Yeremia 19 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mufano wa mutungi 1 Yawe akaniambia hivi: Kwenda kununua mutungi kwa mufinyanzi. Kisha, uwatwae wakubwa wamoja wa watu na makuhani waongozi wamoja. 2 Halafu uende pamoja nao katika bonde la Mwana wa Hinomu, kwa kupitia mulango unaoitwa mulango wa Vigae. Ukifika huko, utangaze maneno ninayokuambia. 3 Utasema hivi: Musikilize neno la Yawe, enyi wafalme wa Yuda nanyi wakaaji wa Yerusalema. Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Kweli ninaleta hasara kwenye nafasi hii, hata kila mumoja atakayesikia habari ile, atastajabu. 4 Kwa maana watu wameniacha mimi na kuchafua nafasi hii kwa kufukizia miungu mingine ubani; miungu ambayo wao wenyewe, babu zao wala wafalme wa Yuda hawaijui. Zaidi ya ile wamejaza pahali hapa damu ya watu wasiokuwa na kosa, 5 wanamujengea mungu Bali mazabahu, kwa kusudi la kuwachoma wana wao kama sadaka ya kuteketezwa kwa moto kwa ajili ya mungu yule. Mimi sikuwaamuru hata kidogo kufanya vile, wala halikunifikia katika roho. 6 Kwa hiyo, siku zinakuja ambazo nafasi hii haitaitwa tena Tofeti, wala bonde la Mwana wa Hinomu, lakini itaitwa bonde la Mauaji. –Ni ujumbe wa Yawe. 7 Vilevile kwa nafasi hii nitaivuruga mipango ya watu wa Yuda na ya watu wa Yerusalema. Nitawatoa washindwe na kuuawa kwa panga na waadui zao, wale wanaovizia maisha yao. Nazo maiti zao nitaziacha kuwa chakula cha ndege na nyama wa pori. 8 Nitaufanya muji huu kuwa pahali pa kushangaza; nitaufanya kuwa kitu cha kuzomewa. Kila mutu anayepita karibu nao atashangaa na kuuzomea kwa sababu ya hasara zote zitakazowapata. 9 Waadui wao wanavizia maisha yao watauzunguka muji ule kwa vita. Wataleta taabu na masumbuko hata watu watakula wenzao. Nitawafanya wakule miili ya wana na wabinti zao. 10 Kisha wewe utavunja ule mutungi mbele ya watu wale watakaoenda pamoja nawe, 11 na kuwaambia kwamba: Yawe wa majeshi, anasema hivi: Nitavunjavunja watu hawa na muji huu sawa vile mutu anavyovunja chombo cha mufinyanzi, hata kisiweze kutengenezwa tena. Watu watazikwa Tofeti, kwa sababu hapatakuwa pahali pengine pa kuzikia. 12 Vile ndivyo nitakavyotendea nafasi hii na wakaaji wake. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitaufanya muji huu kama Tofeti. 13 Nyumba za Yerusalema na nyumba za wafalme wa Yuda, ndizo nyumba zote ambazo juu ya paa zao watu walifukiza ubani kwa kutambikia makundi ya nyota, na kuitolea miungu mingine sadaka za divai, zote zitageuzwa kuwa chafu kama Tofeti. 14 Nyuma ya mambo haya, Yeremia aliondoka Tofeti, pahali ambapo Yawe alipomutuma aende kutoa unabii, akaenda kusimama katika kiwanja cha nyumba ya Yawe, akawatangazia watu wote maneno haya: 15 Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Mimi nitaleta juu ya muji huu na juu ya vijiji vyote vinavyokuwa kandokando yake hasara zote nilizotangaza juu yake, kwa sababu wakaaji wake ni wenye mioyo migumu, nao wamekataa kusikia maneno yangu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo