Yoane 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Ndoa katika muji wa Kana 1 Siku mbili zilipopita, kulikuwa ndoa katika muji wa Kana, katika Galilaya. Mama ya Yesu alikuwa pale. 2 Yesu alialikwa vilevile kwenye ndoa ile pamoja na wanafunzi wake. 3 Wakati divai ilipomalizika, mama ya Yesu akamwambia: “Hawana divai tena.” 4 Lakini Yesu akamujibu: “Mama, kuna maneno gani kati yako nami? Saa yangu haijatimia bado.” 5 Halafu mama yake akawaambia watumishi: “Mufanye kila kitu atakachowaambia.” 6 Pale kulikuwa mitungi sita iliyotengenezwa kwa mawe iliyotumiwa na Wayuda kwa kutilia maji ya kujitakasa. Ndani ya kila mumoja kuliweza kuingia yapata litre mia moja za maji. 7 Yesu akawaambia watumishi: “Mujaze mitungi hii na maji.” Nao wakaijaza kabisa. 8 Kisha Yesu akamwambia: “Muteke sasa kwa maji haya na muyapeleke kwa mukubwa wa karamu.” Watumishi wakayapeleka 9 kwa mukubwa wa karamu, akaonja yale maji yaliyogeuka kuwa divai. Mukubwa ule hakujua pahali divai ile ilipotoka, lakini watumishi walioleta maji walijua. Basi akamwita bwana-arusi, 10 na kumwambia: “Watu wote wanapatia waalikwa divai nzuri zaidi kwanza, kisha wakati wanapokwisha kunywa sana, wanawapatia ile isiyokuwa nzuri zaidi. Lakini wewe umechunga divai nzuri mpaka sasa.” 11 Ni vile Yesu alivyofanya kitambulisho chake cha kwanza katika Kana ya Galilaya. Pale alionyesha utukufu wake na wanafunzi wake wakamwamini. 12 Nyuma ya maneno yale, akaenda Kapernaumu pamoja na mama yake, wandugu zake na wanafunzi wake. Nao wakakaa kule siku chache. Yesu katika hekalu ( Mat 21.12-13 ; Mk 11.15-17 ; Lk 19.45-46 ) 13 Wakati sikukuu ya Pasaka ya Wayuda ilipokaribia, Yesu akaenda Yerusalema. 14 Akakuta watu katika hekalu wakiuzisha ngombe, kondoo na njiwa, na wengine wenye kubadilisha feza wakiikaa kwenye meza zao. 15 Basi akasokota kamba kuwa fimbo na kuwafukuza wote toka hekalu pamoja na kondoo na ngombe wao. Kisha akapindua meza za wenye kubadilisha feza na kuzimwanga chini. 16 Akawaambia wachuuzi wa njiwa: “Muondoshe vile vitu hapa. Musifanye nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya biashara!” 17 Wanafunzi wake wakakumbuka maneno haya yaliyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Upendo wangu kwa ajili ya nyumba yako unanichoma.” 18 Basi Wayuda wakamwuliza: “Utaonyesha kitambulisho gani kwa kutuhakikishia kwamba uko na haki ya kufanya hivi?” 19 Yesu akawajibu: “Mubomoe hekalu hili, nami nitalijenga katika siku tatu.” 20 Wayuda wakamwambia: “Hekalu hili lilijengwa kwa muda wa miaka makumi ine na sita, nawe utalijenga tena katika siku tatu?” 21 Lakini hekalu ambalo Yesu alisema juu yake lilikuwa mwili wake. 22 Wakati Yesu alipokwisha kufufuka, wanafunzi wake wakakumbuka kwamba alikuwa anasema juu ya jambo lile, wakaamini Maandiko Matakatifu na maneno yale aliyosema. Yesu anajua yote 23 Wakati ule Yesu alipokuwa Yerusalema kwa sikukuu ya Pasaka, watu wengi walimwamini kwa sababu waliona vitambulisho alivyofanya. 24 Lakini Yesu hakuwaaminia kwa sababu aliwajua wote vizuri. 25 Naye hakuhitaji kupewa ushuhuda juu ya mutu yeyote, kwa maana yeye mwenyewe alijua yanayokuwa ndani ya mioyo ya watu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo