Yobu 20 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Kisha Zofari wa inchi ya Namati akajibu: 2 Mafikiri yangu yananisukuma nikujibu, wala siwezi kujizuia tena. 3 Ninasikia maonyo nisiyoweza kuvumilia, lakini akili yangu inanisukuma nijibu. 4 Wewe labda umesahau jambo hili: kwamba tangu zamani Mungu alipomwumba mutu katika dunia, 5 mwovu atajiona ameshinda kwa muda tu, furaha ya asiyemwogopa Mungu ni ya muda mufupi tu! 6 Mwovu akiweza kupanda hata kufikia mbingu, na kichwa chake kufika kwenye mawingu, 7 atatupiliwa mbali kama mavi yake. Waliopata kumujua watajiuliza: “Yuko wapi?” 8 Atatoweka kama ndoto, asionekane tena, atafutikana kama maono ya usiku. 9 Aliyemwona, hatamwona tena, wala pale alipoishi hapatatambuliwa tena. 10 Yeye mwenyewe atarudisha mali yake yote, watoto wake wataomba huruma kwa wamasikini. 11 Japo alijisikia amejaa nguvu ya ujana, lakini italala pamoja naye katika mavumbi. 12 Katika kinywa chake uovu ni mutamu kama sukari, anauficha chini ya ulimi wake; 13 hataki kabisa kuuachilia, lakini anaushikilia katika kinywa chake. 14 Lakini unapofika ndani ya tumbo unakuwa muchungu, mukali kama sumu ya nyoka. 15 Mwovu anameza mali haramu na kuitapika; Mungu anaitoa ndani ya tumbo lake. 16 Ananyonya sumu ya nyoka na nyoka atamuuma na kumwua. 17 Hataona tena mitiririko ya asali na ya maziwa. 18 Ataacha matunda ya jasho lake. Hatakuwa na uwezo wa kuyaonja, 19 kwa sababu amewaangamiza wamasikini na kuwaachilia, amenyanganya nyumba ambazo hakuzijenga. 20 Kwa vile ulafi wake hauna mwisho, hataweza kuokoa kitu chochote cha lazima. 21 Kisha kula hakuacha hata makombo. Kwa hiyo fanaka yake yote haitadumu. 22 Atakapotajirika sana atapatwa na taabu, hasara itamupata kwa nguvu zote. 23 Akiwa anajishugulisha kwa kushibisha tumbo, Mungu atamuletea kasirani yake imutiririkie kama chakula chake. 24 Labda ataweza kuepuka upanga wa chuma, kumbe atachomwa na upanga wa shaba. 25 Mushale utachomolewa kutoka katika mwili wake; incha yake itatolewa katika mugongo wake ikingaa, vitisho vya kifo vitamupata. 26 Hazina zake zitaharibiwa, moto wa ajabu utamuteketeza; kilichobaki katika nyumba yake kitateketezwa. 27 Mbingu zitafichua uovu wake, dunia itajitokeza kumushambulia. 28 Mali zake zitanyanganywa katika siku ya kasirani ya Mungu. 29 Hii ndiyo sehemu ya mutu mwovu kutoka kwa Mungu, ndio mwisho aliopangiwa na Mungu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo