Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Walawi 21 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Maisha ya ukuhani

1 Yawe akamwambia Musa: Uwaambie makuhani, wana wa Haruni, kwamba kusikuwe mutu yeyote kati yao atakayejichafua kwa kugusa maiti ya watu wa jamaa yake,

2 isipokuwa kama ni maiti ya ndugu yake wa karibu, ni kusema mama yake, baba yake, mwana wake, binti yake, ndugu yake

3 au dada yake ambaye (aliyekuwa wa jamaa yake ya karibu), naye hajaolewa bado.

4 Yeye, akiwa mwenye madaraka katika jamaa yake, asijichafue.

5 Wazao wa Haruni wasijinyoe upaa kwa kuomboleza wala wasikate pembe za ndevu zao wala kujichanja chanjo juu ya mwili.

6 Watakuwa watakatifu kwa Mungu wao wala wasichafue jina la Mungu wao. Maana wao ndio wanaotolea zile sadaka Yawe anazopewa kwa moto, ni kusema chakula cha Mungu. Basi, wanapaswa kuwa watakatifu.

7 Kwa sababu kuhani ametakaswa kwa ajili ya Mungu wake, asioe kahaba wala mwanamuke asiyekuwa bikira wala aliyefukuzwa na mume wake.

8 Utamutambua kuhani kuwa aliyetakaswa, maana yeye ndiye anayetolea sadaka ya mukate wa Mungu wako. Utamutambua kuwa mutakatifu, maana mimi Yawe ninayekutakasa wewe ni mutakatifu.

9 Binti wa kuhani yeyote akijichafua kwa kufanya ukahaba, atateketezwa kwa moto maana anamuchafua baba yake.

10 Kuhani Mukubwa ni mukubwa kati ya wandugu zake, naye amemiminiwa mafuta ya kupakaa juu ya kichwa chake, na kutakaswa kusudi avae nguo takatifu. Asiache nywele zake kuwa ovyo wala asipasue nguo zake kwa kuomboleza.

11 Asikaribie maiti wala kujichafua kwa maiti hata kama ni ya baba yake au ya mama yake.

12 Kwa sababu ametakaswa kwa kupakwa mafuta ya Mungu wake juu ya kichwa, basi asiondoke katika Pahali Patakatifu wala asipachafue. Mimi ni Yawe.

13 Kuhani Mukubwa anaweza tu kumwoa binti ambaye ni bikira.

14 Haruhusiwi kuoa mwanamuke mujane, mwanamuke asiyekuwa bikira, wala kahaba. Anapaswa kuoa bikira kutoka watu wake mwenyewe

15 kusudi asichafue watoto wake mwenyewe. Mimi ni Yawe niliyemutakasa.

16 Yawe akamwambia Musa:

17 Umwambie Haruni hivi: Muzao wako yeyote katika vizazi vyote vinavyokuja ambaye ana kilema juu ya mwili, haruhusiwi kukaribia na kunitolea mimi Mungu wake sadaka ya mukate.

18 Mutu yeyote anayekuwa na kilema, kipofu, aliyelemaa, mwenye uso uliokatwakatwa, mwenye kiungo kirefu kuliko kawaida,

19 mwenye muguu au mukono uliovunjika,

20 mwenye kigongo, mutu mufupi kuliko kawaida, asiyeona sawasawa, mwenye kivimba, mwenye upele au mutu anayekuwa towashi, asikaribie kumutolea Mungu mukate wake.

21 Muzao yeyote wa kuhani Haruni mwenye kilema asikaribie kwa kunitolea sadaka za kuteketezwa kwa moto. Kwa vile ana kilema, basi, asikaribie kunitolea mimi Mungu mukate wangu.

22 Mutu huyo anaweza kula mukate wa Mungu wake, vitu vitakatifu na vile vitakatifu kabisa.

23 Lakini asilikaribie lile pazia wala ile mazabahu maana ana kilema, asipate kuchafua Pahali Patakatifu, kwa sababu mimi Yawe ndiye ninayewatakasa.

24 Musa akamwelezea Haruni na wana wake na Waisraeli wote mambo hayo yote.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ