Matayo 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kujaribiwa kwa Yesu ( Mk 1.12-13 ; Lk 4.1-13 ) 1 Kisha Roho Mutakatifu akamwongoza Yesu kwenda katika jangwa kusudi ajaribiwe na Shetani. 2 Naye Yesu alipomaliza kufunga kula chakula kwa muda wa siku makumi ine, muchana na usiku, akasikia njaa. 3 Shetani akamufikia na kumwambia: “Kama wewe ni Mwana wa Mungu, amuru mawe haya yageuke kuwa mikate.” 4 Yesu akamujibu: “Imeandikwa hivi katika Maandiko Matakatifu: ‘Mutu hawezi kuishi kwa mukate tu, lakini kwa njia ya kushika kila neno Mungu analosema.’ ” 5 Halafu Shetani akamupeleka katika Yerusalema, muji mutakatifu, akamusimamisha kwenye pembe la juu sana la hekalu, na kumwambia: 6 “Kama wewe ni Mwana wa Mungu, ujitupe chini; kwa maana imeandikwa: ‘Mungu atawaamuru wamalaika wake na watakubeba katika mikono yao, kusudi muguu wako usijikwae juu ya jiwe.’ ” 7 Yesu akamujibu: “Imeandikwa hivi vilevile: ‘Usimujaribu Bwana Mungu wako.’ ” 8 Shetani akamupeleka tena mpaka juu ya mulima murefu, akamwonyesha falme zote za dunia na utajiri wao. 9 Halafu akamwambia: “Nitakupa hivi vyote, kama ukipiga magoti mbele yangu na kuniabudu.” 10 Lakini Yesu akamwambia: “Toka wewe, Shetani! Kwa maana imeandikwa: ‘Umwabudu Bwana Mungu wako na umutumikie yeye peke yake.’ ” 11 Basi Shetani akamwacha Yesu, nao wamalaika wakakuja kushugulika naye. Mwanzo wa mahubiri katika Galilaya ( Mk 1.14-15 ; Lk 4.14-15 ) 12 Yesu aliposikia kwamba Yoane ametiwa katika kifungo, akaenda zake Galilaya. 13 Yeye akatoka Nazareti, akaenda kukaa Kapernaumu, pembeni ya ziwa la Galilaya, katika wilaya ya Zebuluni na ya Nafutali, kusudi yatimie 14 maneno yaliyosemwa kwa njia ya nabii Isaya: 15 “Inchi ya Zebuluni na ya Nafutali, kufuata barabara inayokwenda kwenye ziwa, ngambo ya magaribi ya Yordani, katika jimbo la Galilaya, inchi ya watu wa mataifa mengine. 16 Watu hao wanaokaa katika giza, mwangaza umewatokea! Hao wanaoishi katika inchi yenye giza nzito sana ya lufu, wameona mwangaza mukubwa.” 17 Tangia wakati huo Yesu akaanza kuhubiri, akisema: “Mugeuke toka zambi zenu, kwa maana Ufalme wa mbinguni umekaribia!” Yesu anawaita wavuvi wane wamufuate ( Mk 1.16-20 ; Lk 5.1-11 ) 18 Yesu alipokuwa akitembea pembeni ya ziwa la Galilaya, akawaona wavuvi wawili, waliokuwa wandugu wa tumbo, Simoni (aliyeitwa Petro) na ndugu yake Andrea. Walikuwa wakitupa nyavu katika ziwa. 19 Yesu akawaambia: “Munifuate, nami nitawaweka kwa kazi ya kuopoa watu.” 20 Mara moja wakaacha nyavu zao, na kumufuata. 21 Yesu alipoendelea mbele kidogo, akawaona wandugu wengine wawili, Yakobo na Yoane, waliokuwa wana wa Zebedayo. Walikuwa ndani ya chombo pamoja na baba yao Zebedayo, wakitengeneza nyavu zao. Yesu akawaita. 22 Na mara moja wakaacha chombo pamoja na baba yao, wakamufuata Yesu. 23 Yesu alizunguka katika Galilaya yote akifundisha katika nyumba zao za kuabudia, akihubiri Habari Njema ya Ufalme. Aliponyesha watu waliokuwa na magonjwa yote na uzaifu wa kila namna. 24 Habari zake zikavuma katika inchi yote ya Suria. Wakamuletea watu wote walioteswa na magonjwa mbalimbali na wenye maumivu ya kila namna, wenye pepo, wenye kifafa na wenye kupooza, naye Yesu akawaponyesha. 25 Makundi mengi ya watu yakamufuata kutoka Galilaya, inchi ya Miji Kumi, Yerusalema, Yudea, na toka ngambo ya mashariki ya muto Yordani. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo