Yobu 33 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Sasa, Yobu, sikiliza masemi yangu; sikiliza maneno yangu yote. 2 Sikia! Ninafumbua kinywa changu. Ulimi wangu utasema. 3 Nitasema kadiri ya usawa wa moyo wangu; ninayoyajua nitayasema kwa uaminifu. 4 Roho ya Mungu iliniumba, nayo pumzi ya Mungu Mwenye Uwezo inanipa uzima. 5 Unijibu, kama unaweza. Panga masemi yako vizuri mbele yangu, ushike musimamo wako. 6 Wewe na mimi ni sawa mbele ya Mungu; mimi vilevile niliumbwa kwa sehemu ya udongo. 7 Kwa hiyo hauna sababu ya kuniogopa; maneno yangu mazito hayatakulemea. 8 Kweli umesema, nami nikasikia; nimesikia yote uliyosema. 9 Wewe umesema hivi: “Mimi niko safi, wala sina kosa. Hakuna ubaya wowote katika moyo wangu. 10 Mungu ananitafutia sababu, ananiona kama adui yake. 11 Ananifunga miguu kwa minyororo, na kuchunguza hatua zangu zote.” 12 Lakini Yobu, ninakuambia pale umekosa. Mungu ni mukubwa kuliko mwanadamu. 13 Kwa nini unashindana naye, ukisema hatajibu ulizo lako moja? 14 Mungu anaweza kusema kwa njia moja au ingine lakini mutu hatambui. 15 Mungu anaongea na watu katika ndoto na maono, wakati usingizi muzito unapowapata, 16 wanaposinzia katika vitanda vyao. Halafu anawafungua watu masikio yao; anawatia hofu kwa maonyo yake, 17 wapate kuachana na matendo yao mabaya, na kuvunja kiburi chao. 18 Hivyo anamukinga mutu asiangamie katika shimo, maisha yake yasiangamie kwa upanga. 19 Mungu anamwazibu mutu kwa maumivu yanayomuweka katika kitanda, maumivu yanashika viungo vyake bila kukoma; 20 naye anapoteza hamu yote ya chakula, hata chakula ni chukizo kwake. 21 Mwili wake unakonda hata hawezi kutambuliwa, na mifupa yake iliyofichama ikatokea inje. 22 Yuko karibu sana kuingia ndani ya kaburi, na maisha yake karibu na wale wanaoleta kifo. 23 Lakini inawezekana kwamba malaika, ambaye ni mupatanishi mumoja kati ya maelfu, atakuwa karibu na mutu yule kwa kumufunulia jambo la kufanya. 24 Yule malaika anaweza kumwonea huruma na kumwomba Mungu: “Umwokoe asiingie katika shimo; nimepata ukombozi wake.” 25 Mwili wake utaweza kuwa tena kama kijana, ataweza kurudilia tena nguvu zake za ujana. 26 Kisha atamwomba Mungu na kukubaliwa, atakuja mbele yake kwa furaha, na Mungu atamurudishia utukufu wake. 27 Atashangilia mbele ya watu na kusema: “Nilitenda zambi na kupotosha usawa, nami sikuazibiwa kutokana na hayo. 28 Mungu aliniokoa nisiangamie katika shimo; nimebaki muzima na ninaona mwangaza.” 29 Sikia! Mungu anamufanyia mwanadamu haya yote, tena mara mbili, mara tatu. 30 Anamwokoa mwanadamu asiangamie katika shimo, aweze kuona mwangaza wa maisha. 31 Sikia Yobu, unisikilize kwa uangalifu; ukae kimya, nami nitasema. 32 Kama una la kusema, unijibu; sema, maana ninataka kukuona bila kosa. 33 Kama sivyo, nyamaza unisikilize, ukae kimya nami nikufundishe hekima. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo