Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Yoshua 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Mawe ya ukumbusho kumi na mawili

1 Taifa zima lilipokwisha kuvuka muto Yordani, Yawe akamwambia Yoshua:

2 “Chagua watu kumi na wawili kati ya hao Waisraeli, ni kusema mutu mumoja kutoka kila kabila,

3 uwaagize hivi: ‘Mutwae mawe kumi na mawili kutoka hapa katikati ya muto Yordani, kutoka hapa miguu ya makuhani ilipokuwa, mutwae mawe hayo, muyaweke pahali pale ambapo mutalala leo hii.’ ”

4 Yoshua akawaita hao watu kumi na wawili ambao alikuwa amewachagua kati ya Waisraeli, kila kabila mutu mumoja,

5 akawaambia: “Mulitangulie Sanduku la Agano la Yawe, Mungu wenu, mpaka katikati ya muto Yordani. Kila mumoja wenu abebe jiwe kwenye bega lake, jiwe moja kwa ajili ya kila kabila la Israeli.

6 Jambo hilo litakuwa kitambulisho kati yenu; na watoto wenu watakapowauliza kwa siku zinazokuja: ‘Mawe haya yana maana gani kwenu?’

7 Ninyi mutawaambia: ‘Sanduku la Agano la Yawe lilipopitishwa katika muto Yordani, maji ya muto huo yalizuiliwa yasitiririke!’ Kwa hiyo mawe haya yatakuwa ukumbusho kwa Waisraeli milele.”

8 Wale wanaume wakafanya kama vile walivyoamriwa na Yoshua, wakatwaa mawe kumi na mawili kutoka katikati ya muto Yordani, jiwe moja kwa ajili ya kila kabila la Israeli, kama Yawe alivyomwambia Yoshua, wakaenda nayo mpaka pahali pale walipolala, wakayaweka kule.

9 Yoshua akasimika vilevile mawe kumi na mawili katikati ya muto Yordani, pahali pale miguu ya makuhani waliobeba lile Sanduku la Agano iliposimama. Mawe hayo yako kule mpaka hivi leo.

10 Wale makuhani waliobeba Sanduku la Agano, walisimama katikati ya muto Yordani mpaka watu walipomaliza kutimiza kila kitu ambacho Yawe alimwamuru Yoshua awaambie watu; Yoshua alifanya yote ambayo Musa alikuwa amemwamuru. Watu wakaharakisha kuvuka muto,

11 na watu wote walipokwisha kuvuka, wale makuhani wakawatangulia na lile Sanduku la Agano la Yawe.

12 Wanaume wa kabila la Rubeni na la Gadi na nusu ya kabila la Manase waliwatangulia Waisraeli wakiwa na silaha zao, kama vile walivyoagizwa na Musa.

13 Watu yapata elfu makumi ine wakiwa na silaha tayari kwa vita walipita mbele ya Yawe wakielekea bonde la muji wa Yeriko.

14 Katika siku hiyo Yawe akamutukuza Yoshua mbele ya Waisraeli wote, nao wakamuheshimu Yoshua maisha yake yote kama walivyomuheshimu Musa katika maisha yake.

15 Kisha Yawe akamwambia Yoshua:

16 “Uamuru makuhani wanaobeba sanduku la agano, watoke katika muto Yordani.”

17 Basi, Yoshua akawaamuru wale makuhani: “Mutoke katika muto Yordani.”

18 Hao makuhani waliokuwa wanabeba lile Sanduku la Agano la Yawe walipotoka katikati ya muto Yordani, na kukanyaga ukingo wa muto, maji ya muto Yordani yakaanza kutiririka tena, na kufurika kama mbele.

19 Waisraeli walivuka muto Yordani katika siku ya kumi ya mwezi wa kwanza, wakapiga kambi kule katika muji wa Gilgali, upande wa mashariki wa Yeriko.

20 Yoshua akayasimika yale mawe kumi na mawili ambayo waliyatwaa kutoka muto Yordani, kule Gilgali.

21 Kisha Yoshua akawaambia Waisraeli: “Watoto wenu watakapowauliza kwa siku zinazokuja: ‘Mawe haya yana maana gani?’

22 Mutawaambia hivi: ‘Taifa la Israeli lilivuka muto huu wa Yordani pahali pakavu.’

23 Mutawaambia kwamba Yawe, Mungu wenu, aliyakausha maji ya muto Yordani kwa ajili yenu mpaka mukavuka, kama vile alivyofanya kwa bahari Nyekundu. Akaikausha mbele yetu mpaka tulipovuka

24 kusudi watu wote wa dunia wajue kwamba mukono wa Yawe una nguvu; nanyi mupate kumwogopa Yawe, Mungu wenu, milele.”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ