Marko 3 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yesu anaponyesha mwenye mukono unaokauka ( Mat 12.9-14 ; Lk 6.6-11 ) 1 Yesu aliingia tena katika nyumba ya kuabudia. Na mule ndani mulikuwa mutu mumoja mwenye mukono unaokauka. 2 Watu waliokuwa mule wakamuchunguza Yesu kusudi waone kama atamuponyesha mutu yule kwa siku ya Sabato, wapate sababu ya kumushitaki. 3 Halafu Yesu akamwambia yule mwenye mukono unaokauka: “Simama hapa katikati.” 4 Kisha akawauliza: “Sheria inaturuhusu kufanya mema au kufanya mabaya kwa siku ya Sabato? Kuponyesha mutu au kumwua?” Lakini wakakaa kimya. 5 Yesu akawakazia macho kwa kasirani, akihuzunika kwa sababu ya ugumu wao. Akamwambia yule mutu: “Nyoosha mukono wako.” Akaunyoosha, nao ukakuwa muzima tena. 6 Pale pale Wafarisayo wakatoka inje na kwenda kukusanyika na watu wa Herode kusudi wafanye mipango ya kumwua Yesu. Makundi mengi ya watu wanamufikia Yesu 7 Yesu na wanafunzi wake wakaenda peke yao pembeni ya ziwa la Galilaya, na kundi kubwa la watu walimufuata. Watu hawa walitoka Galilaya na Yudea, 8 Yerusalema, Idumea, katika inchi za upande mwengine wa muto Yordani na pande za muji wa Tiro na wa Sidona. Kundi hili kubwa la watu walimufikia Yesu kwa sababu walisikia habari za mambo aliyofanya. 9 Na kwa kuona uwingi wa watu wale, Yesu akawaambia wanafunzi wake wamutayarishie chombo kidogo kusudi wasimusonge. 10 Watu waliokuwa na magonjwa walikuwa wakisukumana kusudi wamufikie na kumugusa kwa maana aliwaponyesha watu wengi. 11 Na wakati pepo walipomwona Yesu, wakaanguka mbele yake na kulalamika, wakisema: “Wewe ni Mwana wa Mungu.” 12 Lakini Yesu aliwakaripia kwa nguvu wasimutambulishe yeye ni nani. Yesu anachagua mutime kumi na mwili ( Mat 10.1-4 ; Lk 6.12-16 ) 13 Kisha Yesu akapanda juu ya kilima, akawaita watu aliowataka mwenyewe, nao wakakuja kwake. 14 Akachagua kumi na wawili kati yao, kusudi wakae pamoja naye na apate kuwatuma kwa kuhubiri, 15 na kuwapa uwezo wa kufukuza pepo. 16 Wale kumi na wawili aliowachagua ni hawa: Simoni (Yesu aliyemupa jina la Petro), 17 Yakobo na ndugu yake Yoane, wote wawili walikuwa wana wa Zebedayo (Yesu aliwapa jina la Boanerge, maana yake ngurumo ya radi), 18 Andrea na Filipo, Bartolomayo, Matayo, Toma, Yakobo mwana wa Alfayo, Tadeo, Simoni wa kundi la Wazeloti 19 na Yuda Iskariota, yule aliyemutoa Yesu. Wandugu za Yesu wanaenda kumutwaa 20 Kisha Yesu akarudi kwenye nyumba. Kundi kubwa la watu wakakusanyika tena hata Yesu na wanafunzi wake hawakupata wakati wa kula. 21 Wandugu zake za jamaa waliposikia maneno haya, wakaondoka kwenda kumutwaa, kwa maana walisema kwamba amepotelewa na akili. Yesu anashitakiwa kuwa Belzebuli ( Mat 12.22-32 ; Lk 11.14-23 ; 12.10 ) 22 Walimu wa Sheria waliotoka Yerusalema, wakasema hivi juu ya Yesu: “Amepatwa na Belzebuli.” Na wengine wao wakasema: “Ni huyo mukubwa wa pepo ndiye anayemupa uwezo wa kufukuza pepo.” 23 Basi Yesu akawaita, akawaambia kwa mifano akisema: “Namna gani Shetani anaweza kujifukuza mwenyewe? 24 Watu wa ufalme mumoja wakigombana wao kwa wao, ufalme ule utaanguka. 25 Nao watu wa jamaa moja wakigombana wao kwa wao, jamaa ile haitadumu. 26 Kama Shetani akijigombanisha yeye mwenyewe, na ufalme wake ukigawanyika, uwezo wake hautaendelea, lakini utaanguka. 27 “Mutu hawezi kuingia ndani ya nyumba ya mwenye nguvu na kunyanganya vitu vyake, isipokuwa kwanza anamufunga. Kisha anaweza kunyanganya vitu vyake. 28 “Kweli ninawaambia: watu wataweza kusamehewa zambi zao zote na matusi yao yote. 29 Lakini mutu anayemutukana Roho Mutakatifu hatasamehewa hata milele, kwa maana zambi ile inadumu kwa milele.” 30 Yesu aliwaambia vile kwa sababu walisema kwamba yuko na pepo. Mama na wandugu za Yesu ( Mat 12.46-50 ; Lk 8.19-21 ) 31 Mama ya Yesu na wandugu zake wakakuja, wakasimama inje, wakatuma mutu kwenda kumwita. 32 Kundi kubwa la watu waliikaa, wakizunguka Yesu. Halafu wakamwambia: “Mama yako na wandugu zako wako inje, wanakutafuta.” 33 Yesu akawajibu: “Nani ndiye mama yangu, na nani ndio wandugu zangu?” 34 Kisha akawaangalia watu waliomuzunguka, na kusema: “Mama yangu na wandugu zangu, ni hawa wanaoikaa hapa. 35 Kwa sababu mutu yeyote anayefanya mapenzi ya Mungu, huyu ndiye ndugu yangu, dada yangu na mama yangu.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo