Marko 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mufano wa mupandaji wa mbegu ( Mat 13.1-9 ; Lk 8.4-8 ) 1 Yesu alianza kufundisha tena pembeni ya ziwa la Galilaya. Kundi kubwa la watu walikusanyika karibu naye, kwa hiyo akaingia ndani ya chombo na kuikaa mule. Chombo kilikuwa katika ziwa na watu walisimama inchi kavu, pembeni ya ziwa. 2 Yesu akawafundisha mambo mengi akitumia mifano. Yeye akawaambia hivi katika mafundisho yake: 3 “Musikilize! Mutu mumoja alikwenda kupanda mbegu. 4 Alipokuwa akipanda mbegu katika shamba, zimoja zikaanguka pembeni ya njia, nao ndege wakakuja na kuzikula. 5 Zingine zikaanguka pahali penye mawe pasipokuwa udongo mwingi. Mbegu zile zikaota upesi kwa sababu hapakukuwa udongo mwingi. 6 Wakati jua lilipokuwa kali, likazichoma, na kwa sababu hazikukuwa na mizizi mikubwa zikakauka. 7 Mbegu zingine zilianguka katikati ya miiba. Ile miiba ikaota na kuzisonga mbegu hata hazikuweza kutoa kitu. 8 Lakini mbegu zingine zikaanguka katika udongo muzuri, mimea ikaota, ikakomaa na kuzaa matunda: zimoja zikazaa punje makumi tatu, zingine makumi sita na zingine punje mia moja.” 9 Kisha akawaambia: “Mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie!” Kusudi la kutumia mifano ( Mat 13.10-17 ; Lk 8.9-10 ) 10 Wanafunzi kumi na wawili wa Yesu pamoja na watu waliokuwa pembeni yake walipokuwa peke yao, wakamwuliza awaelezee maana ya mifano ile. 11 Yesu akawajibu: “Ninyi mumefunuliwa kujua siri ya Ufalme wa Mungu, lakini watu wengine wanaokuwa inje ya kikundi chenu wanasikia mambo yote kwa njia ya mifano, 12 kusudi ‘Wapate kuangalia, lakini wasione; nao wapate kusikia, lakini wasikuwe na ufahamu, kusudi wasipate kumugeukia Mungu na kusamehewa.’ ” Yesu anaeleza mufano wa mupandaji ( Mat 13.18-23 ; Lk 8.11-15 ) 13 Yesu akaongeza kuwaambia: “Kama musipoelewa mufano huu, namna gani mutaelewa mifano mingine? 14 Mupandaji anapanda Neno la Mungu. 15 Nafasi ile mbegu zilipoanguka pembeni ya njia, ni mufano wa watu wanaosikia Neno la Mungu, lakini mara moja Shetani anakuja na kuondoa lile Neno lililopandwa ndani yao. 16 Udongo wenye mawe, pahali mbegu zilipoanguka ni mufano wa watu wanaosikia Neno la Mungu, na mara moja wanalipokea kwa furaha. 17 Lakini halizami ndani yao kama mizizi; wanalishika kwa muda mufupi tu. Wakati taabu na mateso vinapowafikia kwa ajili ya Neno la Mungu, mara moja wanaanguka. 18 Udongo wenye miiba, pahali mbegu zilipoanguka, ni mufano wa wale wanaosikia Neno la Mungu, 19 lakini masumbuko ya dunia hii, udanganyifu wa mali, na tamaa za namna nyingine vikiwaingia, vinasonga lile Neno linalokuwa ndani yao na kulizuiza kuzaa matunda. 20 Nao udongo muzuri, walimopanda mbegu, ni mufano wa watu wanaosikia Neno la Mungu na kulipokea. Nao wanazaa matunda; wamoja matunda makumi tatu, wengine makumi sita na wengine mia moja.” Mufano wa tua ( Lk 8.16-18 ) 21 Kisha Yesu akawaambia: “Taa inaletwa kwa kufunikiwa chini ya kitunga au chini ya kitanda? Si wanaiweka juu ya kinara? 22 Ni hivi vilevile hakuna chochote kinachofichwa kitakachokosa kuonekana wazi, wala hakuna siri itakayokosa kufunuliwa waziwazi. 23 Mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie!” 24 Yesu akawaambia tena: “Muangalie vizuri maneno munayosikia! Mungu atawapimia na kipimo kile munachowapimia wengine, na kuwaongezea hata zaidi. 25 Kwa maana anayekuwa na kitu, ataongezewa kingine; lakini asiyekuwa na kitu, ataondolewa hata kidogo anachokuwa nacho.” Mufano wa mbegu zinazoota zenyewe 26 Yesu akaendelea kusema: “Ufalme wa Mungu unafanana na mutu mumoja aliyepanda mbegu katika shamba lake. 27 Kila siku alilala na kuamuka na mbegu ziliota na kukomaa. Lakini hakujua namna gani mbegu zilivyoota. 28 Udongo wenyewe unaotesha mimea; kwanza majani, halafu masuke na kisha ngano zinazokomaa ndani ya masuke. 29 Wakati ngano zinapokomaa, mutu anazivuna, kwa maana ni wakati wa mavuno.” Mufano wa mbegu ndogo sana ya haradali ( Mat 13.31-32 , 34 ; Lk 13.18-19 ) 30 Yesu akasema tena: “Tufananishe Ufalme wa Mungu na nini? Au tuulinganishe na mufano gani? 31 Unafanana na mbegu ya haradali. Inapopandwa katika udongo ni ndogo sana kuliko mbegu zote za dunia. 32 Lakini ikiisha kupandwa, inaota na kuwa kubwa zaidi kuliko mimea yote. Inatoa matawi makubwa hata ndege wanaweza kujenga chicha zao juu yake, kwenye kivuli chake.” 33 Yesu aliwafundisha watu kwa mifano mingi ya namna hii kwa kadiri walivyoweza kuelewa. 34 Hakusema nao pasipo kutumia mifano lakini alipokuwa pamoja na wanafunzi wake peke yao, aliwafasiria mambo yote. Yesu anatuliza zoruba ( Mat 8.23-27 ; Lk 8.22-25 ) 35 Na ilipotimia magaribi siku ile ile, Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Tuvuke ngambo ingine ya ziwa.” 36 Basi wanafunzi wakaaga kundi la watu, wakaingia ndani ya chombo Yesu alimokuwa na kuondoka pamoja naye. Na vyombo vingine vikamusindikiza. 37 Zoruba kali ikavuma ndani ya ziwa, maji yakajitupatupa ndani ya chombo hata kikaanza kujaa. 38 Yesu alikuwa upande wa nyuma wa chombo, akilala usingizi akilalisha kichwa juu ya mufuko wa kuegemea. Wanafunzi wake wakamwamusha na kumwambia: “Mwalimu, haikuhangaishi kuona sisi tunakufa?” 39 Yesu akaamuka, akakaripia ile zoruba na kuiambia ziwa: “Kimya! Tulizana!” Basi zoruba ikakoma na kukakuwa kimya kabisa. 40 Kisha Yesu akawaambia wanafunzi: “Sababu gani munaogopa? Mpaka sasa hamujakuwa na imani?” 41 Halafu wakaogopa sana, nao wakaanza kuulizana: “Huyu ni mutu gani, hata zoruba na ziwa vinamutii?” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo