Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Yoshua 18 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Makabila mengine yanagawanyiwa inchi

1 Nyuma ya kuishinda ile inchi, Waisraeli wote pamoja wakakusanyika kule Shilo na kulisimika hema la kusanyiko.

2 Kulikuwa kunabaki kati yao makabila saba ambayo hayakuwa yamegawanyiwa sehemu yao ya inchi.

3 Kwa hiyo, Yoshua akawaambia Waisraeli: “Mutangojea mpaka wakati gani kwenda kuikamata inchi ile ambayo Yawe, Mungu wa babu zenu, amewapatia?

4 Muchague watu watatu kutoka kila kabila niwatume katika inchi yote wachunguze na kuchapa taswira kulingana na makabila yao, kisha waniletee habari.

5 Nao wataigawanya inchi hiyo kwa sehemu saba. Kabila la Yuda litabaki na sehemu yake ya kusini na kabila la Yosefu kaskazini.

6 Mutayarishe maelezo kamili juu ya sehemu zote saba na kuniletea. Hapo, nitapiga kura mbele ya Yawe, Mungu wetu, juu ya sehemu ya kila kabila lenu.

7 Lakini Walawi hawatapata sehemu yoyote kati yenu, maana sehemu yao ni kuwa makuhani wa kumutumikia Yawe. Gadi, Rubeni na nusu ya kabila la Manase walikwisha kupata sehemu yao upande wa mashariki wa muto Yordani. Walipewa sehemu hii na Musa, mutumishi wa Yawe.”

8 Basi, watu hao wakaanza safari ya kwenda kuichunguza inchi. Mbele hawajakwenda, Yoshua akawapa maagizo: “Muende katika inchi yote muandike maelezo kamili juu ya hiyo inchi, kisha murudie kunielezea, nami nitapiga kura mbele ya Yawe hapahapa Shilo juu ya sehemu mutakayopewa.”

9 Wanaume hao wakazunguka katika inchi yote, wakachapa taswira kamili juu ya sehemu zake saba pamoja na miji yake, kisha wakarudi kwa Yoshua kule katika kambi Shilo.

10 Kule Shilo, Yoshua akazipigia kura sehemu hizo mbele ya Yawe, akawagawanyia Waisraeli; kila kabila na sehemu yake.


Inchi ya kabila la Benjamina

11 Kura ya kwanza ililipata kabila la Benjamina kulingana na ukoo zake. Eneo walilopewa watu hao lilikuwa katikati ya lile la kabila la Yuda na lile la kabila la Yosefu.

12 Mupaka wake wa kaskazini ulianzia kwenye muto Yordani na kupitia upande wa kaskazini wa Yeriko na inchi ya milima ukaelekea upande wa magaribi mpaka kwenye jangwa la Beti-Aweni.

13 Kutoka kule, mupaka wake ulikwenda kusini kuelekea Luzi kupitia upande wa kusini wa Luzi, ni kusema Beteli, hata Ataroti-Adari, kwenye mulima unaokuwa upande wa kusini wa Beti-Horoni ya Chini.

14 Upande wa magaribi wa mulima huo unaokuwa upande wa kusini wa Beti-Horoni, mupaka uligeuka ukaelekea kusini hata Kiriati-Bali, muji unaoitwa vilevile Kiriati-Yearimu, muji ambao ni mali ya kabila la Yuda. Huu ndio uliokuwa mupaka wake upande wa magaribi.

15 Upande wa kusini mupaka wake ulianzia Kiriati-Yearimu, ukafika Efuroni na kwenda mpaka kwenye chemichemi ya maji ya Nefutoa.

16 Kisha ulielekea chini kupitia pembeni ya mulima unaokuwa karibu na bonde la mwana wa Hinomu, ambalo lilikuwa katika sehemu ya kaskazini zaidi ya bonde la Warefaimu. Halafu mupaka uliteremuka kuelekea bonde la Hinomu, upande wa kusini wa kilima cha Wayebusi, ukaendelea kuteremuka mpaka Eni-Rogeli.

17 Kule, mupaka uligeuka kwenda kaskazini kuelekea Eni-Semesi, ukapitia Geliloti karibu na mwinuko wa Adumimu na kuteremuka mpaka kwenye jiwe la Bohani mwana wa Rubeni.

18 Kutoka pale, mupaka ulizunguka upande wa kaskazini kwenye ukingo wa juu wa Araba na kuishia kule Araba.

19 Tena, ukaendelea kwa upande wa kaskazini wa kilima cha Beti-Hogla na kuishia kaskazini kabisa ya guba ya bahari ya Chumvi, pahali muto Yordani unapoingilia. Huu ni mupaka wake kwa upande wa kusini.

20 Muto Yordani ndio uliokuwa mupaka wake upande wa mashariki. Ndivyo zilivyowekewa mipaka inchi zilizopewa ukoo za kabila la Benjamina.

21-28 Miji ya ukoo za kabila la Benjamina ni: Yeriko, Beti-Hogla, Emeki-Kesisi, Beti-Araba, Zemaraimu, Beteli, Awimu, Para, Ofura, Kefari-Amoni, Ofuni na Geba. Jumla ya miji kumi na miwili pamoja na vijiji vyake. Gibeoni, Rama, Beroti, Misipa, Kefira, Moza, Rekemu, Iripeli, Tarala, Zela, Ha-Elefu, Yebusi, ni kusema Yerusalema, Gibea na Kiriati-Yearimu. Jumla ya miji kumi na mine pamoja na vijiji vyake. Hiyo yote ni sehemu watu wa kabila la Benjamina na ukoo zao waliyopewa.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ