Luka 22 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Shauri la kumwua Yesu ( Mat 26.1-5 ; Mk 14.1-2 ; Yn 11.45-53 ) 1 Sikukuu ya Mukate Usiotiwa Chachu, inayoitwa Pasaka, ilikaribia. 2 Wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria walitafuta njia ya kumwua Yesu, lakini waliogopa watu. Yuda anakubali kumutoa Yesu ( Mat 26.14-16 ; Mk 14.10-11 ) 3 Basi Shetani akamwingia Yuda, yule anayeitwa Iskariota, aliyekuwa mumoja wa wanafunzi kumi na wawili. 4 Halafu Yuda akaenda kusikilizana na wakubwa wa makuhani na wakubwa wa walinzi wa hekalu juu ya namna ya kumutoa Yesu kwao. 5 Wakafurahi sana, wakapatana kumupa feza. 6 Yuda akakubali na kuanza kutafuta wakati unaokuwa muzuri kwa kumutoa Yesu kwao, kwa uficho pasipo watu kujua. Yesu anakula Pasaka na wanafunzi wake ( Mat 26.17-25 ; Mk 14.12-21 ; Yn 13.21-30 ) 7 Siku ya karamu ya Mukate Usiotiwa Chachu, ndiyo siku ile walipaswa kuchinja kondoo waliotayarishwa kwa ajili ya Pasaka ikatimia. 8 Yesu akawatuma Petro na Yoane, akisema: “Mwende mututayarishie chakula cha karamu ya Pasaka.” 9 Wakamwuliza: “Ni wapi unapotaka tuende tukitayarishie?” 10 Akawajibu: “Mutakapoingia katika muji, mutakutana mutu mumoja anayebeba mutungi wenye maji. Mumufuate mutu yule katika nyumba atakamoingia, 11 mumwambie mwenye nyumba: ‘Mwalimu anakuuliza kwamba ni wapi kunapokuwa chumba cha kukulia karamu ya Pasaka pamoja na wanafunzi wake.’ 12 Naye atawaonyesha chumba kikubwa cha gorofi kilichokwisha kupangwa vizuri. Ni mule mutakapotayarishia karamu.” 13 Wakaenda na kukuta vitu vyote sawa vile Yesu alivyowaambia. Nao wakatayarisha karamu ya Pasaka. Karamu ya Bwana ( Mat 26.26-30 ; Mk 14.22-26 ; 1 Kor 11.23-25 ) 14 Saa ilipotimia, Yesu akaikaa kula chakula pamoja na wanafunzi wake. 15 Akawaambia: “Nimetamani sana kula karamu hii ya Pasaka pamoja nanyi mbele ya kuteswa kwangu! 16 Kwa maana ninawaambia, sitakula tena karamu hii ya Pasaka mpaka siku ile nitakapokula ile yenye kukamilika katika Ufalme wa Mungu.” 17 Kisha Yesu akatwaa kikombe, akakibariki na kusema: “Mutwae kikombe hiki na mukigawanye kati yenu. 18 Kwa maana ninawaambia kwamba tangia sasa sitakunywa tena divai mpaka Ufalme wa Mungu utakapokuja.” 19 Halafu akatwaa mukate, akaubariki, kisha akaumega na kuwapa akisema: “Huu ni mwili wangu [unaotolewa kwa ajili yenu. Mufanye hivi kwa kunikumbuka.” 20 Vilevile kisha kula akatwaa kikombe na kuwapa akisema: “Kikombe hiki ni agano jipya la Mungu, linalohakikishwa kwa njia ya damu yangu.] 21 “Lakini muangalie: yule anayenitoa anachangia chakula pamoja nami. 22 Kwa maana Mwana wa Mutu atakufa sawa vile ilivyokusudiwa na Mungu; lakini ole kwa mutu yule atakayemutoa!” 23 Basi wakaanza kuulizana wao kwa wao ni nani kati yao atakayefanya jambo lile. Ni nani anayekuwa mukubwa katika Ufalme wa Mungu 24 Kulitokea ubishi kati ya wanafunzi wa kujua nani anayekuwa mukubwa kati yao. 25 Yesu akawaambia: “Wafalme wa mataifa wanawatawala watu wao kwa nguvu; na wale wenye mamlaka juu yao wanajiita ‘Watenda mema.’ 26 Lakini isikuwe hivi katikati yenu. Lakini yule anayekuwa mukubwa kati yenu sherti akuwe mudogo zaidi, na yule anayekuwa mwongozi sherti akuwe kama mutumishi. 27 Kwa maana, ni nani anayekuwa mukubwa; yule anayeikaa kwa kula chakula au yule anayemushugulikia? Hakika ni yule anayeikaa kwa kula chakula. Ingawa vile mimi niko hapa katikati yenu kama mwenye kushugulika! 28 “Ninyi ndio muliokuwa pamoja nami katika majaribu yangu. 29 Nami ninawawekea ninyi ufalme kama vile Baba yangu alivyoniwekea mimi, 30 kusudi mupate kula na kunywa pamoja nami katika ufalme wangu. Mutaikaa vilevile juu ya viti vya kifalme, kwa kuhukumu makabila kumi na mawili ya Waisraeli.” Yesu anajulisha ya kama Petro atamukana ( Mat 26.31-35 ; Mk 14.27-31 ; Yn 13.36-38 ) 31 “Simoni, Simoni! Sikiliza: Shetani ameachiliwa wakati wa kuwajaribu na kuwatenga kabisa. 32 Lakini mimi nimekuombea, kusudi usipungukiwe na imani. Nawe utakaponirudilia tena, uwatie wandugu zako moyo.” 33 Petro akamwambia: “Bwana, mimi niko tayari kufungwa pamoja nawe na hata kufa pamoja nawe.” 34 Yesu akamujibu: “Ninakuambia wewe Petro kwamba leo, mbele jogoo hajawika utakuwa umenikana mara tatu kuwa haunijui.” Feza, mufuko na upanga 35 Halafu Yesu akawauliza wanafunzi wake: “Nilipowatuma pasipo kubeba feza, wala mufuko, wala viatu, mulikosewa na kitu gani?” Wakamujibu: “Hakuna.” 36 Naye akawaambia: “Lakini sasa, yule anayekuwa na feza azitwae, na anayekuwa na mufuko autwae vilevile. Na yeyote asiyekuwa na upanga, auzishe nguo yake apate kuununua. 37 Kwa maana ninawaambia, ni lazima yatimie kwangu maneno haya yaliyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: ‘Naye alihesabiwa pamoja na watenda maovu.’ Kwa sababu yanayonielekea mimi yanafikia kwa mwisho wake.” 38 Wanafunzi wakasema: “Bwana, angalia, tuna panga mbili hapa.” Akajibu: “Basi, inatosha.” Yesu anaomba katika Getesemane ( Mat 26.36-46 ; Mk 14.32-42 ) 39 Yesu akatoka na kwenda kwa mulima wa Mizeituni kama ilivyokuwa desturi yake. Na wanafunzi wake wakamufuata. 40 Alipofika kwenye nafasi ile, akawaambia: “Muombe kusudi musianguke katika majaribu.” 41 Kisha akajitenga nao na kuenda kwenye hatua ya mutu kuweza kutupa jiwe, akapiga magoti, akaomba akisema: 42 “Baba, kama ukitaka, ninakuomba uniondolee mbali kikombe cha mateso. Lakini isikuwe mapenzi yangu ndiyo yafanyike, lakini yako.” [ 43 Halafu malaika toka mbinguni alimutokea kwa kumutia moyo. 44 Yesu alikuwa katika uchungu mukubwa, akazidi kuomba kwa bidii. Jasho iliyomutoka ikakuwa kama matone ya damu yaliyokuwa yakitiririka mpaka chini.] 45 Kisha kuomba, alirudia pahali alipoacha wanafunzi wake, akawakuta wamelala kwa sababu walikuwa na huzuni. 46 Akawaambia: “Sasa, ninyi munalala? Muamuke na muombe, kusudi musianguke katika majaribu.” Kukamatwa kwa Yesu ( Mat 26.47-56 ; Mk 14.43-50 ; Yn 18.3-11 ) 47 Yesu alipokuwa hajamaliza kusema, kundi la watu wakafika, wakiongozwa na Yuda, mumoja wa wanafunzi kumi na wawili. Akamujongelea Yesu kusudi amubusu. 48 Lakini Yesu akamwuliza: “Yuda, unamutoa Mwana wa Mutu kwa kumubusu?” 49 Wale wanafunzi wa Yesu walipoona mambo yatakayotendeka, wakamwuliza: “Bwana, tuwakate kwa panga?” 50 Na mumoja wao akamupiga mutumishi wa Kuhani Mukubwa upanga na kumukata sikio la kuume. 51 Lakini Yesu akasema: “Mwache, inatosha!” Akagusa sikio la mutu yule, na kumuponyesha. 52 Halafu Yesu akawaambia wakubwa wa makuhani, wakubwa wa walinzi wa hekalu na wazee waliokuja kumukamata: “Mumekuja na panga na magongo kama vile wanavyokwenda kukamata munyanganyi? 53 Siku zote nilipokuwa pamoja nanyi katika hekalu, ninyi hamukunikamata. Lakini hii ni saa yenu; saa ya utawala wa bwana wa giza.” Petro anamukana Yesu ( Mat 26.57-58 , 69-75 ; Mk 14.53-54 , 66-72 ; Yn 18.12-18 , 25-27 ) 54 Walipokwisha kumukamata, wakamupeleka katika nyumba ya Kuhani Mukubwa. Petro akamufuata Yesu kwa mbali. 55 Wakakonga moto katikati ya kiwanja na kuikaa, na Petro akakuja kuota moto pamoja nao. 56 Mutumishi mumoja mwanamuke alipomwona Petro akiikaa karibu na moto, akamukazia macho na kusema: “Mutu huyu vilevile alikuwa pamoja naye.” 57 Lakini Petro akakana, akisema: “Ewe mama, mimi simujui!” 58 Nyuma kidogo mutu mwingine akamwona, na akasema: “Wewe vilevile ni mumoja wao!” Lakini Petro akamujibu mutu yule: “Mimi si mumoja wao.” 59 Kisha muda wa karibu saa moja, mutu mwingine akatia mukazo akisema: “Hakika, mutu huyu alikuwa pamoja naye, kwa sababu yeye ni wa Galilaya.” 60 Lakini Petro akasema: “Sijui mambo unayoyasema.” Wakati ule alipokuwa angali akisema, jogoo akawika. 61 Bwana akageuka na kumwangalia Petro. Petro akakumbuka maneno yale Bwana aliyomwambia kwamba mbele jogoo hajawika atakuwa amemukana mara tatu. 62 Basi akatoka inje, akalia kwa uchungu sana. Yesu anachekelewa ( Mat 26.67-68 ; Mk 14.65 ) 63 Wale watu waliokuwa wakimuchunga Yesu walimuchekelea na kumupiga. 64 Walimufunika uso kwa kitambaa na kumwuliza: “Tambua sasa, ni nani aliyekupiga?” 65 Nao walimutusi kwa maneno mengine mengi. Yesu mbele ya Baraza Kubwa ( Mat 26.59-66 ; Mk 14.55-64 ; Yn 18.19-24 ) 66 Usiku ulipokucha, wazee wa Wayuda, wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria, wakakusanyika. Wakamuleta Yesu mbele ya Baraza yao Kubwa, 67 na kumwuliza: “Kama wewe ni Kristo, utuambie.” Akawajibu: “Kama ninawaambia, hamutanisadiki, 68 na kama ninawauliza ulizo, hamutanijibu. 69 Lakini zaidi ya hiyo Mwana wa Mutu ataikaa na mamlaka karibu na Mungu Mwenye Uwezo.” 70 Wote wakamwuliza: “Basi, wewe ni Mwana wa Mungu?” Yesu akawajibu: “Ninyi munasema kwamba mimi ndiye.” 71 Halafu wakasema: “Hatuhitaji tena ushuhuda wowote juu yake. Kwa maana tunatoka kusikia maneno aliyosema!” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo