Yoshua 14 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kugawanywa kwa inchi ya Kanana 1 Haya ndiyo maeneo ya inchi ambayo Waisraeli walipewa katika inchi ya Kanana. Kuhani Eleazari na Yoshua mwana wa Nuni, pamoja na wakubwa wa ukoo za makabila ya Waisraeli waliyowagawanyia Waisraeli. 2 Sehemu hiyo yao waligawanyiwa kwa kura kama vile Yawe alivyomwamuru Musa awape yale makabila tisa na nusu. 3 Musa alikuwa ameyapa yale makabila mawili na nusu sehemu yao upande wa mashariki wa Yordani, lakini Walawi hawakukuwa wamepewa sehemu yao pamoja nao. 4 Wazao wa Yosefu walikuwa makabila mawili: Manase na Efuraimu. Kabila la Lawi halikupewa sehemu yoyote ya inchi, lakini miji tu ya kuishi na mashamba ya malisho kwa ajili ya nyama wao na riziki zao. 5 Basi, Waisraeli wakaigawanya inchi kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Kalebu anapewa muji wa Hebroni 6 Siku moja watu wa kabila la Yuda wakamwendea Yoshua kule Gilgali. Kalebu mwana wa Yefune, ambaye alikuwa Mukenizi, akamwambia Yoshua: “Bila shaka unakumbuka jinsi Yawe alivyomwambia Musa, mutu wa Mungu, juu yangu na wewe tulipokuwa Kadesi-Barnea. 7 Nilipokuwa na umri wa miaka makumi ine, Musa mutumishi wa Mungu, akanituma kutoka Kadesi-Barnea, kwenda kuipeleleza inchi. Niliporudi nikamuletea habari za mambo ya kule kadiri nilivyoamini katika moyo wangu. 8 Wakati wale wenzangu waliokwenda pamoja nami waliwavunja watu moyo, lakini mimi nilimufuata Yawe, Mungu wangu, kwa uaminifu. 9 Siku hiyo Musa akaniapia: ‘Hakika sehemu ya inchi ile ambayo ulipita ndani yake itakuwa yako wewe na wazao wako milele. Kwa sababu ya uaminifu wako kwa Yawe, Mungu wako’. 10 Lakini sasa ni muda wa miaka makumi ine na mitano tangu Yawe aliposema na Musa, wakati Waisraeli walipokuwa wanapita katika jangwa. Tangu wakati ule Yawe, kama vile alivyoahidi, amenilinda muzima mpaka leo, na sasa mimi nina umri wa miaka makumi nane na mitano. 11 Lakini bado nina nguvu kama nilivyokuwa wakati ule Musa aliponituma. Hata sasa nina nguvu za kuweza kupigana vita au kufanya kazi nyingine yoyote. 12 Sasa ninaomba unipe inchi hii ya milima ambayo Yawe aliniahidi siku ile. Wewe ulisikia siku ile kwamba Waanaki waliishi humo katika miji yenye kuta; labda Yawe atakuwa pamoja nami, nami nitawafukuza kama vile Yawe alivyosema.” 13 Halafu Yoshua akamubariki Kalebu mwana wa Yefune na kumupa muji wa Hebroni kuwa sehemu yake. 14 Kwa hiyo, muji wa Hebroni ni sehemu yao wazao wa Kalebu mwana wa Yefune Mukenizi mpaka hivi leo, kwa sababu Kalebu alikuwa mwaminifu kwa Yawe, Mungu wa Israeli. 15 Muji wa Hebroni zamani uliitwa Kiriati-Arba. Arba alikuwa mutu mukubwa kuliko wote kati ya Waanaki. Inchi nzima ikakuwa tulivu bila vita. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo