Yoshua 23 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Hotuba ya mwisho ya Yoshua 1 Nyuma ya muda murefu, Yawe aliwajalia Waisraeli amani kwa kuwaokoa na waadui zao pande zote. Wakati ule Yoshua alikuwa muzee wa miaka mingi. 2 Yoshua aliwaita Waisraeli wote pamoja na viongozi na wazee wao, waamuzi na wakubwa, akawaambia: “Sasa mimi nimekuwa muzee wa miaka mingi. 3 Ninyi mumeona mambo yote Yawe, Mungu wenu, aliyoyatendea mataifa haya yote kwa ajili yenu. Yawe, Mungu wenu, ndiye aliyewapigania. 4 Inchi za mataifa yaliyobaki na yale niliyoyaangamiza nimewagawanyia zikuwe mali ya makabila yenu, kutoka Yordani mpaka bahari ya Mediteranea, upande wa magaribi. 5 Yawe, Mungu wenu, atayaondoa mbele yenu na kuyafukuza kabisa, nanyi mutarizi inchi yao kama vile Yawe, Mungu wenu, alivyowaahidi. 6 Kwa hiyo, mukuwe imara katika kushika yote yaliyoandikwa katika kitabu cha Sheria ya Musa, musiyaache hata kidogo. 7 Musishirikiane na mataifa haya yaliyobaki kati yenu. Musiitaje miungu yao wala musiape kwa majina ya miungu yao; musiitumikie wala kuinama mbele yao. 8 Lakini muambatane na Yawe, Mungu wenu, kama mulivyofanya mpaka leo. 9 Maana Yawe ameyafukuza mbele yenu mataifa makubwa na yenye nguvu na hakuna mutu ambaye ameweza kuwapinga ninyi mpaka leo. 10 Mutu wenu mumoja tu anaweza kuwakimbiza waadui elfu moja, maana Yawe Mungu wenu ndiye anayewapigania kama alivyowaahidi. 11 Basi, mukuwe waangalifu sana kumupenda Yawe, Mungu wenu. 12 Maana, kama mukimwasi Yawe na kujiunga na mataifa haya yaliyobaki kati yenu, mukioa kwao nao wakioa kwenu, 13 mujue kwa hakika kwamba Yawe, Mungu wenu, hataendelea kuyafukuza mataifa haya mbele yenu, lakini yatakuwa kwenu kikwazo na mutego. Yatakuwa kwenu mujeledi wa kuwapiga na miiba ya kuwachoma kwa macho mpaka pale mutakapoangamia na kutoka katika inchi hii nzuri ambayo Yawe, Mungu wenu, amewapa. 14 “Sasa, wakati wangu wa kufa kama inavyokuwa kawaida ya wanadamu wote umekaribia. Lakini ninyi wote munajua wazi ndani ya mioyo na roho zenu kwamba katika mambo yote mema ambayo Yawe, Mungu wenu aliwaahidi, hakuna hata moja ambalo halikutimia. Yote yametimia kama vile alivyoahidi. 15 Lakini kama vile Yawe, Mungu wenu, alivyotimiza mambo yote mema aliyowaahidi, ni vile vile anavyoweza kuwaletea maovu yote mpaka awaangamize wote kutoka inchi hii nzuri ambayo amewapa. 16 Kama mukivunja agano la Yawe, Mungu wenu, ambalo aliwaamuru mulishike, mukienda kuitumikia miungu mingine na kuinama mbele yao; basi, hasira ya Yawe itawaka juu yenu, nanyi mutaangamia mara moja kutoka inchi hii nzuri ambayo amewapa.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo