Yeremia 22 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Ujumbe juu ya jamaa ya kifalme ya Yuda 1 Yawe anasema hivi: Kwenda kwa jamaa ya kifalme ya Yuda, na utoe ujumbe huu kule: 2 Wewe mufalme wa Yuda unayetawala kwa kiti cha kifalme cha Daudi pamoja na wakubwa wa serikali yako na watu wako wanaopita katika milango hii, musikilize neno la Yawe. 3 Yawe anasema hivi: Mufuate sheria yangu na kutenda kwa haki. Muokoe kila mutu aliyenyanganywa mali zake toka katika mikono ya mutesaji. Musiwatendee vibaya au kwa ukali wageni, wayatima na wajane, wala musimwange damu ya mutu asiyekuwa na kosa kwa nafasi hii. 4 Kama mukishika neno hili nililowaambia, basi wafalme watakaotawala kwa kiti cha kifalme cha Daudi wataendelea kuingia wakipitia milango ya nyumba hii ya kifalme. Watapita pamoja na wakubwa wa serikali yao na watu wao, wakipanda juu ya farasi na magari yenye kukokotwa na farasi. 5 Lakini kama hamutatii maneno haya, ninaapa kwa nafsi yangu mwenyewe kwamba nafasi hii itakuwa mabomoko. –Ni ujumbe wa Yawe. 6 Yawe anasema hivi juu ya nyumba ya kifalme ya Yuda: Ingawa unaonekana vizuri kama inchi ya Gileadi, kama vichwa vya milima ya Lebanoni, ninaapa kwamba nitakufanya kuwa jangwa, ukuwe muji usiokaliwa na watu. 7 Nitawatayarisha waangamizaji wakufikie, kila mumoja akishika silaha yake. Watazikata nguzo zako nzuri za mierezi, na kuzitumbukiza katika moto. 8 Na watu wengi wa mataifa watapita karibu na muji huu, kila mumoja atamwuliza mwenzake: Kwa nini Yawe ameutendea muji huu mukubwa hivi? 9 Nao watajibiana hivi: Ni kwa sababu wakaaji wake walivunja agano la Yawe, Mungu wao, wakaabudu miungu mingine na kuitumikia. Ujumbe juu ya Salumu 10 Musimulilie yule aliyekufa, musiomboleze kwa ajili yake. Lakini mumulilie kwa uchungu yule anayekwenda mbali kwa sababu hatarudi tena kuiona inchi yake. 11 Maana, Yawe anasema hivi juu ya Salumu mwana wa Yosia, mufalme wa Yuda aliyetawala kwa pahali pa baba yake Yosia, na ambaye aliondoka pahali hapa: Salumu hatarudi tena pahali hapa, 12 lakini atakufia kulekule alipelekwa katika utumwa. Yeye hataiona tena inchi hii. Ujumbe juu ya Yoyakimu 13 Ole kwako Yoyakimu, wewe unayejijengea nyumba kwa njia isiyokuwa ya haki, na kuiwekea magorofi kwa njia isiyofuata sheria ya Mungu. Unayewatumikisha watu bure pasipo kuwalipa mishahara yao. 14 Wewe unayesema: Nitajijengea nyumba kubwa, yenye vyumba vikubwa vya magorofi. Kisha unaifanyia madirisha, ukafunika kuta zake kwa mbao za mierezi, na kuipaka rangi nyekundu! 15 Unazani umekuwa mufalme kwa kujenga na mierezi? Baba yako alikula na kunywa, alifuata sheria yangu na kutenda mambo ya haki, na mambo yake yaliendeka vizuri. 16 Aliwapatia haki wamasikini na wakosefu, na mambo yake yaliendeka vizuri. Si hivi ndivyo kunijua mimi? –Ni ujumbe wa Yawe.– 17 Lakini macho yako wewe na moyo wako, vinaelekea tu mapato yasiyokuwa ya haki. Unamwanga damu ya wasiokuwa na kosa, nawe unawatesa watu na kuwatendea kwa ukali. 18 Kwa hiyo, Yawe anasema hivi juu ya Yoyakimu mwana wa Yosia, mufalme wa Yuda: Wakati atakapokufa, hakuna atakayeomboleza juu yake, akisema: Yowe, ndugu yangu! Yowe, dada yangu! Wala hakuna atakayemulilia, akisema: Yowe, bwana wetu! Yowe, muheshimiwa wetu! 19 Yeye atazikwa sawa nyama: atakokotwa na kutupiliwa mbali, inje ya milango ya Yerusalema. Hasira itakayoupata Yerusalema 20 Enyi watu wa Yerusalema, mupande kwa milima ya Lebanoni mupige kelele, munyanyue sauti zenu huko kwenye uwanja wa Basani; mulalamike kutoka milima ya Abarimu, maana wapenzi wenu wote wameangamizwa. 21 Yawe aliongea nanyi mulipokuwa katika ustawi, lakini ninyi mukasema: Hatutasikiliza. Hii ndiyo tabia yenu tangu utoto wenu, hamujatii sauti ya Yawe. 22 Waongozi wenu watapeperushwa na upepo, wapenzi wenu watapelekwa katika uhamisho. Halafu mutapata haya na kufazaika, kwa sababu ya uovu wenu wote. 23 Enyi wakaaji wote wa Lebanoni, ninyi munaokaa salama kati ya miti ya mierezi, mutaugua sana wakati mutakaposhikwa na uchungu unaokuwa kama wa mwanamuke anayezaa! Hukumu ya Mungu juu ya Konia 24 Yawe anasema hivi: Kama vile ninavyoishi, hata kama wewe Konia mwana wa Yoyakimu, mufalme wa Yuda, ungekuwa wa lazima kwangu kama vile pete yangu ya muhuri ninayovaa kwa mukono wangu wa kuume, ningekuvua. 25 Nitakutoa katika mikono ya wale wanaovizia maisha yako, ndiyo mikono ya wale unaowaogopa, hata katika mikono ya Nabukadneza, mufalme wa Babeli na watu wake. 26 Nitakupeleka mbali katika inchi ya kigeni, wewe pamoja na mama yako muzazi. Mutakuwa watumwa katika inchi hiyo ambamo ninyi wote wawili hamukuzaliwa, nanyi mutakufia kulekule. 27 Mutatamani kwa hamu kubwa kurudi katika inchi hii, lakini hamutarudi. 28 Mbona huyu mutu Konia, amekuwa kama chungu kilichovunjika, ambacho kinazarauliwa na kutupwa inje? Kwa nini yeye na watoto wake wamefukuzwa, wametupwa katika inchi wasiyoijua? 29 Ee inchi, ee inchi, ee inchi! Sikia neno la Yawe! 30 Yawe anasema hivi: Muandike mutu huyu kwamba hana watoto, ni mutu ambaye hatafanikiwa katika maisha yake. Maana hakuna hata mumoja wa wazao wake atakayekiikalia kiti cha kifalme cha Daudi na kutawala tena katika Yuda. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo