Yoeli 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mungu atayahukumu mataifa 1 Kwa wakati ule, na katika siku zile nitakapowarudisha tena watu wa Yuda na Yerusalema katika hali yao ya mbele, 2 nitayakusanya mataifa yote, niyapeleke katika bonde linaloitwa: “Yawe anahukumu”. Huko nitayahukumu mataifa hayo, kwa mambo waliyowatendea watu wangu Waisraeli, hao wanaokuwa mali yangu mimi mwenyewe. Maana waliwatawanya kati ya mataifa, waligawanya inchi yangu 3 na kugawanya watu wangu kwa kupiga kura. Waliuzisha vijana wanaume kwa kuhonga kahaba, na wabinti kwa kupata divai. 4 Munataka nini juu yangu enyi watu wa Tiro na Sidona na maeneo yote ya Filistia? Munataka kunilipiza kisasi? Kama munalipiza kisasi, mimi nitawalipiza mara moja! 5 Mumetwaa feza na zahabu yangu, na kuvibeba vitu vyangu vya bei kali mpaka kwenye mahekalu yenu. 6 Mumewapeleka watu wa Yuda na Yerusalema mbali na inchi yao, mukawauzisha kwa Wagriki. 7 Sasa, nitawarudisha watu wangu kutoka kule mulikowauzisha. Nitawalipiza kisasi kwa yote muliyowatendea. 8 Nitawauzisha watoto wenu wanaume na wanawake kwa watu wa Yuda, nao Wayuda watawauzishia watu wa Seba, watu wa taifa la mbali kabisa. –Ni Yawe anayesema hivyo. 9 Muwatangazie watu wa mataifa jambo hili: Mujitayarishe kwa vita, muwaite mashujaa wenu; waaskari wote wakusanyike, waende mbele. 10 Mufue majembe yenu kuwa mapanga, visu vyenu vikubwa vikuwe mikuki. Hata yule anayekuwa zaifu aseme: “Mimi vilevile ni shujaa”. 11 Mukuje upesi, enyi mataifa yote jirani, mukusanyike kule katika bonde. Ee Yawe! Telemusha waaskari wako kuwashambulia! 12 Mataifa haya yajiweke tayari; yakuje kwenye bonde la Yawe Anahukumu. Kule, mimi Yawe, nitaikaa kwa kuyahukumu mataifa yote jirani. 13 Mutwae kisu cha kuvuna, maana sasa ni wakati wa mavuno. Muingie! Muwapondeponde kama zabibu ambazo zimejaza kikamulio. Uovu wao umepita kipimo kama mitungi inayofurika. 14 Wanafika makundi kwa makundi kwenye bonde la Hukumu, maana siku ya Yawe imekaribia. 15 Jua na mwezi vinatiwa giza, na nyota zimeacha kuangaza. Mungu atawabariki watu wake 16 Yawe ananguruma kule Sayuni; sauti yake inavuma kutoka Yerusalema; mbingu na dunia vinatetemeka. Lakini Yawe ni kimbilio la watu wake, ni kikingio cha usalama kwa Waisraeli. 17 Hapo, enyi Waisraeli, mutajua kwamba mimi ni Yawe, Mungu wenu, ninakaa Sayuni, mulima wangu mutakatifu. Muji Yerusalemu utakuwa muji mutakatifu; na wageni hawatapita tena ndani yake. 18 Wakati ule, divai mupya itatiririka juu ya milima, na maziwa yatatiririka juu ya milima. Vijito vyote vya Yuda vitajaa maji; chemichemi itatokea ndani ya nyumba ya Yawe, na kulinyweshea bonde la Sitimu. 19 Misri itakuwa matongo, Edomu itakuwa jangwa tupu, kwa sababu waliwashambulia watu wa Yuda wakawaua watu wasiokuwa na kosa. 20 Lakini inchi ya Yuda itakaliwa na watu kwa milele, na Yerusalema kwa kizazi hata kizazi. 21 Nitawaazibu waliomwanga damu ya watu wa Yuda wala sitawaachilia wenye makosa. Yawe anakaa Sayuni. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo