Waamuzi 13 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kuzaliwa kwa Samusoni 1 Waisraeli walitenda tena uovu mbele ya Yawe, naye akawaacha watawaliwe na Wafilistini kwa miaka makumi ine. 2 Kulikuwa mutu mumoja kule Zora, wa kabila la Dani, jina lake Manoa. Muke wake alikuwa tasa. 3 Siku moja, malaika wa Yawe akamutokea yule mwanamuke, akamwambia: “Wewe ni tasa, hauna watoto. Lakini utapata mimba na kumuzaa mutoto mwanaume. 4 Kwa hiyo ukuwe mwangalifu, usikunywe divai au kileo wala usikule kitu chochote kinachohesabiwa kuwa kichafu, 5 kwa maana utabeba mimba na kuzaa mutoto mwanaume. Nywele za mutoto huyo zisinyolewe hata kidogo, maana atakuwa Munaziri wa Mungu tangu kuzaliwa kwake. Naye ataanza kuwakomboa Waisraeli toka katika mikono ya Wafilistini.” 6 Mwanamuke huyo akaenda kumwambia mume wake: “Mutu wa Mungu ambaye sura yake ilikuwa kama ya malaika wa Mungu alinitokea. Sikumwuliza anatoka wapi wala hakuniambia jina lake. 7 Lakini aliniambia kwamba nitabeba mimba na kuzaa mutoto mwanaume. Aliniamuru nisikunywe divai au kileo wala kula chochote kinachohesabiwa kuwa kichafu, maana mutoto huyo atakuwa Munaziri wa Mungu tangu kuzaliwa kwake mpaka atakapokufa.” 8 Kisha Manoa akamwomba Yawe, akisema: “Ninakuomba, ee Yawe, umutume tena yule mutu wako uliyemutuma kusudi atufundishe mambo tunayopaswa kumutendea huyo mutoto atakayezaliwa.” 9 Yawe akalisikia ombi la Manoa, na yule malaika wa Mungu akamwendea tena yule mwanamuke alipokuwa akiikaa katika shamba. Lakini mume wake Manoa hakukuwa pamoja naye. 10 Mwanamuke akakimbia upesi, akamwambia mume wake: “Yule mutu aliyenijia siku ile amenitokea tena.” 11 Manoa akafuatana naye mpaka kwa mutu huyo, akamwuliza: “Wewe ni yule mutu aliyezungumuza na mwanamuke huyu?” Yule mutu akamujibu: “Ni mimi.” 12 Kisha Manoa akasema: “Sasa maneno yako yatakapotimia ni mambo gani tutakayofuata kwa ajili ya huyo mutoto? Tutafanya nini kwa ajili yake?” 13 Malaika wa Yawe akamwambia Manoa: “Muke wako atapaswa kushika yote niliyomwambia: 14 asionje mazao yoyote ya muzabibu, wala asikunywe divai au kileo wala kula chochote kinachohesabiwa kuwa kichafu. Yote niliyomwamuru, ayafuate.” 15 Manoa akamwambia huyo malaika wa Yawe: “Tafazali, ukae kidogo tukutayarishie mwana-mbuzi.” 16 Yule malaika wa Yawe akamwambia Manoa: “Hata kama mukinilazimisha kukaa, sitakula chakula chenu. Lakini kama ukipenda, tayarisha sadaka ya kuteketezwa kwa moto, umutolee Yawe.” Manoa hakujua kwamba huyo alikuwa malaika wa Yawe. 17 Basi, Manoa akamwambia huyo malaika wa Yawe: “Utuambie jina lako kusudi tukuheshimu wakati maneno yako yatakapotimia.” 18 Malaika wa Yawe akamujibu: “Kwa nini unataka kujua jina langu? Ni la ajabu.” 19 Hapo Manoa akatayarisha mwana-mbuzi na sadaka, akaviweka juu ya jiwe apate kumutolea Yawe anayefanya maajabu. 20 Basi wakati Manoa na muke wake walipokuwa wanaangalia ndimi za moto zikipanda juu mbinguni kutoka kwenye mazabahu, wakamwona malaika katika ndimi hizo akipanda kwenda mbinguni. Basi Manoa na muke wake wakainama uso mpaka chini. 21 Manoa akajua kwamba huyo alikuwa malaika wa Yawe. Malaika hakumutokea tena Manoa na muke wake. 22 Basi, Manoa akamwambia muke wake: “Hakika tutakufa, maana tumemwona Mungu.” 23 Lakini muke wake akamujibu: “Kama Yawe angetaka kutuua hangepokea sadaka yetu ya kuteketezwa kwa moto na ya ngano; wala hangetuonyesha mambo hayo wala kutuambia maagizo.” 24 Kisha muke wa Manoa akazaa mutoto mwanaume, naye Manoa akamupa jina la Samusoni. Mutoto huyo akakomaa naye Yawe akamubariki. 25 Roho wa Yawe akaanza kumusukuma akiwa kule Mahane-Dani, kati ya muji wa Zora na wa Estaoli. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo