Yobu 37 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Kutokana na hayo, moyo wangu unatetemeka, na kuruka kutoka pahali pake. 2 Musikilize ngurumo ya sauti ya Mungu, na muvumo wa sauti kutoka ndani ya kinywa chake. 3 Anafanya uenee chini ya mbingu yote, anaeneza umeme wake katika pembe zote za dunia. 4 Halafu sauti yake inanguruma, sauti ya Mungu inanguruma kwa utukufu; yeye hazuizi umeme wakati inaposikilika. 5 Mungu anapiga radi ya ajabu kwa sauti yake, anafanya mambo makubwa tusiyoweza kuyaelewa. 6 Anaiambia teluji: “Anguka juu ya inchi!” na manyunyu na mvua: “Nyesha kwa nguvu.” 7 Anafunga shuguli za kila mutu kusudi watu wote watambue kazi yake. 8 Nyama wa pori wanarudi katika maficho yao na kubaki katika mapango yao. 9 Zoruba inavuma kutoka chumba chake, na baridi kali kutoka katika gala yake. 10 Kwa pumzi ya Mungu barafu inatokea, uso wa maji unaganda kwa haraka. 11 Mungu analijaza wingu manyunyu mazito; mawingu yanasambaza umeme wake. 12 Kwa amri yake vyote vinazunguka huku na kule, kutimiza kila kitu anachoviamuru, kufanya katika ulimwengu wa viumbe. 13 Mungu anatimiza mapenzi yake katika dunia, ikuwe ni kwa ajili ya kuwaazibu watu, au kwa ajili ya kuonyesha wema wake. 14 Unapaswa kusikiliza Yobu! Nyamaza, usikilize maajabu ya Mungu. 15 Unajua jinsi Mungu anavyovipa amri yake, na kuyafanya umeme wa mawingu yake uangae? 16 Unajua jinsi mawingu yanavyoelea katika anga? Ndizo kazi za ajabu za yule anayekuwa mukamilifu wa maarifa! 17 Wewe unajiona umevaa nguo za joto sana, wakati upepo wa kusini unapovuma juu ya inchi. 18 Unaweza kuzitandaza mbingu kama yeye hata zikuwe ngumu kama kioo cha shaba? 19 Utufundishe tutakachomwambia Mungu; maana masemi yetu si wazi, tuko katika giza. 20 Yeye anahitaji kujulishwa kwamba ninataka kusema? Au mutu anaweza kujitakia kuangamizwa? 21 Kwa rafla mutu hawezi tena kuona waziwazi: Jua limefichwa nyuma ya mawingu, na upepo umesafisha anga! 22 Mwangaza muzuri unatokea upande wa kaskazini; Mungu amezungukwa na utukufu wa kutisha. 23 Mungu Mwenye Uwezo asiyeweza kufikiwa na mutu, uwezo na haki yake ni mukubwa. Amejaa haki wala hapotoshi sheria hata kidogo. 24 Kwa hiyo, watu wote wanamwogopa. Yeye hawajali watu wanaojiona kuwa wenye hekima. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo