Yoane 11 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kufa kwa Lazaro 1 Kulikuwa mutu mumoja aliyeitwa Lazaro, muzaliwa wa Betania aliyepatwa na ugonjwa. Wadada zake Maria na Marta walikaa katika kijiji kile. 2 (Huyu Maria ndiye yule aliyemupakaa Bwana marasi na kupanguza miguu yake na nywele zake, na ni Lazaro kaka yake ndiye alikuwa mugonjwa.) 3 Hawa wadada wawili wakatuma habari hii kwa Yesu: “Bwana, rafiki yako mupendwa ni mugonjwa.” 4 Wakati Yesu aliposikia habari hii, akasema: “Tukio la ugonjwa huu si la kumwua, lakini shabaha yake ni kuonyesha utukufu wa Mungu na kusudi Mwana wa Mungu atukuzwe.” 5 Yesu aliwapenda Marta na dada yake pamoja na Lazaro. 6 Yesu aliposikia kwamba Lazaro yuko mugonjwa, akabaki tena kwa muda wa siku mbili pahali alipokuwa. 7 Kisha akawaambia wanafunzi wake: “Turudi Yudea.” 8 Wanafunzi wakamwambia: “Mwalimu, hakujapita siku nyingi tokea pale Wayuda walipotaka kukutupia mawe, na sasa unataka kwenda tena kule!” 9 Yesu akajibu: “Katika muchana kuna saa kumi na mbili. Kama mutu akitembea wakati wa muchana hajikwai, kwa sababu anaona mwangaza wa dunia hii. 10 Lakini kama mutu akitembea usiku, anajikwaa, kwa sababu hana mwangaza ndani yake.” 11 Yesu alipokwisha kusema maneno haya, akaongeza kuwaambia: “Rafiki yetu Lazaro amelala usingizi, lakini ninakwenda kumwamusha.” 12 Basi wanafunzi wake wakamujibu: “Bwana, ikiwa amelala usingizi, atapona.” 13 Yesu alikuwa akisema kwamba Lazaro amekufa, lakini wanafunzi wake walizani kwamba amesema juu ya kulala usingizi. 14 Basi Yesu akawaambia waziwazi: “Lazaro amekufa. 15 Nami ninafurahi kwa ajili yenu, kwa sababu sikukuwa kule, kusudi mupate kuamini. Tuende kule anapokuwa.” 16 Basi Toma, anayeitwa “Pacha,” akawaambia wanafunzi wenzake: “Nasi tuende vilevile, tukufie pamoja naye.” Yesu ni ufufuko na uzima 17 Wakati Yesu alipofika, akamukuta Lazaro amekwisha kuzikwa tangu siku ine. 18 Kati ya kijiji cha Betania na Yerusalema kulikuwa umbali yapata kilometre tatu. 19 Wayuda wengi walikuwa wamekuja kwa Marta na Maria kwa kuwafariji kwa ajili ya kifo cha kaka yao. 20 Marta aliposikia kama Yesu anakuja, akaenda kumupokea katika njia, lakini Maria alibaki ndani ya nyumba. 21 Marta akamwambia Yesu: “Bwana, kama ungekuwa hapa, kaka yangu hangekufa. 22 Lakini ninajua kwamba hata sasa, kitu chochote utakachomwomba Mungu, atakupa.” 23 Yesu akamwambia: “Kaka yako atafufuka.” 24 Marta akajibu: “Ninajua kwamba atafufuka wakati watu watakapofufuka siku ya mwisho.” 25 Yesu akamwambia: “Mimi ni ufufuko na uzima, kwa maana anayeniamini, ataishi tena hata ikiwa amekufa. 26 Vilevile yeyote anayeishi ndani yangu na kuniamini, hatakufa hata milele. Unaamini maneno haya?” 27 Akamujibu: “Ndiyo, Bwana, ninaamini kwamba wewe ni Kristo, Mwana wa Mungu, yule aliyepaswa kuja katika dunia.” Yesu anafufua Lazaro 28 Marta alipokwisha kusema maneno hayo, akaenda kumwita dada yake Maria na kumwambia kwa siri: “Mwalimu amekuja, na anakuita.” 29 Wakati Maria aliposikia hivi, akaondoka upesi kwenda kumukuta. 30 (Yesu alikuwa hajaingia bado katika kijiji, alikuwa angali pahali Marta alipomukuta.) 31 Wakati wale Wayuda waliokuwa ndani ya nyumba pamoja na Maria kwa kumufariji walipomwona akisimama upesi na kutoka, wakamufuata. Walizani kama anakwenda kulia kwenye kaburi. 32 Maria alipofika pale Yesu alipokuwa na kumwona, akaanguka kwenye miguu yake na kusema: “Bwana, kama ungekuwa hapa, kaka yangu hangekufa.” 33 Wakati Yesu alipomwona akilia, na wale Wayuda waliokuja pamoja naye wakilia vilevile, akasisimua kwa huzuni nyingi na kufazaika. 34 Akauliza: “Mulimuzika wapi?” Wakamujibu: “Bwana, kuja uone.” 35 Yesu akatoa machozi. 36 Halafu Wayuda wamoja wakasema: “Angalia namna alivyomupenda kweli!” 37 Lakini wengine kati yao wakasema: “Yeye aliyeponyesha kipofu, asingeweza kuzuia mutu huyu asikufe?” 38 Basi Yesu akasisimua tena kwa huzuni, na kwenda kwenye kaburi. Kaburi lile lilikuwa pango lililofungwa na jiwe kubwa. 39 Yesu akasema: “Muondoshe jiwe hili!” Marta, dada wa yule marehemu, akamujibu: “Bwana, anaanza sasa kunuka, kwa maana ni siku ine sasa tangu alipozikwa!” 40 Yesu akamwambia: “Sikukuambia kwamba ukiamini utaona utukufu wa Mungu?” 41 Basi wakaondosha lile jiwe. Yesu akainua macho juu, akasema: “Baba, ninakushukuru kwa sababu umenisikia. 42 Na ninajua kwamba unanisikia siku zote, lakini ninasema hivi kwa sababu ya watu hawa wanaokusanyika hapa kusudi wapate kuamini kwamba wewe ndiwe uliyenituma.” 43 Wakati alipokwisha kusema maneno haya, akaita kwa sauti kubwa, akisema: “Lazaro, toka inje.” 44 Halafu yule marehemu akatoka inje, akiwa amefungwa mikono na miguu kwa vitambaa, na uso wake ukifunikwa na nguo. Yesu akawaambia: “Mumufungue, mumwache ajiendee.” Shauri la kumwua Yesu ( Mat 26.1-5 ; Mk 14.1-2 ; Lk 22.1-2 ) 45 Wayuda wengi kati ya wale waliokuja kwa Maria, na walioona mambo Yesu aliyofanya, wakamwamini. 46 Lakini wengine kati yao wakawaendea Wafarisayo na kuwaambia mambo Yesu aliyofanya. 47 Basi wakubwa wa makuhani na Wafarisayo wakakusanya Baraza yao Kubwa, na kusema: “Tufanye nini kwa kuona mutu huyu anaonyesha vitambulisho vingi? 48 Kama tukimwachilia kuendelea hivi, watu wote watamwamini, nao Waroma watakuja kuharibu hekalu letu na taifa letu!” 49 Halafu mumoja kati yao, jina lake Kayafa, aliyekuwa Kuhani Mukubwa mwaka ule, akasema: “Hamujui kitu, ninyi! 50 Hamufahamu kwamba ni afazali mutu mumoja akufe kwa ajili ya watu, kuliko taifa zima kuangamizwa?” 51 (Yeye hakusema maneno haya kutokana na mawazo yake mwenyewe; lakini kwa maana yeye ndiye aliyekuwa Kuhani Mukubwa mwaka ule, alitabiri kwamba Yesu atakufa kwa ajili ya taifa la Wayuda. 52 Na kufa kwake si kwa ajili ya taifa hili tu, lakini vilevile kwa ajili ya watoto wa Mungu waliosambazwa, kusudi apate kuwaunga katika umoja.) 53 Basi tangia siku ile wakakusudia kumwua Yesu. 54 Kwa sababu hii Yesu hakutembea tena akijionyesha waziwazi kati ya Wayuda. Kisha akajiendea pamoja na wanafunzi wake katika inchi iliyokuwa karibu na jangwa katika muji unaoitwa Efuraimu. Nao wakabaki kule. 55 Sikukuu ya Wayuda ya Pasaka ilikuwa karibu. Basi watu wengi toka katika vijiji wakaenda Yerusalema kusudi wajitakase mbele ya Pasaka. 56 Wakamutafuta Yesu, na wakaulizana hivi ndani ya hekalu: “Munawaza nini? Atakuja kwa karamu au hapana?” 57 Nao wakubwa wa makuhani na Wafarisayo walikuwa wametoa amri kwamba mutu akijua pahali Yesu alipokuwa, alete habari kusudi wapate kumufunga. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo