Yobu 35 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Kisha Elihu akaendelea kusema: 2 Yobu, unaona jambo hili ni sawa? Unasema: “Mimi ni mwenye haki mbele ya Mungu.” 3 Tena unauliza: “Nimepata faida gani kama sikutenda zambi? Nimefaidika kuliko kama vile ningetenda zambi?” 4 Mimi nitakujibu wewe na warafiki zako vilevile. 5 Basi uangalie mbingu! Angalia mawingu yanayokuwa juu kuliko wewe! 6 Ukitenda zambi, Mungu ndiye unayemuzuru? Na kama ukizidisha makosa yako, unazani unamwumiza? 7 Kama wewe ni mwenye haki, unamupatia faida, au yeye anapokea kitu kutoka kwako? 8 Uovu wako utamuzuru mwanadamu kama wewe, haki yako itamufalia mwanadamu mwenzako. 9 Kwa sababu ya mateso mengi watu wanalia, wanaomba musaada kwa sababu ya mapigo ya wenye nguvu. 10 Lakini hakuna anayesema: “Yuko wapi Mungu, Muumba wangu, mwenye kunifanya nichangamuke usiku, 11 anayetuelimisha kuliko nyama, na kutufanya wenye hekima kuliko ndege!” 12 Watu wale wanaomba musaada lakini Mungu hawajibu, kwa sababu ya majivuno ya watu waovu. 13 Kweli Mungu hasikilizi kilio cha bure; Mungu Mwenye Uwezo hajali kilio kile. 14 Atakujibu namna gani wakati wewe unasema kwamba haumwoni na kwamba maneno yako iko mbele yake na wewe unamungojea! 15 Sasa, kwa vile Mungu anazuia hasira yake, wala hajali sana makosa ya watu, 16 Yobu anafungua kinywa kusema maneno matupu, anazidisha maneno bila akili. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo