Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Yoane 19 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002

1 Halafu Pilato akaamuru wamukamate Yesu na kumupiga fimbo.

2 Kisha kwa kumuchekelea, waaskari wakasokota taji na tawi lenye miiba na kumuvalisha nalo juu ya kichwa; vilevile wakamuvalisha nguo nyekundu-nyeusi.

3 Wakafika kila wakati mbele yake na kusema: “Jambo, Mufalme wa Wayuda.” Nao wakamupiga makofi.

4 Pilato akatoka tena inje na kuwaambia Wayuda: “Angalia, nitawaletea naye hapa inje kusudi mupate kujua kwamba mimi sioni hata sababu moja ya kumuhukumu.”

5 Basi Yesu akatoka inje, akivaa ile taji ya miiba na ile nguo nyekundu. Pilato akawaambia watu: “Mutu wenu huyu!”

6 Basi wakati wale wakubwa wa makuhani na walinzi walipomwona, wakapiga kelele, wakisema: “Umutundike juu ya musalaba! Umutundike juu ya musalaba!” Pilato akawaambia: “Mumutwae ninyi wenyewe na kumutundika, kwa maana mimi sioni sababu ya kumuhukumu.”

7 Wayuda wakamujibu: “Kufuatana na moja ya sheria zetu, mutu huyu anapaswa kuuawa, kwa sababu alijiita Mwana wa Mungu.”

8 Pilato aliposikia neno hili, akazidi kuogopa.

9 Akaingia tena katika nyumba yake na kumwuliza Yesu: “Wewe ni muzaliwa wa wapi?” Lakini Yesu hakumujibu neno.

10 Basi Pilato akamwambia: “Hautaki kusema nami? Wewe haujui kama mimi nina mamlaka ya kukufungua na mamlaka ya kukutundika juu ya musalaba?”

11 Yesu akamujibu: “Wewe hauna mamlaka yoyote juu yangu, isipokuwa tu yale uliyopewa na Mungu toka juu. Ni kwa hiyo, yule aliyenitoa kwako anabeba zambi kubwa zaidi.”

12 Tokea saa ile Pilato alitafuta njia ya kumufungua Yesu. Lakini Wayuda wakapiga kelele, wakisema: “Ukimufungua mutu huyu, wewe si rafiki wa Mufalme wa Roma. Kila mutu anayejifanya kuwa mufalme, anamupinga Mufalme wa Roma!”

13 Pilato aliposikia maneno haya, akamupeleka Yesu inje; akaikaa katika kiti cha hukumu kwenye nafasi inayoitwa katika Kiebrania “Gabata,” maana yake “Sakafu ya Mawe.”

14 Siku ile ilikuwa siku ya matayarisho ya Pasaka, karibu na saa sita. Pilato akawaambia Wayuda: “Mufalme wenu huyu!”

15 Lakini wakapiga kelele wakisema: “Umwue! Umwue! Umutundike juu ya musalaba!” Pilato akawauliza: “Munataka nimutundike mufalme wenu juu ya musalaba?” Wakubwa wa makuhani wakajibu: “Sisi hatuna mufalme mwingine isipokuwa Mufalme wa Roma.”

16 Halafu Pilato akamutoa Yesu kwao, kusudi atundikwe juu ya musalaba. Basi wakamukamata Yesu.


Yesu anatundikwajuu ya musalaba
( Mat 27.32-44 ; Mk 15.21-32 ; Lk 23.26-43 )

17 Yesu akaondoka katika muji akibeba musalaba wake mpaka kwenye nafasi inayoitwa katika Kiebrania “Golgota”, maana yake: “Kilima cha Mufupa wa Kichwa.”

18 Waaskari wakamutundika Yesu juu ya musalaba kule pamoja na watu wengine wawili, mumoja kila upande na Yesu katikati.

19 Pilato akaamuru andiko liandikwe na kuwekwa juu ya musalaba. Nalo liliandikwa hivi: “Yesu wa Nazareti, Mufalme wa Wayuda.”

20 Pahali pale Yesu alipotundikwa palikuwa karibu na muji, kwa hiyo Wayuda wengi walisoma andiko lile. Nalo lilikuwa limeandikwa katika Kiebrania, Kilatini na Kigriki.

21 Basi wakubwa wa makuhani wa Wayuda wakamwambia Pilato: “Usiandike: ‘Mufalme wa Wayuda,’ lakini uandike hivi: ‘Mutu huyu alisema, Mimi ni Mufalme wa Wayuda!’ ”

22 Pilato akajibu: “Yale niliyoandika, yameandikwa!”

23 Waaskari walipokwisha kumutundika Yesu juu ya musalaba wakakamata nguo zake na kuzigawanya katika sehemu ine, wakimupa kila askari sehemu moja. Wakakamata vilevile kanzu yake iliyokuwa bila mushono, iliyofumwa kwa kipande kimoja tu tokea juu mpaka chini.

24 Waaskari wakaambiana: “Tusipasue kanzu hii, lakini tuipigie kura, kusudi tujue itakuwa ya nani.” Mambo haya yalifanyika kusudi Maandiko Matakatifu yanayosema hivi yatimie: “Waligawanya nguo zangu nayo kanzu yangu wakaipigia kura.” Mambo hayo ndiyo waaskari waliyofanya.

25 Mama ya Yesu, dada ya mama yake, Maria muke wa Kleopa na Maria wa muji wa Magdala walikuwa wamesimama karibu na musalaba wake.

26 Basi wakati Yesu alipoona mama yake pale na yule mwanafunzi aliyemupenda, akisimama karibu, akamwambia mama yake: “Mama, sasa huyu ndiye mwana wako.”

27 Na kisha akamwambia yule mwanafunzi: “Sasa huyu ndiye mama yako.” Na tokea saa ile, mwanafunzi yule alimupeleka Maria kwake.


Kufa kwa Yesu
( Mat 27.45-56 ; Mk 15.33-41 ; Lk 23.44-49 )

28 Kisha, Yesu akiwa anajua kwamba mambo yote yametimia, akasema hivi kusudi Maandiko Matakatifu yatimie: “Ninasikia kiu.”

29 Pale kulikuwa chombo chenye kujaa divai yenye kuchacha. Basi waaskari wakachovya kikausho ndani ya ile divai, wakakifungia juu ya tawi la hisopo na kukiweka kwa kinywa chake.

30 Wakati Yesu alipokwisha kumeza ile divai, akasema: “Yote yametimilika!” Kisha akainamisha kichwa na kukata roho.


Askari anatoboa ubavu wa Yesu

31 Siku ile ilikuwa ya matayarisho ya siku ya Sabato iliyofuata. Kwa sababu hii Wayuda hawakutaka maiti za wale waliotundikwa zibaki juu ya misalaba kwa maana siku ile ilikuwa kubwa sana. Kwa hiyo wakamwomba Pilato ruhusa kwamba miguu ya wale waliotundikwa ivunjwe kusudi wakufe mbio na maiti zao ziondoshwe.

32 Basi waaskari walikuja, wakavunja miguu ya mutu wa kwanza na kisha miguu ya yule wa pili aliyetundikwa pamoja na Yesu juu ya musalaba.

33 Lakini walipofika kwenye Yesu, walikuta amekwisha kufa; kwa hiyo hawakumuvunja miguu.

34 Lakini askari mumoja akamuchoma mukuki katika ubavu; mara moja damu na maji vikatoka.

35 Mutu aliyeona mambo hayo ndiye anayeyashuhudia, nao ushuhuda wake ni wa kweli. Na anajua kama anasema ukweli, kusudi mupate kuamini vilevile.

36 Mambo haya yalifanyika kusudi Maandiko Matakatifu yanayosema hivi yatimie: “Hakuna hata mufupa wake mumoja utakaovunjwa.”

37 Na tena Maandiko mengine Matakatifu yanasema: “Watamwangalia yule waliyemutoboa kwa mukuki.”


Yesu anazikwa
( Mat 27.57-61 ; Mk 15.42-47 ; Lk 23.50-56 )

38 Nyuma ya mambo hayo, Yosefu, mutu wa Arimatea, akamwomba Pilato ruhusa ya kuondoa maiti ya Yesu. (Yosefu alikuwa mumoja wa wanafunzi wa Yesu lakini kwa siri, kwa sababu aliwaogopa wakubwa wa Wayuda.) Pilato akamuruhusu. Basi Yosefu akaenda na kuondoa maiti ya Yesu.

39 Naye Nikodemo, yule aliyemwendea Yesu siku moja usiku, alikuja vilevile. Alikuwa akileta yapata kilo makumi tatu ya marasi yaliyochangwa na udi.

40 Wote wawili wakatwaa maiti ya Yesu, wakaifunga na vitambaa vyenye kupakaliwa mafuta zenye harufu nzuri sawa na desturi za maziko za Wayuda.

41 Kulikuwa bustani pale walipomutundika Yesu, na katika bustani ile kulikuwa kaburi jipya, mulimokuwa hamujazikwa mutu.

42 Na kwa kuona siku ile ilikuwa ya matayarisho ya siku ya Sabato ya Wayuda na kaburi lilikuwa karibu, wakamuzika Yesu mule.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ