Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Luka 5 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Yesu anaita wanafunzi wa kwanza
( Mat 4.18-22 ; Mk 1.16-20 )

1 Siku moja, Yesu alisimama pembeni ya ziwa la Genezareti na watu wengi walimusongasonga kusudi wasikie neno la Mungu.

2 Akaona vyombo viwili vyenye kuezeka pembeni ya ziwa, na wavuvi walikuwa wametoka ndani yao, na walikuwa wakisafisha nyavu zao.

3 Yesu akaingia ndani ya moja kati ya vile vyombo, nacho kilikuwa cha Simoni. Yesu akamwomba akisukume mbali kidogo na kivuko. Halafu akaikaa mule na kuwafundisha watu.

4 Alipokwisha kufundisha, akamwambia Simoni: “Uendeshe chombo mpaka kwenye maji mengi na mushushe nyavu zenu, muvue samaki.”

5 Simoni akajibu: “Mwalimu, tumetumika usiku kucha bila kupata kitu. Lakini kwa sababu umeniambia, nitashusha nyavu.”

6 Na waliposhusha nyavu, wakanasa samaki wengi sana hata nyavu zao zikaanza kupasuka.

7 Halafu wakawafanyia wale wenzao waliokuwa ndani ya chombo kingine alama kwa mikono, kusudi wakuje kuwasaidia. Wakakuja, wakajaza vyombo vyote viwili na samaki wengi, hata vyombo vikaanza kuzama.

8 Simoni Petro alipoona mambo hayo, akapiga magoti mbele ya Yesu na kusema: “Bwana, utoke karibu nami, kwa sababu mimi ni mutu mwenye zambi!”

9 Simoni na wote waliokuwa pamoja naye walishangaa sana kwa sababu ya wingi wa samaki waliowapata.

10 Yakobo na Yoane wana wa Zebedayo waliokuwa wavuvi wenzake na Simoni, walishangaa vilevile. Na Yesu akamwambia Simoni: “Usiogope; tangia sasa utafanya kazi ya kuopoa watu.”

11 Basi wakakokota vyombo vyao mpaka inchi kavu, wakaacha vyote na kumufuata.


Yesu anatakasa mwenye ukoma
( Mat 8.1-4 ; Mk 1.40-45 )

12 Yesu alipokuwa katika muji mumoja kati ya miji ile, kukatokea mutu aliyejaa na ukoma mwili wote. Naye alipomwona Yesu, akainama uso mpaka chini, akamusihi akisema: “Bwana, kama ukitaka, unaweza kunitakasa.”

13 Yesu akanyoosha mukono, akamugusa na kumwambia: “Ninataka, utakaswe!” Na mara moja mutu yule akapona ukoma.

14 Yesu akamwamuru hivi: “Usimwambie mutu neno juu ya hii. Lakini kwenda na kumwonyesha kuhani jinsi unavyokuwa sasa. Kisha utoe sadaka kama Musa alivyoamuru, kuwa ushuhuda kwa watu wote kwamba umetakaswa.”

15 Hata hivi habari juu ya Yesu zikazidi kuvuma na makundi mengi ya watu wakakusanyika kwa kumusikiliza na kuponyeshwa magonjwa yao.

16 Lakini alikuwa akienda mbali nao kwenye ukiwa na kuomba kule.


Yesu anaponyesha mutu mwenye kupooza
( Mat 9.1-8 ; Mk 2.1-12 )

17 Siku moja Yesu alipokuwa akifundisha, Wafarisayo na walimu wakubwa wa Sheria waliotoka katika kila kijiji cha jimbo la Galilaya na la Yudea na toka Yerusalema, walikuwa wakiikaa pale. Naye alikuwa akiponyesha wagonjwa kwa uwezo wa Bwana.

18 Watu wamoja wakakuja wakimubeba mutu aliyepooza juu ya kipoyi. Wakatafuta njia ya kumwingiza ndani ya nyumba kusudi wamuweke mbele ya Yesu.

19 Lakini kwa kuona walikosa njia ya kumwingiza ndani, kwa sababu ya wingi wa watu, wakapanda juu ya paa, wakaondosha matebura na kumushusha yule mugonjwa katikati ya watu, akiwa juu ya kipoyi chake, hata wakamufikisha mbele ya Yesu.

20 Yesu alipoona namna walivyomwaminia, akasema: “Rafiki yangu, zambi zako zimesamehewa.”

21 Walimu wa Sheria na Wafarisayo wakaanza kujiuliza: “Ni mutu gani huyu anayemutukana Mungu? Ni nani anayeweza kusamehe zambi, isipokuwa Mungu peke yake?”

22 Halafu Yesu akitambua mafikiri yao, akawauliza: “Sababu gani munajiuliza mambo hayo yote?

23 Kitu gani kinachokuwa chepesi, kusema: ‘Zambi zako zimesamehewa,’ au kusema: ‘Simama, utembee?’

24 Basi, ninataka mujue kwamba Mwana wa Mutu yuko na mamlaka ya kusamehe zambi hapa katika dunia.” Kwa hiyo akamwambia yule mutu aliyepooza: “Ninakuamuru, simama, utwae kipoyi chako na urudie kwako.”

25 Pale pale mutu yule akasimama mbele yao wote, akatwaa kipoyi alichokilalia, akaenda kwake akimusifu Mungu.

26 Wote wakashangaa na kushikwa na woga, wakamutukuza Mungu wakisema: “Leo tumeona mambo ya ajabu.”


Yesu anamwita Lawi
( Mat 9.9-13 ; Mk 2.13-17 )

27 Nyuma ya mambo hayo, Yesu alipoondoka akamwona mulipishaji mumoja wa kodi anayeitwa Lawi, akiikaa katika nyumba ya kulipishia kodi. Yesu akamwambia: “Unifuate!”

28 Lawi akasimama, akaacha vyote na kumufuata.

29 Kisha Lawi akamufanyia Yesu karamu kubwa katika nyumba yake. Walipishaji wengi wa kodi na watu wengine walikuwa wakikula pamoja nao.

30 Wafarisayo na walimu wa Sheria wa kikundi chao wakawanungunikia wanafunzi wake, wakisema: “Kwa sababu gani munakula na kunywa pamoja na walipishaji wa kodi na watenda mabaya?”

31 Yesu akawajibu: “Wenye afya nzuri hawahitaji muganga, lakini wale wanaokuwa wagonjwa.

32 Sikukuja kuwaita wenye haki, lakini wenye zambi kusudi wageuke toka zambi zao.”


Ulizo juu kufunga kula chakula
( Mat 9.14-17 ; Mk 2.18-22 )

33 Watu wamoja wakamwambia Yesu: “Wanafunzi wa Yoane na wale wa Wafarisayo wanafunga mara nyingi na kuomba, lakini wanafunzi wako wanaendelea kula na kunywa.”

34 Yesu akawajibu: “Munafikiri kwamba munaweza kuwazuiza warafiki za bwana-arusi kula chakula cha karamu wakati bwana arusi akingali pamoja nao? Hapana!

35 Lakini kutakuwa siku bwana-arusi atakapoondoshwa kati yao. Katika siku zile ndipo watafunga kula.”

36 Yesu akawaambia mufano huu vilevile: “Hakuna mutu anayekata kiraka kwenye nguo mupya na kukishonea juu ya nguo ya zamani. Kama anafanya vile, atakuwa amepasua ile nguo mupya na kile kiraka cha nguo mupya hakitashikamana na nguo ya zamani.

37 Vilevile hakuna mutu anayetia divai mupya ndani ya machupa ya ngozi yenye kuzeeka. Kama akifanya vile, ile divai mupya itapasua yale machupa; divai itamwangika na machupa yatapotea bure.

38 Lakini inafaa kutia divai mupya ndani ya machupa mapya ya ngozi.

39 Hakuna mutu aliyekwisha kunywa divai ya zamani atakayetaka tena divai mupya. Kwa maana anasema kwamba ile ya zamani ni nzuri zaidi.”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ