Luka 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kuzaliwa kwa Yesu ( Mat 1.18-25 ) 1 Katika siku zile, Augusto, mufalme wa Roma akatoa amri kwamba wafanye hesabu ya watu wa utawala wake wote. 2 Hesabu hii ya kwanza ilifanyika katika siku Kurenio alipokuwa liwali wa jimbo la Suria. 3 Watu wote walienda kujiandikisha, kila mumoja katika muji wake wa kuzaliwa. 4 Basi Yosefu naye vilevile akaondoka katika muji Nazareti, wa jimbo la Galilaya, na kwenda Yudea katika muji wa kuzaliwa wa mufalme Daudi, unaoitwa Betelehemu. Alienda kule kwa sababu alikuwa mutu wa ukoo wa Daudi. 5 Alienda kujiandikisha kule pamoja na muchumba wake Maria ambaye alikuwa mimba. 6 Walipokuwa kule Betelehemu, wakati wake wa kuzaa ukatimia. 7 Akazaa mwana, ndiye muzaliwa wake wa kwanza. Akamufunika nguo za kitoto na kumulalisha katika sanduku ya kukulishia nyama, kwa sababu walikosa nafasi ya kukaa katika nyumba ya kupangisha wageni. Malaika anawatokea wachungaji 8 Na katika pande zile, kulikuwa wachungaji kule katika mbuga wakichunga kondoo zao usiku. 9 Na kwa rafla malaika wa Bwana akawatokea, na mwangaza wa utukufu wa Bwana ukawazunguka. Nao wakaogopa sana. 10 Lakini malaika akawaambia: “Musiogope, kwa sababu ninawaletea Habari Njema itakayofurahisha sana watu wote. 11 Leo hii Mwokozi amezaliwa kwa ajili yenu katika muji wa Daudi, yeye ndiye Kristo na Bwana. 12 Na hiki ndicho kitambulisho kwenu: mutamukuta mutoto muchanga amefunikwa nguo za kitoto, naye amelalishwa katika sanduku ya kukulishia nyama.” 13 Mara moja kukaonekana kundi kubwa la wamalaika kutoka mbinguni wakiwa pamoja na yule malaika, wakimutukuza Mungu na kusema: 14 “Sifa kwa Mungu juu mbinguni, na amani katika dunia kwa watu anaowapenda.” Wachungaji wanakwenda Betelehemu 15 Wale wamalaika walipoondoka na kurudia mbinguni, wachungaji wakasemezana: “Basi tuende Betelehemu, kusudi tupate kuona jambo lile lililotokea, ambalo Bwana alitujulisha.” 16 Halafu wakaenda kwa haraka, wakawakuta Maria, Yosefu na mutoto amelalishwa katika sanduku ya kukulishia nyama. 17 Nao walipokwisha kumwona mutoto huyo muchanga, wakaeleza maneno waliyoambiwa na malaika juu yake. 18 Na wote waliosikia habari ile waliyoieleza wakashangaa. 19 Lakini Maria akachunga mambo hayo yote ndani ya moyo na kuyafikiri sana. 20 Kisha wachungaji wakarudia wakitukuza Mungu na kumusifu kwa ajili ya mambo yote waliyoyasikia na kuyaona, kwa maana yote yalifanyika sawa vile malaika alivyokuwa amewaambia. Mutoto anapewa jina 21 Ilipotimia siku ya kumutahiri mutoto, ndiyo siku ya nane tangu alipozaliwa, wakamupa jina lake Yesu. Jina hili ni lile malaika alilojulisha mbele mama yake hajabeba mimba. Yesu anaonyeshwa katika hekalu 22 Siku zilipotimia za Maria na Yosefu kutakaswa kama vile Sheria ya Musa inavyoagiza, wakamupeleka mutoto Yerusalema, kusudi wapate kumutolea kwa Bwana. 23 Imeandikwa katika Sheria ya Bwana: “Kila muzaliwa wa kwanza wa kiume atatolewa kwa Bwana.” 24 Wakatoa vilevile sadaka sawa vile inavyoagizwa katika Sheria ile: “Hua wawili au vitoto viwili vya njiwa.” 25 Wakati ule katika Yerusalema kulikuwa mutu mumoja aliyeitwa Simeoni. Mutu huyo alikuwa mwenye haki na mwenye kuogopa Mungu. Alikuwa akitazamia kwa hamu ukombozi wa taifa la Israeli. Roho Mutakatifu alikuwa pamoja naye; 26 alikuwa amemufunulia kwamba hatakufa mbele hajamwona Kristo wa Bwana. 27 Na ilimutokea Simeoni kuingia ndani ya hekalu, akiongozwa na Roho. Wazazi walipomuleta mutoto wao Yesu kusudi wamutendee sawa ilivyoagizwa na Sheria, 28 Simeoni akamupokea katika mikono, akamushukuru Mungu, akisema: 29 “Sasa, Ee Bwana, umuruhusu mutumishi wako akufe katika amani, maana umetimiza ahadi yako. 30 Nimejionea mwenyewe wokovu unaotoka kwako, 31 ulioutayarisha mbele ya watu wote. 32 Ndio utakaowaangazia mataifa, na kuleta utukufu kwa watu wako Waisraeli.” 33 Wazazi wa Yesu wakashangaa kusikia maneno yale Simeoni aliyosema juu ya mutoto. 34 Simeoni akawabariki na kumwambia Maria, mama yake: “Mutoto huyu amezaliwa kwa sababu ya kuwaangusha na kuwasimamisha watu wengi katika Israeli. Naye atakuwa kitambulisho kutoka kwa Mungu watu watakachokipinga, 35 kusudi mawazo ya wengi yanayofichwa yapate kufunuliwa wazi. Na kwa ngambo yako wewe, uchungu utakuchoma moyo kama upanga.” Nabii muke Ana 36 Kulikuwa vilevile nabii mumoja mwanamuke, aliyeitwa Ana, aliyekuwa binti ya Fanueli, wa kabila la Aseri. Yeye alikuwa muzee sana. Aliishi miaka saba na mume wake tangu alipoolewa. 37 Kisha akabaki mujane, hata akaeneza umri wa miaka makumi nane na mine. Alibaki katika hekalu, akitumikia Mungu usiku na muchana, akifunga kula chakula na kuomba. 38 Basi, akafika saa ile ile, akaanza kumushukuru Mungu. Naye akaeleza habari za mutoto huyo kwa watu wote waliokuwa wakingojea jinsi Mungu atakavyokomboa Yerusalema. Wazazi wa Yesu wanarudia Nazareti 39 Wakati wazazi wa Yesu walipokwisha kutimiza kanuni zote zilizoagizwa na Sheria ya Bwana, wakarudia pamoja naye Galilaya, katika muji wao wa Nazareti. 40 Mutoto yule akakomaa, akazidi kuwa na nguvu, akajaa hekima, na neema ya Mungu ilikuwa pamoja naye. Yesu katika hekalu 41 Kila mwaka wazazi wa Yesu walikwenda Yerusalema kuhuzuria sikukuu ya Pasaka. 42 Yesu alipokuwa na umri wa miaka kumi na miwili, akaenda pamoja nao kule kwa sikukuu ile kama ilivyokuwa desturi. 43 Siku za karamu zilipopita, wakarudia kwao, lakini mutoto Yesu akabaki Yerusalema bila wazazi wake kujua. 44 Walizania kama alikuwa pamoja na wenzake aliosafiri nao. Kisha kutembea mwendo wa siku nzima, wakaanza kumutafuta katikati ya wandugu zao na ya watu waliojuana nao. 45 Lakini kwa kuwa hawakumwona, wakarudia tena Yerusalema kumutafuta. 46 Nyuma ya siku tatu, wakamukuta ndani ya hekalu, akiikaa katikati ya walimu wakubwa wa Sheria, akiwasikiliza na kuwauliza maulizo. 47 Na wote waliomusikia walishangaa kuona akili yake na majibu yake. 48 Wazazi wake walipomwona, wakashangaa sana. Mama yake akamwuliza: “Mutoto wangu, kwa nini umetufanyia kama hivi? Mimi na baba yako tulikutafuta tukiwa na wasiwasi.” 49 Yesu akawajibu: “Kwa nini mulinitafuta? Hamujui kwamba ninapaswa kuwa katika nyumba ya Baba yangu?” 50 Lakini hawakufahamu neno lile alilowaambia. 51 Basi Yesu akarudia Nazareti pamoja nao, akaendelea kuwatii. Na mama yake alichunga maneno haya yote katika moyo wake. 52 Na Yesu alizidi kuwa na hekima, na kuongezeka kimo na kuendelea kumupendeza Mungu na watu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo