Yawe, mbele haijawafikia siku ya kasirani ya Yawe. 3 Mutafute Yawe, enyi wanyenyekevu wote katika inchi, enyi munaozitii amri zake. Mutafute haki, mutafute unyenyekevu; labda mutaiponyoka siku ya kasirani ya Yawe. Maangamizi kwa mataifa jirani 4 Muji wa Gaza utahamwa, muji wa Askeloni utakuwa tupu. Wakaaji wa Asidodi watafukuzwa muchana, na wale wa Ekroni wataongolewa. 5 Ole wenu wakaaji wa inchi za pembeni ya bahari, watu wanaoishi kule Krete! Yawe amesema juu yenu, enyi wakaaji wa Kanana, inchi ya Wafilistini: Mimi nitawaangamiza wala hakutabaki hata mukaaji mumoja! 6 Nanyi inchi ya pembeni ya bahari mutafanywa kuwa shamba la malisho; mutakuwa vibanda vya wachungaji na mazizi ya kondoo. 7 Inchi ya pembeni ya bahari itakuwa makao ya mabaki ya ukoo wa Yuda. Watachunga nyama wao kule. Nyumba za muji wa Askeloni zitakuwa pahali pao pa kulala. Maana mimi Yawe, Mungu wao nitawakumbuka na kuwarudishia hali yao njema. 8 Nimeyasikia matusi ya Wamoabu na mazarau ya Waamoni, jinsi walivyowatusi watu wangu na kujivuna kwamba wamenyanganya inchi yao. 9 Kwa hiyo, kama vile ninavyoishi, –ni ujumbe wa Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli– inchi ya Moabu itakuwa kama Sodoma na ya Amoni itakuwa kama Gomora. Inchi zake zitakuwa shamba la miiba na mashimo ya chumvi, zitakuwa ukiwa milele. Watu wangu watakaobaki wataziteka, watu wa taifa langu waliobaki watazirizi. 10 Hayo yatakuwa malipo ya kiburi chao, kwa sababu waliwachekelea na kujivuna mbele ya watu wa Yawe wa majeshi. 11 Wao watamwogopa sana Yawe; ataiangamiza miungu yote ya dunia. Mataifa yote katika dunia yatamwabudu; kila taifa katika pahali pake. 12 Nanyi watu wa Kushi vilevile mutauawa kwa upanga. 13 Yawe atanyoosha mukono wake kwa kuazibu inchi ya upande wa kaskazini, na kuiangamiza inchi ya Asuria. Ataufanya muji wa Ninawe kuwa ukiwa, kuwa pahali penye kukauka kama jangwa. 14 Makundi ya nyama wa kufugwa watalala ndani yake, vilevile kila nyama wa pori. Tai, nyangenyange na korongo wataishi juu ya nguzo zake, bundi watalia kwenye madirisha yake, vibombobombo watalia kwenye vizingiti, maana nyumba zake za mierezi zitakuwa tupu. 15 Basi huu ndio muji uliojivuna na kuishi kwa usalama, muji uliojisemesha: Ni mimi tu, hakuna mwingine! Jinsi gani umekuwa mutupu na makao ya nyama wa pori! Kila mutu anayepita karibu atauzomea na kuuzarau. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo