Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Mika 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Mungu atatawala watu wote kwa amani
( Isa 2.1-4 )

1 Kutakuja wakati ambapo mulima wa nyumba ya Yawe utakuwa mukubwa kuliko milima yote. Utanyanyuliwa juu ya vilima vyote. Watu wengi watakimbilia kule,

2 mataifa mengi yataufikia na kusema: Tuende juu kwenye mulima wa Yawe, tuende katika nyumba ya Mungu wa Yakobo, kusudi atufundishe njia zake, nasi tuzifuate. Maana sheria itatoka kule Sayuni; na neno la Yawe kule Yerusalema.

3 Mungu atatoa hukumu kati ya mataifa mengi, atakata mashauri ya mataifa makubwa ya mbali. Nayo yatafua mapanga yao kuwa majembe, na mikuki yao kuwa visu vya kuvuna. Taifa halitapigana na taifa lingine, wala hayatafanya tena mazoezi ya vita.

4 Kila mutu atakaa kwa amani chini ya miti ya tini na mizabibu yake, bila kutishwa na mutu yeyote. –Maneno haya yanatoka katika kinywa cha Yawe wa majeshi.

5 Mataifa mengine yanafuata njia zao, kwa kuitegemea miungu yao, lakini sisi tunafuata njia zetu kwa kumutegemea Yawe, Mungu wetu, milele na milele.


Waisraeli watarudi kutoka katika utumwa

6 Siku ile, nitawakusanya waliolemewa, nitawakusanya waliopelekwa katika uhamisho, watu wale ambao niliwaazibu. –Ni ujumbe wa Yawe.–

7 Hao waliolemewa ndio watakaobaki wazima; hao waliopelekwa katika uhamisho watakuwa taifa lenye nguvu. Yawe atawatawala kwenye mulima Sayuni, tangu wakati ule na hata milele.

8 Nawe kilima cha Yerusalema, wewe munara wa Sayuni, ambamo Mungu anafanya ulinzi juu ya watu wake, kama muchungaji juu ya kondoo wake, wewe utakuwa tena muji wenye mamlaka sawa zamani. Yerusalema utakuwa tena muji mukubwa wa mufalme.

9 Sasa kwa nini munalia kwa sauti? Hamuna mufalme tena? Mushauri wenu ametoweka? Munalalamika kwa uchungu, kama mwanamuke anayezaa!

10 Enyi watu wa Sayuni, mulie na kugaagaa kama mwanamuke anayezaa! Maana sasa mutaondoka katika muji huu muende kukaa katika mbuga, mutakwenda mpaka Babeli. Lakini kule, mutaokolewa. Kule Yawe atawakomboa toka katika makucha ya waadui zenu.

11 Mataifa mengi yamekusanyika kwa kuwashambulia. Yanasema: Muache muji wao uchafuliwe, nasi tufurahie kuona uharibifu wa Sayuni!

12 Lakini wao hawafahamu mawazo ya Yawe wala hawaelewi mupango wake: kwamba amewakusanya pamoja, kama miganda pahali pa kupepetea.

13 Yawe anasema: Enyi watu wa Sayuni, musimame muwakanyagekanyage! Nitawapatia nguvu kama ngombe dume mwenye pembe za chuma na kwato za shaba. Mutawasaga watu wa mataifa mengi; mutanitolea mimi mapato yao, mutanitolea mali zao mimi Bwana wa dunia yote.

14 Mujikusanye enyi watu wa Yerusalema; mukisema: Tumeshambuliwa, tumesongwa; naye mutawala wa Israeli wanamupiga fimbo kwenye shavu.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ