Yobu 24 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Mbona Mungu Mwenye Uwezo hapangi wakati wa hukumu? Kwa nini wanaomujua hawajui hizo siku zake? 2 Watu wanaondoa vitambulisho vya mipaka ya mashamba, na wengine wanaiba makundi ya nyama na kuwafuga. 3 Wananyanganya wayatima punda wao, wanatwaa ngombe dume wa mujane kuwa rehani. 4 Wanasukuma wamasikini kandokando ya barabara; wamasikini wa dunia wanajificha mbele yao. 5 Kwa hiyo kama punda wa pori katika jangwa, wanatoka mapema kwenda kutumika, wakitafuta chakula kwa bidii, kusudi wapate chochote cha kukulisha watoto wao. 6 Wamasikini wanalazimishwa kuvuna mashamba ya wengine, wanaokota katika shamba la mizabibu la waovu. 7 Usiku kucha wanalala uchi bila nguo, wakati wa baridi hawana cha kujifunikia. 8 Wanalowana kwa mvua ya juu ya milima, wanajibanisha kwenye mawe kwa ukosefu wa makimbilio. 9 Kuna watu wanaoondoa watoto wayatima kwenye vifua vya mama yao. Wengine wanatwaa nguo ya masikini kuwa rehani. 10 Wamasikini wanatembea uchi, bila nguo; wenye njaa wanabeba miganda ya ngano. 11 Wanawatengenezea waovu mafuta yao, au kukamua divai bila hata kuionja. 12 Kutoka katika muji, kilio cha wanaokufa kinasikilika, na walioumizwa wanalalamika kuomba musaada. Lakini Mungu hasikilizi kabisa maombi yao. 13 Kuna wengine waovu wasiopenda mwangaza, wasiofahamu njia za mwangaza, na hawapendi kushika njia zake. 14 Mwuaji anaamuka asubui mapema, kwa kwenda kuwaua wamasikini na wakosefu, na usiku ukifika, kazi yake ni kuiba. 15 Muzinzi naye anangojea giza liingie, akisema: “Hakuna atakayeniona”; kisha anaficha uso wake kwa nguo. 16 Usiku wezi wanavunja nyumba, lakini muchana wanajifungia ndani; wala hawajui kabisa mwangaza ni nini. 17 Kwao wote giza kubwa ni mwangaza wa asubui; wao ni warafiki za vitisho vya giza kubwa. 18 Lakini munasema: “Waovu wanapelekwa haraka na mafuriko ya maji, makao yao yanabaki kuwa inchi iliyolaaniwa; hakuna anayeenda kwenye mashamba yao ya mizabibu.” 19 Kama vile teluji inavyoyeyuka katika joto na kipwa ndivyo kuzimu inavyotowesha waovu. 20 Maana muzazi wao anawasahau watu hao, hakuna atakayewakumbuka tena. Ndivyo uovu ulivyovunjika kama muti. 21 Waovu wanatesa wanawake wasiopata watoto wala hawawatendei vizuri wanawake wajane. 22 Mungu, kwa nguvu yake, anawaangamiza wenye uwezo; anasimama, nao wanakata tamaa ya kuishi. 23 Anawaacha waovu wajione salama, lakini macho yake yanachunguza mienendo yao. 24 Waovu wanafanikiwa kwa muda tu, kisha wanatoweka, wananyauka na kufifia kama vile jani, wanakatwa kama vile masuke ya ngano. 25 Nani basi, anayeweza kuhakikisha kwamba mimi ni mwongo na kuonyesha kwamba maneno yangu si kweli? |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo