Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Luka 24 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Ufufuko wa Yesu
( Mat 28.1-10 ; Mk 16.1-8 ; Yn 20.1-10 )

1 Siku ya kwanza ya juma, asubui mapema, wale wanawake wakaenda kwenye kaburi, nao walibeba yale mafuta waliyotengeneza.

2 Walipofika, wakakuta jiwe kubwa limekwisha kusukumwa pembeni ya kiingilio cha kaburi.

3 Lakini walipoingia ndani ya kaburi hawakuona maiti ya Bwana Yesu.

4 Walipokuwa wakifazaika kwa ajili ya jambo hili, mara moja watu wawili waliovaa nguo zenye kungaa wakawatokea.

5 Kwa sababu ya woga, wale wanawake wakainama uso mpaka chini. Lakini wale watu wakawaambia: “Kwa sababu gani munamutafuta yule anayekuwa muzima kati ya waliokufa?

6 Yeye hayuko hapa; amefufuka! Mukumbuke jinsi alivyowaambia wakati alipokuwa angali Galilaya.

7 Aliwaambia kwamba Mwana wa Mutu anapaswa kutolewa katika mikono ya wenye zambi, na kutundikwa juu ya musalaba, lakini kwa siku ya tatu kisha kufa, atafufuka.”

8 Halafu wakakumbuka maneno yale Yesu aliyosema.

9 Waliporudia toka kwenye kaburi, wakapasha habari ile kwa wanafunzi kumi na mumoja na kwa wafuasi wengine wote wa Yesu.

10 Na hawa ndio waliowapasha habari ile kwa mitume: Maria wa Magdala, Yoana na Maria mama ya Yakobo. Kulikuwa vilevile wanawake wengine pamoja nao.

11 Lakini mitume hawakusadiki maneno ya wale wanawake, waliwaza kwamba ni ya bure.

12 Lakini Petro alisimama, akaenda mbio mpaka kwenye kaburi. Alipoinama kuchungulia ndani yake, akaona tu vile vitambaa. Kisha akarudia kwake, akishangaa kwa ajili ya mambo yaliyotokea.


Katika njia ya Emau
( Mk 16.12-13 )

13 Siku ile ile, wawili kati ya wanafunzi walikuwa wakienda kwenye kijiji cha Emau, kilichokuwa kwa umbali wa kilometre kumi na moja kutoka Yerusalema.

14 Walikuwa wakiongea juu ya mambo yote yaliyotokea.

15 Walipokuwa wakiongea na kuulizana, Yesu mwenyewe akafika karibu nao, akaendelea kutembea pamoja nao,

16 lakini macho yao yalizuizwa kumutambua.

17 Yesu akawauliza: “Ni maneno gani haya munayosumulia hapa katika njia.” Nao wakasimama, wakiwa wanahuzunika.

18 Na mumoja wao, aliyeitwa Kleopa, akamujibu: “Kati ya wageni wanaokaa Yerusalema ni wewe tu usiyejua mambo yaliyotokea kule katika siku hizi?”

19 Naye akawauliza: “Ni mambo gani?” Nao wakamujibu: “Haujui mambo yaliyomupata Yesu wa Nazareti? Yeye alishuhudiwa na Mungu na watu wote kwamba alikuwa nabii mwenye uwezo katika mambo aliyofanya na kusema.

20 Wakubwa wa makuhani na wasimamizi wetu walimutoa kusudi ahukumiwe kufa, nao wamemutundika juu ya musalaba.

21 Sisi tulikuwa na tumaini kwamba yeye ndiye atakayekomboa Waisraeli. Lakini sasa, leo ni siku ya tatu tangu mambo hayo yalipofanyika.

22 Zaidi ya hiyo wanawake wamoja wa kundi letu walitushitusha. Walienda kwenye kaburi asubui mapema,

23 lakini hawakuona maiti yake. Basi wakarudia kutuelezea kwamba wamalaika waliwatokea na kuwaambia kwamba yeye ni muzima.

24 Halafu wamoja kati yetu walienda kwenye kaburi, nao wakakuta mambo yote ni sawa na vile wale wanawake walivyosema, lakini hawakumwona.”

25 Basi Yesu akawaambia: “Enyi wajinga na wenye mioyo mizito kwa kuamini maneno yote manabii waliyosema!

26 Haikumupasa Kristo ateswe kama vile na aingie kwenye nafasi atakapotukuzwa?”

27 Kisha akawaelezea maneno yaliyoandikwa juu yake katika Maandiko Matakatifu yote, akianza toka vitabu vya Musa na kuendelea katika vitabu vya manabii wote.

28 Nao walipofika karibu na kile kijiji ambamo walikuwa wakienda, Yesu akaendelea mbele, akiwa sawa mwenye kuwaacha.

29 Lakini wakamusihi sana abakie pamoja nao, kwa maana ilikuwa magaribi na giza lilitaka kuingia. Basi akaingia ndani ya nyumba kubakia pamoja nao.

30 Alipokuwa akiikaa kula chakula pamoja nao, akatwaa mukate na kuubariki. Kisha akaumega na kuwapatia.

31 Halafu, macho yao yakafumbuliwa, wakamutambua. Lakini yeye akatoweka, nao hawakumwona tena.

32 Basi wakasemezana: “Mioyo yetu ilichangamuka sana wakati alipokuwa akisimulia nasi katika njia na kutuelezea Maandiko Matakatifu.”

33 Wakaondoka saa ile ile, na kurudia Yerusalema. Kule wakakuta wale mitume kumi na mumoja wamekusanyika pamoja na watu wengine wa kundi lao.

34 Hao waliokusanyika wakawaambia: “Hakika Bwana amefufuka, na amemutokea Simoni!”

35 Nao vilevile wakawaelezea mambo yote yaliyotokea katika njia na namna walivyomutambua Yesu wakati alipomega mukate.


Yesu anawatokea wanafunzi wake
( Mat 28.16-20 ; Mk 16.14-18 ; Yn 20.19-23 ; Mdo 1.6-8 )

36 Walipokuwa hawajamaliza kuwaelezea mambo hayo, mara moja Yesu mwenyewe akasimama katikati yao, na kuwaambia: “Amani kwenu!”

37 Wakashituka na kuogopa, wakizani kwamba wameona muzimu.

38 Lakini Yesu akawaambia: “Kwa sababu gani munafazaika na kuwa na mashaka?

39 Muangalie mikono yangu na miguu yangu, kusudi mupate kutambua kwamba ni mimi. Muniguse, muone, kwa maana muzimu hana mwili wala mifupa kama hivi munavyoniona kuwa navyo.”

40 Alipokwisha kusema vile, akawaonyesha mikono na miguu yake.

41 Nao walipokuwa hawajasadiki bado kwa sababu ya furaha na mushangao, akawauliza: “Muko na chakula chochote hapa?”

42 Wakamupa kipande cha samaki iliyochomwa.

43 Akakitwaa na kukikula mbele yao.

44 Kisha akawaambia: “Haya ndiyo maneno niliyowaambia wakati nilipokuwa ningali pamoja nanyi, kwamba sherti yatimizwe maneno yote yaliyoandikwa juu yangu katika Sheria ya Musa, katika maandiko ya manabii na katika Zaburi.”

45 Halafu akawafungua akili kusudi wapate kufahamu Maandiko Matakatifu

46 akiwaambia: “Imeandikwa katika Maandiko Matakatifu kwamba Kristo atateswa na kufufuka kwa siku ya tatu kisha kufa kwake.

47 Iliandikwa vilevile kwamba kwa jina lake watahubiri mataifa yote, kuanzia Yerusalema, kusudi wageuke toka katika zambi na wapate kusamehewa.

48 Na ninyi ndio mutakaotoa ushuhuda juu ya maneno haya.

49 Na mimi mwenyewe nitawatumia zawadi ile Baba yangu aliyoahidi ishuke juu yenu. Lakini mungojee kule Yerusalema mpaka mutakapojazwa uwezo kutoka juu.”


Yesu ananyanyuliwa mbinguni
( Mk 16.19-20 ; Mdo 1.9-11 )

50 Kisha Yesu akatoka nao katika muji na kwenda karibu na kijiji cha Betania na pale akainua mikono yake juu na kuwabariki.

51 Alipokuwa akiwabariki akajitenga nao na kunyanyuliwa mbinguni.

52 Nao walipokwisha kumwabudu, wakarudia Yerusalema wakifurahi sana.

53 Na siku zote walikuwa ndani ya hekalu wakimusifu Mungu.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ