Yeremia 31 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kurudi kwa Waisraeli kwao 1 Kutakuja siku ambazo nitakuwa Mungu wa jamaa zote za Waisraeli, nao watakuwa watu wangu. –Ni ujumbe wa Yawe. 2 Yawe anasema hivi: Watu walioponyoka kuuawa, nilionyesha neema yangu kwao katika jangwa. Wakati Israeli alipotafuta kwenda kupumzika, 3 mimi Yawe nilimutokea kwa mbali. Nami nimekupenda kwa mapendo ya milele, kwa hiyo nimeendelea kuwa mwema kwako. 4 Nitakurudisha katika hali mupya, ewe binti Israeli! Utazitwaa tena ngoma zako, nawe utajitokeza tena kwa kucheza na wenye shangwe. 5 Utapanda tena mizabibu juu ya milima ya Samaria; walimaji watapanda mbegu na kuyafurahia mazao yake! 6 Maana kutakuja siku ambapo walinzi watalalamika hivi katika vilima vya Efuraimu: Musimame, tupande kwenda Sayuni kwa Yawe, Mungu wetu. 7 Maana Yawe anasema hivi: Mushangilie kwa furaha kwa ajili ya Yakobo, mupige vigelegele kwa ajili ya taifa kubwa, mutangaze, musifu na kusema: Yawe ameokoa watu wake, ameleta ukombozi kwa wale waliobaki kati ya Waisraeli! 8 Nitawarudisha kutoka inchi ya kaskazini, nitawakusanya kutoka miisho ya dunia. Wote watakuwa pale; hata vipofu na vilema, wanawake wenye mimba na wanaosikia maumivu ya kuzaa; kundi kubwa sana la watu litarudi hapa. 9 Watarudi wakiwa wanatoa machozi, nami nitawaongoza nikiwafariji; nitawapitisha kando ya vijito vya maji, katika njia iliyonyooka ambamo hawatajikwaa; maana mimi nimekuwa baba wa Israeli, Efuraimu ni muzaliwa wangu wa kwanza. 10 Enyi mataifa, musikilize neno langu mimi Yawe, mulitangaze katika visanga vya mbali, museme hivi: Aliyemusambaza Israeli, atamukusanya, atamutunza kama muchungaji anavyotunza kondoo wake. 11 Maana mimi Yawe nimemukomboa Yakobo, nimemwokoa kutoka kwa wenye nguvu kuliko yeye. 12 Watakuja na kuimba kwa sauti juu ya mulima Sayuni, watapata utukufu juu ya wema wangu mimi Yawe, kwa ajili ya ngano, divai na mafuta ninavyowapa, kwa ajili ya kondoo na ngombe vilevile; maisha yao yatakuwa kama bustani iliyotiliwa maji, wala hawataregea tena. 13 Halafu wabinti zao watafurahi na kucheza, vijana na wazee watashangilia kwa furaha. Nitageuza maombolezo yao kuwa furaha, nitawafariji na kuwapa furaha pahali pa huzuni. 14 Nitawashibisha makuhani kwa nyama wenye kunona, watu wangu watatosheka kwa wema wangu. –Ni ujumbe wa Yawe. Huruma ya Mungu kwa Israeli 15 Yawe anasema hivi: Sauti imesikilika katika muji wa Rama, maombolezo na kilio cha uchungu. Rakeli anawalilia watoto wake, wala hataki kufarijiwa kwa ajili yao, maana wote hawako tena. 16 Yawe anasema hivi: Acha kulia, panguza machozi yako, maana utapata malipo kwa kazi yako. –Ni ujumbe wa Yawe.– Watoto wenu watarudi kutoka inchi ya waadui zenu. 17 Kuna matumaini kwa siku zenu zinazokuja, maana watoto wenu watarudia katika inchi yao. –Ni ujumbe wa Yawe. 18 Nimesikia Efuraimu akilalamika hivi: Umeniazibu vikali, maana nilikuwa kama mwana-ngombe asiyezoea nira. Unigeuze nami nitakugeukia, maana wewe ndiwe Yawe, Mungu wangu. 19 Maana kisha kukuasi, niligeuka toka zambi zangu, na kisha kufundishwa, nilijilaumu, nikapata haya na kufezeheka, maana nilibeba haya za ujana wangu. 20 Efuraimu ni mwana wangu mupendwa; yeye ni mutoto wangu ninayemupenda sana. Ndiyo maana kila mara ninapomutisha, ninaendelea kumukumbuka. Moyo wangu unamwelekea kwa wema; hakika nitamuhurumia. –Ni ujumbe wa Yawe. 21 Weka kitambulisho katika njia zako, simika nguzo za kukuongoza, ukumbuke vema ile njia kubwa, barabara uliyopita ndani yake ukienda. Ewe Israeli rudi, rudi kwa nyumba katika miji yako. 22 Utasitasita mpaka wakati gani, ewe binti usiyekuwa mwaminifu? Maana, mimi nimefanya kitu kipya katika dunia; mwanamuke anamulinda mwanaume. Baraka katika siku zinazokuja 23 Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Nitakapowafanikisha tena watu wa Israeli, wao watatangaza tena katika inchi ya Yuda na katika miji yake wakisema: Yawe akubariki, ewe makao ya haki; akubariki, ee mulima mutakatifu! 24 Halafu watu wa Yuda na miji yake yote, walimaji na wachungaji wanaopitapita na makundi yao watakaa huko pamoja. 25 Waliochoka nitawachangamusha, na waregevu nitawapa nguvu. 26 Ndiyo maana mutu ataweza kusema hivi: Niliamuka nikatambua kwamba usingizi wangu ulinifalia sana. 27 Siku zinakuja ambapo nitaijaza inchi ya Israeli na inchi ya Yuda watu na nyama kama vile mulimaji anavyopanda mbegu. 28 Na kadiri nilivyokuwa mwangalifu kuwaongoa, kuwabomoa, kuwaangusha, kuwaharibu na kuwatesa, ndivyo nitakavyokuwa mwangalifu kwa kuwapanda na kuwajenga. –Ni ujumbe wa Yawe. 29 Siku hizo watu hawatasema tena: Wazee walikula matunda mabichi ya mizabibu, na meno ya watoto ndiyo yanaumizwa. 30 Lakini kila mumoja atakufa kwa sababu ya zambi zake mwenyewe; ni yule tu atakayekula matunda mabichi ya mizabibu ndiye meno yake yataumizwa. 31 Siku zinakuja ambapo nitafanya agano jipya na watu wa Israeli na watu wa Yuda. 32 Agano hili halitakuwa kama lile nililofanya na babu zao nilipowatoa kwa mukono wangu kutoka Misri; agano hilo walilivunja, ingawa mimi nilikuwa Bwana wao. 33 Kisha siku hizo, nitafanya agano hili na Waisraeli. Nitaiweka sheria yangu ndani yao, na kuiandika katika mioyo yao. Mimi nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. Ni mimi Yawe ninayesema hivyo. 34 Wala hawatafundishana tena kila mutu na jirani yake, na kila mutu na ndugu yake na kusema “Mumujue Yawe”, kwa sababu wote, wadogo kama vile wakubwa, watanijua mimi Mungu. Maana nitawasamehe makosa yao, wala sitazikumbuka tena zambi zao. 35 Yawe, yule aliyepanga jua liangaze muchana, mwezi na nyota viangaze usiku, na anayevumisha mawimbi ndani ya bahari, yule ambaye jina lake ni Yawe wa majeshi, anasema hivi: 36 Ikiwa itanifikia kuvunja mipango ile, halafu nitaweza vilevile kukomesha kizazi cha Waisraeli, wasiitwe tena taifa langu siku zote. –Ni ujumbe wa Yawe. 37 Yawe anasema hivi: Kama mbingu zinaweza kupimwa, na misingi ya dunia kuchunguzwa, basi, nitawatupilia wazao wa Israeli, kwa sababu ya mambo yote waliyotenda. 38 Siku zinakuja ambapo muji huu wa Yerusalema utajengwa upya kwa ajili ya Yawe, kutokea kwenye munara wa Hananeli mpaka kwenye mulango wa Pembe. 39 Nayo kamba ya kupima itanyooshwa moja kwa moja mpaka kwenye mulima Garebu, kisha itazungushwa mpaka Goa. 40 Bonde lote walimozikwa wafu na kutupiwa majivu, mashamba yote, mpaka kijito cha Kidroni, mpaka pembe ya mulango wa Farasi kuelekea upande wa mashariki, litakuwa eneo takatifu kwa Yawe. Hakuna kitakachoharibiwa humo wala kubomolewa tena milele. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo