Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Mwanzo 29 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Yakobo anafika kwa Labani

1 Yakobo aliendelea na safari yake, akafika katika inchi za watu wa upande wa mashariki.

2 Siku moja akaona kisima katika mbuga, na kando yake makundi matatu ya kondoo wakipumzika. Kondoo walikuwa wanakunyweshwa kutoka kisima hicho kilichokuwa kimefunikwa kwa jiwe kubwa.

3 Kwa kawaida, makundi yote ya kondoo yalipokusanyika, wachungaji walirudisha lile jiwe kwa pamoja toka kwenye kisima na kuwakunywesha kondoo. Halafu walifunika tena kisima kwa jiwe lile.

4 Yakobo akawauliza wachungaji: “Wandugu zangu, mumetoka wapi?” Wakamujibu: “Tumetoka Harani.”

5 Naye akawauliza: “Munamufahamu Labani mwana wa Nahori?” Wakamujibu: “Tunamufahamu.”

6 Akaendelea kuwauliza: “Yuko muzima?” Nao wakamujibu: “Yeye ni muzima; hata binti yake Rakeli, yule kule anakuja na kondoo wake!”

7 Kisha Yakobo akawaambia: “Ninaona ingaliki muchana, na si wakati wa kuwakusanya kondoo pamoja. Basi, mukunyweshe kondoo maji, muende kuwachunga.”

8 Lakini wao wakamwambia: “Hatuwezi kufanya hivyo mpaka makundi yote yakuwe yamekusanyika pamoja, jiwe limeviringishwa juu ya kisima, halafu tutakunywesha kondoo.”

9 Yakobo alipokuwa bado anazungumuza na hao wachungaji, Rakeli akafika na kondoo wa baba yake, maana yeye ndiye aliyekuwa akiwachunga.

10 Yakobo akamwona Rakeli, binti ya mujomba wake Labani. Akaona kondoo ambao vilevile ni wa mujomba wake. Akakwenda na kuliviringisha lile jiwe kwenye mudomo wa kisima. Akakunywesha maji kundi la mujomba wake.

11 Kisha Yakobo akamubusu Rakeli na kulia kwa sauti.

12 Akamujulisha Rakeli kwamba yeye ni wa jamaa ya baba yake, na kwamba ni mwana wa Rebeka. Rakeli akakimbia mbio kwa nyumba akamwarifu baba yake.

13 Labani aliposikia habari za mwipwa wake Yakobo, alikwenda mbio kumupokea, akamukumbatia, akamubusu, akamukaribisha ndani ya nyumba yake. Yakobo akamwelezea Labani mambo yote yaliyotokea.

14 Naye Labani akasema: “Hakika, wewe ni jamaa yangu, damu moja nami!” Yakobo akakaa naye kwa muda wa mwezi mumoja.


Yakobo anaoa wabinti za Labani

15 Siku moja Labani akamwambia Yakobo: “Wewe ni jamaa yangu lakini hiyo haisemi kwamba utanitumikia bure. Uniambie unataka mushahara gani!”

16 Sasa, Labani alikuwa na wabinti wawili: mukubwa anayeitwa Lea na mudogo anayeitwa Rakeli.

17 Lea alikuwa na macho zaifu, lakini Rakeli alikuwa muzuri na wa kupendeza.

18 Yakobo akamupenda Rakeli; kwa hiyo akamwambia Labani: “Nitakutumikia miaka saba kwa ajili ya Rakeli, binti yako mudogo.”

19 Labani akamwambia: “Afazali nimwoeshe Rakeli kwako wewe kuliko kumwoesha kwa mutu mwingine yeyote. Endelea kuishi nami.”

20 Basi, Yakobo akamutumikia Labani miaka saba kwa ajili ya Rakeli, lakini kwake muda ule ulikuwa kama siku chache, kwa vile alivyomupenda Rakeli.

21 Kisha Yakobo akamwambia Labani: “Muda wangu umetimia, kwa hiyo unipe muke wangu.”

22 Basi, Labani akafanya karamu na kuwaalika watu wote wa kule.

23 Lakini magaribi, Labani akatwaa Lea, binti yake mukubwa, na kumupeleka kwa Yakobo. Yakobo akalala naye.

24 (Labani akamutoa Zilpa, mujakazi wake, akuwe mutumishi wa Lea.)

25 Asubui, Yakobo akatambua kwamba ni Lea! Basi, akamwuliza Labani: “Umenitendea jambo gani? Si nilikutumikia kwa ajili ya Rakeli? Mbona basi, umenidanganya?”

26 Labani akamujibu: “Katika inchi yetu hatufanyi hivyo. Si desturi yetu kumwoesha binti mudogo mbele ya mukubwa.

27 Umutimizie Lea siku zake saba za ndoa, nasi tutakupa Rakeli kwa utumishi wa miaka saba mingine.”

28 Yakobo akakubali. Na Yakobo alipomutimizia Lea siku zake saba, Labani akamupa Rakeli, binti yake mudogo akuwe muke wake.

29 (Labani akamutoa Biliha, mujakazi wake, akuwe mujakazi wa Rakeli).

30 Basi, Yakobo akalala na Rakeli vilevile. Lakini Yakobo akamupenda Rakeli kuliko Lea. Akamutumikia Labani miaka mingine saba.


Watoto wa Yakobo

31 Yawe alipoona kwamba Lea anachukiwa, akamujalia watoto; lakini Rakeli alikuwa tasa.

32 Lea akapata mimba, akazaa mutoto mwanaume, akamwita Rubeni, akisema: “Yawe ameona mateso yangu; bila shaka sasa mume wangu atanipenda.”

33 Lea akapata mimba tena, akazaa mutoto mwanaume, akamwita Simeoni, akisema: “Yawe amenipa mutoto mwingine mwanaume kwa sababu amesikia jinsi ninavyochukiwa.”

34 Akapata mimba mara nyingine, akazaa mutoto mwanaume, akamwita Lawi, akisema: “Wakati huu mume wangu atajiunga nami, maana nimemuzalia watoto watatu wanaume.”

35 Lea akapata mimba tena, akazaa mutoto mwanaume, akamwita Yuda, akisema: “Mara hii nitamusifu Yawe.” Kisha Lea akaacha kuzaa.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ