Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Yoshua 6 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Waisraeli wanauteka muji wa Yeriko

1 Milango ya kuingilia katika muji wa Yeriko ilikuwa imefungwa imara kwa ndani kwa kuwazuia Waisraeli wasiingie. Hakuna mutu aliyeweza kuingia wala kutoka katika muji huo.

2 Yawe akamwambia Yoshua: “Mimi nitautia katika mikono yako muji wa Yeriko pamoja na mufalme wake na waaskari wake shujaa.

3 Wewe na wale watu wenye silaha wote mutauzunguka ule muji mara moja kila siku kwa muda wa siku sita.

4 Makuhani saba, kila mumoja akiwa anabeba baragumu yake ya pembe ya kondoo dume, watatangulia mbele ya Sanduku la Agano. Katika siku ya saba mutauzunguka muji ule mara saba, nao makuhani wakipiga mabaragumu.

5 Watakapopiga hayo mabaragumu kwa mulio mukubwa na mara tu mutakaposikia huo mulio, watu wote watapiga kelele kubwa, nazo kuta za muji zitaanguka chini. Halafu watu wataushambulia muji kila mumoja kutoka pahali aliposimama.”

6 Basi, Yoshua mwana wa Nuni, akawaita makuhani, akawaambia: “Mulibebe Sanduku la Agano na makuhani saba watwae mabaragumu saba ya kondoo dume, watangulie mbele ya Sanduku la Yawe.”

7 Yoshua akawaambia watu: “Mupite mbele, muzunguke muji, nao watu wenye silaha waende mbele ya Sanduku la Agano la Yawe.”

8 Kulingana na amri ya Yoshua, wale makuhani saba waliokuwa na mabaragumu saba ya kondoo dume wakaenda mbele ya Yawe, wakiwa wanapiga mabaragumu, nyuma yao wakifuatwa na lile Sanduku la Agano.

9 Wale watu wenye silaha wakawatangulia wale makuhani ambao walikuwa wanapiga mabaragumu, na walinzi wengine wakifuata nyuma ya Sanduku hilo, nayo mabaragumu yakilia kwa mufululizo.

10 Lakini Yoshua akawaamuru watu: “Musipige kelele au kutoa sauti, wala neno lolote lisitoke katika vinywa vyenu, mpaka siku ile ambapo nitawaambia mupige kelele; wakati ule ndipo mutakapopiga kelele.”

11 Basi, Yoshua akawaamuru wale watu wauzunguke muji mara moja kila siku wakiwa wanabeba Sanduku la Agano la Yawe na kurudi katika kambi kulala usiku.

12 Asubui yake Yoshua akaamuka mapema sana, na makuhani wakalibeba lile Sanduku la Agano la Yawe.

13 Wale makuhani saba wenye mabaragumu saba ya kondoo dume walitembea mbele ya Sanduku la Yawe wakipiga mabaragumu kwa mufululizo. Watu wenye silaha walilitangulia Sanduku la Yawe na walinzi wengine nyuma yake. Mabaragumu yakaendelea kupigwa.

14 Kwa siku ya pili, waliuzunguka ule muji mara moja; na kurudi tena katika kambi kwao. Wakafanya hivyo kwa muda wa siku sita.

15 Siku ya saba, waliamuka asubui mapema, wakauzunguka muji ule mara saba. Ilikuwa ni siku hiyo tu ambayo waliuzunguka muji ule mara saba.

16 Ilipofika mara ya saba, wakati makuhani walipokwisha kupiga mabaragumu, Yoshua akawaambia watu: “Mupige kelele, kwa kuwa Yawe amekwisha kuwapa huu muji!

17 Muji ule utaangamizwa na kila kitu kinachokuwa mule maana umetolewa kwa Yawe. Rahabu, yule kahaba, ndiye atakayeachwa pamoja na wale ambao wako ndani ya nyumba yake kwa sababu aliwaficha wapelelezi wetu.

18 Lakini musitwae kitu chochote ambacho kimetolewa kusudi kiangamizwe. Mukitwaa kitu chochote ambacho kimetolewa kusudi kiangamizwe, mutaifanya kambi ya Israeli kuwa kitu cha kuangamizwa, na hivyo kuiletea hasara.

19 Lakini feza yote, zahabu, vyombo vya shaba na chuma ni vitakatifu kwa Yawe; hivyo vitawekwa katika hazina ya Yawe.”

20 Basi, watu wakapiga kelele nayo mabaragumu yakiwa yanapigwa. Watu waliposikia sauti ya mabaragumu walipiga kelele kubwa, na kuta za muji zikaanguka chini kabisa. Mara tu watu wakaushambulia muji, kila mumoja kutoka pahali aliposimama, wakauteka.

21 Kisha wakaangamiza kila kitu katika muji ule na kuwaua kwa upanga: wanaume na wanawake, vijana na wazee, ngombe, kondoo na punda.

22 Yoshua akawaambia wale wapelelezi wawili walioipeleleza inchi hiyo: “Muende katika nyumba ya yule kahaba; mumulete yule mwanamuke na wale wote ambao ni wandugu zake kama mulivyomwapia.”

23 Basi, wale vijana wapelelezi wakaenda; wakamuleta Rahabu, baba yake na mama yake, wandugu zake na watu wote wa jamaa yake, wakawaweka inje ya kambi ya Israeli.

24 Kisha, wakauchoma kwa moto muji wa Yeriko na kila kitu kilichokuwa mule isipokuwa feza, zahabu, vyombo vya shaba na vya chuma; hivyo viliwekwa katika hazina ya nyumba ya Yawe.

25 Lakini yule kahaba Rahabu pamoja na watu wote wa nyumba ya baba yake, Yoshua akayaokoa maisha yao. Rahabu akaishi kati ya Waisraeli mpaka leo, kwa sababu aliwaficha wajumbe ambao Yoshua aliwatuma kwenda kuupeleleza muji wa Yeriko.

26 Wakati ule Yoshua akaapa mbele ya watu akisema: “Atakayeujenga tena muji wa Yeriko, alaaniwe na Mungu. Yeyote atakayeweka musingi wa muji huo, muzaliwa wake wa kwanza akufe. Yeyote atakayejenga mulango wa muji huo, mwana wake kitenda mimba akufe.”

27 Basi, Yawe alikuwa pamoja na Yoshua na sifa zake zikaenea katika inchi yote.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ