Marko 14 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Wakubwa wanafanya shauri la kukamata Yesu ( Mat 26.1-5 ; Lk 22.1-2 ; Yn 11.45-53 ) 1 Kulikuwa kumebaki siku mbili mbele ya kutimia kwa sikukuu ya Pasaka na ya Mukate Usiyotiwa Chachu. Wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria walitafuta njia ya kumukamata Yesu kwa werevu kusudi wamwue. 2 Kwa maana walijisemesha: “Tusimukamate kwa wakati wa karamu, kusudi fujo isitokee kati ya watu.” Yesu anamimiwa marasi ( Mat 26.6-13 ; Yn 12.1-8 ) 3 Yesu alikuwa Betania katika nyumba ya mutu aliyeitwa Simoni Mukoma. Walipokuwa wakikula, mwanamuke mumoja akaingia ndani ya nyumba. Alikuwa na chupa la jiwe lenye marasi ya bei kali yaliyotengenezwa na maua ya nardo safi. Kisha akavunja mudomo wa lile chupa na kumimia marasi juu ya kichwa cha Yesu. 4 Na wamoja kati ya watu waliokuwa pale wakachukizwa na kitendo kile na kusemezana: “Kwa nini kupoteza mali namna hii? 5 Marasi hii ingeweza kuuzishwa kwa bei ya vikoroti mia tatu vya feza na kugawanyia wamasikini mali ile.” Na wakamukasirikia yule mwanamuke vikali. 6 Lakini Yesu akasema: “Mumwache kimya! Sababu gani munamusumbua? Yeye amenitendea jambo zuri. 7 Kwa maana mutakuwa na wamasikini pamoja nanyi siku zote, na munaweza kuwasaidia wakati wowote munapotaka, lakini mimi sitakuwa pamoja nanyi siku zote. 8 Amefanya sawa alivyoweza. Ameupakaa mwili wangu marasi mbele ya wakati kwa kuutayarisha kwa ajili ya maziko. 9 Kweli ninawaambia: kwa ajili ya kukumbuka mwanamuke huyu, tendo lile alilofanya litaelezwa popote Habari Njema itakapohubiriwa katika dunia nzima.” Yuda anakubali kumutoa Yesu ( Mat 26.14-16 ; Lk 22.3-6 ) 10 Yuda Iskariota, mumoja wa wanafunzi kumi na wawili, akaenda kwa wakubwa wa makuhani, kusudi amutoe Yesu kwao. 11 Waliposikia habari ile wakafurahi sana, nao wakamwahidia kumupa feza. Basi Yuda akaanza kutafuta wakati muzuri kwa kumutoa. Yesu anakula Pasaka pamoja na wanafunzi wake ( Mat 26.17-25 ; Lk 22.7-14 , 21-23 ; Yn 13.21-30 ) 12 Siku ya kwanza ya karamu ya sikukuu ya Mukate Usiyotiwa Chachu, wakati ambapo walichinja kondoo wa Pasaka, wanafunzi wa Yesu wakamwuliza: “Unataka tuende wapi kukutayarishia karamu ya Pasaka?” 13 Basi Yesu akawatuma wawili kati ya wanafunzi wake akiwaambia: “Mwende katika muji, na kule mutakutana mutu mumoja anayebeba mutungi wenye maji. Mumufuate mutu yule, 14 na pahali atakapoingia, mumwambie mwenye nyumba: ‘Mwalimu anauliza kwamba ni wapi kunapokuwa chumba chake ambamo atakulia karamu ya Pasaka pamoja na wanafunzi wake.’ 15 Naye atawaonyesha chumba kikubwa cha gorofi, kilichokwisha kupangwa vizuri na kuwa tayari. Ni mule mutakapotutayarishia karamu.” 16 Halafu wanafunzi wakaondoka, wakaenda katika muji, wakakuta vitu vyote tayari sawa vile Yesu alivyowaambia. Nao wakatayarisha karamu ya Pasaka. 17 Ilipokuwa magaribi, Yesu akafika pamoja na wanafunzi wake kumi na wawili. 18 Walipokuwa wameikaa kula chakula, Yesu akasema: “Kweli ninawaambia: mumoja kati yenu anayekula pamoja nami atanitoa.” 19 Wanafunzi wakaanza kuhuzunika na kumwuliza mumoja kwa mumoja: “Ni mimi?” 20 Yesu akawajibu: “Ni mumoja kati yenu ninyi kumi na wawili, anayechovya mukate pamoja nami ndani ya sahani moja. 21 Kwa maana Mwana wa Mutu atakufa sawa vile Maandiko Matakatifu yanavyosema juu yake, lakini ole kwa yule mutu atakayemutoa! Ingekuwa heri kwake kama asingezaliwa.” Yesu anasimika karamu ya Bwana ( Mat 26.26-30 ; Lk 22.14-20 ; 1 Kor 11.23-25 ) 22 Walipokuwa wakikula, akatwaa mukate, akaubariki, kisha akaumega na kuwapa wanafunzi wake, akisema: “Mutwae, huu ni mwili wangu.” 23 Kisha akatwaa kikombe, akakibariki na kuwapa, nao wote wakakikunywa. 24 Na Yesu akawaambia: “Hii ni damu yangu; damu inayomwangika kwa ajili ya watu wengi kwa kuhakikisha agano la Mungu. 25 Kweli ninawaambia: Tangia sasa sitakunywa tena divai mpaka siku ile nitakapoikunywa kwa upya katika Ufalme wa Mungu.” 26 Na walipokwisha kuimba wimbo, wakaondoka kwenda kwa mulima wa Mizeituni. Yesu anatabiri kwamba Petro atamukana ( Mat 26.31-35 ; Lk 22.31-34 ; Yn 13.36-38 ) 27 Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Ninyi wote mutaanguka, kwa maana imeandikwa katika Maandiko Matakatifu: ‘Nitamwua muchungaji, na kondoo watasambazwa.’ 28 Lakini nitakapokwisha kufufuka, nitawatangulia Galilaya.” 29 Petro akamwambia: “Hata wote wengine wakianguka, mimi sitaanguka.” 30 Yesu akamujibu: “Kweli ninakuambia kwamba usiku huu, mbele jogoo hajawika mara mbili, utakuwa umenikana mara tatu.” 31 Lakini Petro akazidi kusema kwa nguvu: “Hata ikinipasa kufa pamoja nawe, sitakukana hata kidogo.” Na wote wengine wakasema sawasawa naye. Yesu anaomba katika Getesemane ( Mat 26.36-46 ; Lk 22.39-46 ) 32 Wakafika katika bustani inayoitwa Getesemane, na Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Muikae hapa kwa wakati mimi nitakapokuwa nikiomba.” 33 Kisha akatwaa Petro, Yakobo na Yoane na kwenda nao. Akaanza kuwa na hofu na mahangaiko. 34 Akawaambia: “Ninahuzunika sana, karibu kufa! Mubakie hapa na mukeshe.” 35 Kisha akajitenga mbali kidogo nao, akajitupa chini. Akaomba kwamba ikiwezekana, saa ile ya mateso imuondokee mbali. 36 Akasema: “Ee baba! Yote yanawezekana kwako; ninakuomba uniondolee mbali hiki kikombe cha mateso. Lakini isikuwe kama vile mimi ninavyotaka, lakini kama vile wewe unavyotaka.” 37 Aliporudi akawakuta wamelala usingizi. Akamwambia Petro: “Simoni, umelala? Haukuweza kukesha hata kwa saa moja tu? 38 Mukeshe na kuomba, kusudi musianguke katika majaribu; kwa maana roho ni hodari, lakini mwili ni zaifu.” 39 Mara tena akawaacha, akaomba akirudilia maneno yale yale. 40 Aliporudi tena, akawakuta wanafunzi wale wamelala usingizi, kwa maana macho yao yalikuwa yamewezwa sana na usingizi. Nao hawakujua wamujibu nini. 41 Aliporudi kwa mara ya tatu, akawaambia: “Mungali munalala na kupumzika? Inatosha! Saa imetimia. Sasa Mwana wa Mutu anatolewa katika mikono ya wenye zambi. 42 Musimame, tuende! Yule anayenitoa, amefika karibu!” Kukamatwa kwa Yesu ( Mat 26.47-56 ; Lk 22.47-53 ; Yn 18.3-12 ) 43 Yesu alipokuwa hajamaliza kusema, mara moja Yuda, mumoja wa wanafunzi kumi na wawili, akafika pamoja na kundi kubwa la watu wenye panga na magongo. Hawa wote walikuwa wametumwa na wakubwa wa makuhani, walimu wa Sheria, na wasimamizi wa watu. 44 Yuda, yule aliyekuwa amemutoa, alikuwa amekwisha kuwapa kitambulisho hiki: “Yule nitakayemubusu, ndiye yeye. Mumukamate na mumupeleke, mukimulinda vizuri.” 45 Yuda alipofika, mara moja akamujongelea Yesu na kumwambia: “Mwalimu!” Kisha akamubusu. 46 Basi wale watu wakamukamata Yesu na kumufunga. 47 Lakini mumoja kati ya wale waliokuwa pale, akachomoa upanga wake na kumukata mutumishi wa Kuhani Mukubwa sikio. 48 Kisha Yesu akawaambia: “Mumekuja na panga na magongo kwa kunikamata kama watu wanavyokwenda kumukamata munyanganyi? 49 Siku zote nilikuwa pamoja nanyi, nami nilifundisha ndani ya hekalu, nanyi hamukunikamata. Lakini mambo haya yamefanyika kusudi Maandiko Matakatifu yatimizwe.” 50 Wanafunzi wake wote wakamwacha na kukimbia. 51 Lakini kijana mumoja aliyevaa shuka akaendelea kumufuata Yesu. Walijaribu kumukamata, 52 lakini akaachilia shuka ile na kukimbia uchi. Yesu mbele ya Baraza Kubwa ( Mat 26.57-68 ; Lk 22.54-55 , 63-71 ; Yn 18.13-14 , 19-24 ) 53 Wakamupeleka Yesu mbele ya Kuhani Mukubwa, nao wakubwa wote wa makuhani, na wasimamizi wa watu pamoja na walimu wa Sheria wakakusanyika pale. 54 Petro akamufuata Yesu kwa mbali, hata akaingia ndani ya upango wa nyumba ya Kuhani Mukubwa. Pale akaikaa pamoja na walinzi, akiota moto. 55 Wakubwa wa makuhani na wakubwa wote wa Baraza Kubwa walitafuta mashitaki juu ya Yesu kusudi wapate kumwua, lakini hawakupata neno. 56 Watu wengi walimushuhudia uongo, lakini ushuhuda wao haukupatana. 57 Hata wengine wakasimama kwa kutoa ushuhuda huu wa uongo juu yake wakisema: 58 “Sisi tulimusikia akisema: ‘Mimi nitabomoa hekalu hili lililojengwa na watu, na katika siku tatu nitajenga lingine lisilojengwa na watu.’ ” 59 Lakini hata hivi ushuhuda wao haukupatana. 60 Basi Kuhani Mukubwa akasimama katikati ya watu na kumwuliza Yesu: “Haujibu hata neno? Watu hawa wanakushitakia nini?” 61 Lakini Yesu akanyamaza, wala hakujibu neno. Kuhani Mukubwa akamwuliza tena: “Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu mwenye sifa?” 62 Yesu akajibu: “Mimi Ndiye! Nanyi mutamwona Mwana wa Mutu akiikaa na mamlaka kwa kuume kwa Mungu Mwenye Uwezo. Mutamwona vilevile akikuja katika mbingu katikati ya mawingu!” 63 Wakati Kuhani Mukubwa aliposikia maneno haya, akapasua nguo zake, na kusema: “Hatuhitaji tena ushuhuda wowote juu ya mutu huyu. 64 Mumesikia wenyewe jinsi alivyomutukana Mungu. Munawaza nini?” Wote wakamuhukumu kwamba anastahili kufa. 65 Wengine katikati yao wakaanza kumutemea Yesu mate, wakamufunika uso na kumupiga ngumi, wakimwambia: “Tambua sasa ni nani aliyekupiga!” Nao waaskari walinzi wakamukamata Yesu na kumupiga makofi. Petro anamukana Yesu ( Mat 26.69-75 ; Lk 22.56-62 ; Yn 18.15-18 , 25-27 ) 66 Petro alipokuwa angali chini ndani ya upango, mumoja wa watumishi wanawake wa Kuhani Mukubwa akafika pale. 67 Alipomwona Petro akiota moto, akamwangalia, na kumwambia: “Wewe vilevile ulikuwa pamoja na Yesu wa Nazareti.” 68 Lakini Petro akakana, akisema: “Sijui wala sifahamu maneno unayotaka kusema.” Kisha akatoka inje ya upango na kwenda kwenye kiingilio cha mulango. [Jogoo akawika.] 69 Yule mutumishi mwanamuke akamwona pale, akaanza tena kuwaambia wale waliokuwa pale: “Huyu mutu ni mumoja wao!” 70 Lakini Petro akakana tena. Nyuma kidogo, watu wale wakamwambia Petro tena: “Hakika wewe ni mumoja wao, kwa sababu wewe vilevile ni wa Galilaya.” 71 Basi Petro akaanza kusema: “Nilaaniwe ikiwa ninasema uongo! Ninaapa kwamba simujui mutu huyu munayemutaja.” 72 Mara moja jogoo akawika kwa mara ya pili, na Petro akakumbuka maneno yale Yesu aliyomwambia kwamba mbele jogoo hajawika mara mbili, atakuwa amemukana mara tatu. Basi akaanza kulia. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo