Nahumu 3 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Ole wako muji wa mauaji! Umejaa udanganyifu mutupu na wizi tele, haukomi hata kidogo kunyanganya. 2 Sikia! Mulio wa fimbo, mashindo ya magurudumu, vishindo vya farasi na ngurumo za magari ya vita! 3 Waaskari wapanda-farasi wanashambulia, panga na mikuki inametameta; waliouawa hawana hesabu, kuna maiti nyingi sana; watu wanajikwaa juu ya maiti! 4 Ninawe! Wewe umekuwa kama kahaba. Umewashawishi watu, ewe binti wa uchawi, uliyeyafanya mataifa kuwa watumwa kwa ukahaba wako, na watu wa mataifa kwa uchawi wako. 5 Mimi Yawe wa majeshi ninasema nitakushambulia; nitapandisha nguo yako mpaka kwenye kichwa, niyaache mataifa yauone uchi wako, falme zitaona haya yako. 6 Nitakutupia uchafu, na kukuzaraulisha, na kukufanya kuwa mushangao kwa watu. 7 Kisha wote watakaokuona watakukimbia wakisema: Ninawe umeangamizwa, ni nani atakayekuomboleza? Nani atakayekufariji? 8 Wewe Ninawe, ni bora kuliko Tebe, muji uliojengwa pembeni ya muto Nili? Tebe ulizungukwa na maji, bahari ilikuwa kikingio chake, maji yalikuwa ukuta wake! 9 Inchi ya Kushi ilikuwa nguvu yake; nayo Misri vilevile, tena bila mwisho, watu wa Puti na Libya waliusaidia. 10 Hata hivyo, ulikamatwa mateka, watu wake wakapelekwa katika uhamisho. Hata watoto wake walipondwapondwa katika maingilio ya kila barabara; watu wake wenye heshima waligawanywa kwa kuwapigia kura, wakubwa wake wote walifungwa minyororo. 11 Ninawe, nawe vilevile utalewa; utamukimbia adui na kujaribu kujificha. 12 Kuta zako zote ni kama tini za kwanza; zikitikiswa zinamwangukia mwenye kula katika kinywa. 13 Angalia, waaskari wako ni wanawake tu. Milango ya inchi yako ni wazi mbele ya waadui zako; moto umeteketeza kabisa vifungio vyake. 14 Muteke maji mukuwe tayari kwa kuzungukwa na vita; muimarishe vikingio vyenu. Muponde matope, mutayarishe furu ya kuchomea matofali! 15 Lakini kule vilevile moto utawateketeza, upanga utawamaliza kabisa; utawamaliza kama nzige wanavyokula. Muongezeke kama nzige, mwongezeke kama mapanzi! 16 Wachuuzi wako waliongezeka kuliko nyota; lakini sasa wametoweka kama vile mapanzi wanavyoruka. 17 Wakubwa wako ni kama mapanzi, majemadari wako kama kundi la nzige; wakati wa baridi wanakaa kwenye kuta, lakini jua linapotokea, wanaruka, wala hakuna anayejua nafasi walipokwenda. 18 Ewe mufalme wa Asuria, wachungaji wako wamelala, waheshimiwa wako wamesinzia. Watu wako wametawanyika kwenye milima, wala hakuna yeyote wa kuwakusanya. 19 Hakuna wa kutunza mapigo yako, vidonda vyako ni vya kifo. Wote wanaosikia habari zako wanashangilia. Maana ni nani aliyeponyoka kila mara uovu wako? |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo