Yoshua 13 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Eneo lililokuwa bado kutwaliwa 1 Wakati huu, Yoshua alikuwa muzee wa miaka mingi. Basi, Yawe akamwambia: “Wewe sasa umekuwa muzee wa miaka mingi, na kumebaki bado sehemu kubwa za inchi ambazo hazijatwaliwa. 2 Sehemu hizo ni: inchi yote ya Wafilistini na inchi yote ya Wagesuri, 3 ni kusema eneo linalojulikana kama la Wakanana, kuanzia kwenye kijito cha Sihori kwa mupaka wa Misri mpaka kwenye eneo la Ekuroni kule kaskazini. Maeneo yote ya watawala watano wa Wafilistini: Gaza, Asidodi, Asikeloni, Gati na Ekuroni pamoja na eneo la Awini, 4 upande wa kusini. Vilevile inchi za Wakanana kuanzia Ara ya Wasidoni mpaka Afeki kwa mupaka wa Waamori; 5 vilevile eneo la Gebali na Lebanoni upande wa mashariki ya Bali-Gadi chini ya mulima Hermoni mpaka Lebo-Hamati; 6 vilevile eneo la milima inayokuwa kati ya Lebanoni na Misirepoti-Maimu ambayo wakaaji wake ni Wasidoni. Kadiri na jinsi Waisraeli watakavyoendelea mbele, mimi mwenyewe nitayafukuza mataifa hayo katika inchi hizo mbele yao. Nawe utawagawanyia Waisraeli sehemu mbalimbali za inchi hizo kwa kura kama nilivyokuamuru. 7 Utayagawanyia inchi hizo makabila kenda na nusu ya kabila la Manase ambao bado hawajapata kitu.” Mugawanyo wa upande wa mashariki wa Yordani 8 Makabila ya Rubeni, Gadi na nusu nyingine ya kabila la Manase yalikuwa yamepewa inchi inayokuwa upande wa mashariki wa muto Yordani, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa, mutumishi wake. 9 Eneo lao lilikuwa kuanzia Aroeri kandokando ya bonde la Arnoni na muji ule unaokuwa katikati ya bonde, na inchi ile yote ya bonde tangu Medeba mpaka Diboni, 10 pamoja na miji ya mufalme Sihoni wa Waamori, aliyetawala kule Hesiboni hata kwa mupaka wa Waamoni, 11 pamoja na inchi za Gileadi, eneo la Wagesuri na Wamakati mulima wa Hermoni na inchi yote ya Basani mpaka Saleka; 12 na ufalme wote wa Ogi mumoja wa Warefaimu waliobaki, ambaye alitawala kule Asitaroti na Edirei katika Basani. Musa alikuwa amewashinda hao wote na kuwafukuzia mbali. 13 Hata hivyo, Wagesuri na Wamakati hawakufukuzwa lakini wanaishi kati ya Waisraeli mpaka leo. 14 Musa hakuwapa watu wa kabila la Lawi inchi yoyote. Lakini sadaka za kuteketezwa kwa moto walizomutolea Yawe, Mungu wa Israeli, hizo ndizo zilizokuwa fungu lao, kama vile Yawe alivyomwambia Musa. 15 Sehemu ya inchi ambayo Musa aliwapa watu wa kabila la Rubeni kulingana na jamaa zao, 16 ilikuwa kuanzia Aroeri pembeni ya bonde la Arnoni na muji uliokuwa katika bonde hilo pamoja na inchi yote ya bonde ya Medeba. 17 Ilikuwa vilevile pamoja na Hesiboni na miji yake yote inayokuwa katika sehemu ya bonde: ni kusema Diboni, Bamoti-Bali, Beti-Bali-Meoni, 18 Yasa, Kedemoti, Mefati, 19 Kiriataimu, Sibuma, Zereti-Sahari, kule kwa kilima katika bonde, 20 Beti-Peori, miteremuko ya mulima Pisiga, Beti-Yesimoti 21 na miji yote ya mabonde, inchi yote ya mufalme Sihoni wa Waamori ambaye alitawala kule Hesiboni; Musa alikuwa amemushinda huyu Sihoni pamoja na viongozi wa Midiani, Evi, Rekemu, Suri, Huri na Reba, ambao walitawala inchi kwa jina la mufalme Sihoni. 22 Balamu mwaguzi mwana wa Beori ambaye Waisraeli walimwua alikuwa mumoja wao. 23 Mupaka wa inchi ya kabila la Rubeni upande wa magaribi ulikuwa muto Yordani. Miji na maeneo yaliyotajwa hapa ndiyo sehemu waliyopewa watu wa ukoo za kabila la Rubeni. 24 Sehemu ya inchi ambayo Musa aliwapa watu wa kabila la Gadi kulingana na ukoo zao 25 ilikuwa Yazeri, miji yote ya Gileadi na nusu ya inchi ya Waamoni mpaka Aroeri kwa upande wa mashariki wa Raba. 26 Vilevile kuanzia Hesiboni mpaka Ramati-Misipe, Betonimu, na kutokea Mahanaimu hata kwa mupaka wa Debiri. 27 Vilevile miji iliyokuwa katika bonde la Beti-Haramu, Beti-Nimura, Sukoti na Zafoni na inchi yote iliyokuwa ya mufalme Sihoni wa Hesiboni; eneo hilo lilikuwa upande wa mashariki wa Yordani na kupakana na upande wa kusini wa bahari ya Kineroti. 28 Miji na vijiji hivi ndivyo watu wa kabila la Gadi walivyopewa kulingana na ukoo zao. 29 Tena, Musa alikuwa ameipatia nusu ya kabila la Manase kulingana na ukoo zake, 30 eneo la inchi kuanzia Mahanaimu mpaka kuingia katika inchi yote iliyokuwa ya mufalme Ogi katika Basani, pamoja na miji makumi sita ya Yairi, 31 nusu ya Gileadi, Astaroti, Edirei, ambayo ilikuwa ya mufalme Ogi wa Basani. Nusu ya wazao wa Makiri mwana wa Manase, eneo hili walipewa kulingana na ukoo zao. 32 Musa alikuwa amewagawanyia sehemu hizo mbalimbali za inchi iliyokuwa upande wa mashariki wa Yeriko na Yordani, wakati alipokuwa kwenye mabonde ya Moabu. 33 Lakini kabila la Lawi, Musa hakulipa sehemu yao ya inchi, maana aliwaambia kwamba sehemu yao itakuwa kumutumikia Yawe, Mungu wa Israeli. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo