Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Waamuzi 17 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Sanamu za Mika

1 Kulikuwa mutu mumoja kule katika milima ya Efuraimu, jina lake Mika.

2 Siku moja akamwambia mama yake: “Vile vikoroti vya feza elfu moja na mia moja ulivyoibiwa, nawe ukamulaani aliyekuiba nami nikiwa ninasikia, mimi niko navyo. Mimi ndiye niliyevibeba.” Mama yake akasema: “Mwana wangu ubarikiwe na Yawe.”

3 Mika akamurudishia mama yake hivyo vikoroti vya feza elfu moja na mia moja. Mama yake akasema: “Kusudi laana niliyotoa isikupate, feza hii ninaitoa kwa Yawe kwa kutengeneza sanamu ya kuchonga na ya kuyeyushwa. Sasa ninakurudishia vikoroti vya feza.”

4 Mika alipomurudishia mama yake hiyo feza, mama yake akatwaa vikoroti vya feza mia mbili akamupatia mufua feza ambaye alifua sanamu ya kuchonga na ya kuyeyushwa. Sanamu hiyo ikawekwa katika nyumba ya Mika.

5 Mutu huyo, Mika alikuwa na pahali pake pa ibada. Alitengeneza kizibao cha kuhani na sanamu, kisha akamufanya mumoja wa watoto wake kuwa kuhani wake.

6 Siku hizo hakukukuwa mufalme katika Israeli. Kila mutu alifanya chochote alichotaka.

7 Wakati ule kulikuwa kijana mumoja Mulawi katika muji wa Betelehemu katika inchi ya Yuda.

8 Kijana huyo akaondoka Betelehemu katika inchi ya Yuda, akaenda kutafuta pahali pengine pa kuishi. Katika safari yake akafika katika nyumba ya Mika katika inchi ya milima ya Efuraimu.

9 Mika akamwuliza: “Umetoka wapi?” Naye akamujibu: “Mimi ni Mulawi, kutoka katika muji wa Betelehemu katika inchi ya Yuda. Nitakaa popote nitakapopata nafasi ya kukaa kama mugeni.”

10 Mika akamwambia: “Kaa pamoja nami, ukuwe kwangu kama baba na kuhani wangu. Nitakulipa vikoroti kumi vya feza kila mwaka na nguo pamoja na mahitaji yako.”

11 Yule Mulawi akakubali, akakaa kule na kuwa kama mumoja wa wana wa Mika.

12 Naye Mika akamufanya kijana huyo Mulawi kuwa kuhani wake kule katika nyumba yake.

13 Kisha akasema: “Sasa ninajua kwamba Yawe atanifanikisha maana nina kijana huyu Mulawi kama kuhani wangu.”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ